TaSUBa YAZINDUA DAWATI LA JINSIA


TAASISI ya Sanaa na Utamaduni Bagamoyo (TaSUBa) Mei 17, 2023 imezindua dawati la jinsia ili kutimiza malengo ya Serikali ya kupunguza na kumaliza kabisa vitendo vya ukatili wa kijinsia katika vyuo na jamii yote nchini.

Akizungumza katika hafla ya uzinduzi wa Dawati hilo Mwenyekiti wa Kampeni ya Shujaa wa Maendeleo na Ustawi wa Jamii Tanzania (SMAUJATA) Bi. Irene Mashine ambae ndiye alikua mgeni rasmi amesema, hivi sasa kumekuwa na ongezeko kubwa la matukio yanayohusiana na unyanyasaji wa kijinsia na mashambulio ya aibu ambayo mengine yanahusisha hata wanafamilia.

Bi. Mashine amewataka wajumbe wa dawati kutunza siri na kutoa msaada unaostahili kwa waathiriwa wa unyanyasaji huo ili kujenga jamii iliyo bora.

"Dawati hili la jinsia liwe chachu katika kutokomeza ukatili wa kijinsia hapa chuoni na sehemu zingine," amesema Bi. Mashine.

Naye Kaimu Mkuu wa Chuo Bw. Gabriel Kiiza amesema uzinduzi wa Dawati la Jinsia kwa TaSUBa ni wa umuhimu mkubwa kwa sababu litatoa muongozo nini kifanyike kukomesha vitendo hivyo kulingana na miongozo ya Serikali.

"Hivyo sisi kuzindua dawati hili, inatupa nafasi kubwa ya kuendelea kuwahimiza vijana kuepuka matendo yanayoashiria ukatili wa kijinsia," amesema Bw. Kiiza.

Mwenyekiti wa dawati hilo Bi. Perpetual Katondo amezitaja njia zitakazotumika kupata taarifa za unyanyasaji wa kijinsia kuwa ni pamoja na mlengwa au mtu aliyeshuhudia ukatili kufika moja kwa moja kwenye ofisi za dawati, kupiga simu kupitia namba ya wazi ambayo mtu yeyote anaweza kupiga na kutoa taarifa au kwa njia ya sanduku la maoni.

Hatua ya uzinduzi wa dawati hilo ni utekelezaji wa agizo la Serikali kupitia Wizara ya Maendeleo ya Jamii, Jinsia , Wanawake na Makundi Maalum kwa lengo la dawati kuwa na majukumu ya kutokomeza aina zote za ukatili maeneo ya vyuo.

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527

0/Post a Comment/Comments