MBUNGE CHIKOTA AITAKA SERIKALI KUJENGA VITUO VYA AFYA MNONGODI NA NYUNDO








Na Mwandishi Wetu

Mbunge wa Nanyamba (CCM), Abdallah Chikota amehoji serikali kuhusu fedha za ujenzi wa vituo vya afya katika Kata za Mnongodi na Nyundo.


Akiuliza swali bunge leo, Chikota amehoji serikali katika bajeti ya TAMISEMI iliyopitishwa ya ujenzi wa vituo vipya vya afya, inatoa tamko gani ujenzi wa vituo vya afya kata za kimkakati jimbo la Nanyamba.

Pia, amehoji kutokana na ujenzi wa kituo cha Kitaya kukamilika lini serikali itapeleka vifaa tiba na wataalamu ili huduma zitolewe.

Akijibu maswali hayo, Naibu Waziri Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (TAMISEMI), Deogratius Ndejembi, amesema serikali itaendelea kutenga fedha kwa ajili ya ujenzi wa vituo vya afya kwenye Kata za Kimkakati nchini ikiwa ni Mnongodi na Nyundo.

Ndejembi amesema katika mwaka wa fedha 2021/22 serikali ilitenga Sh.bilioni 117 kwa ajili ya ujenzi wa vituo vya afya vya kimkakati kwenye Kata 234 nchini.


“Halmashauri ya Mji wa Nanyamba ilitengewa kiasi cha Sh.milioni 500 kwa ajili ya ujenzi wa kituo cha afya Kitaya. Ujenzi wa Kituo hicho upo hatua ya ukamilishaji,”amesema.


Naibu Waziri huyo amesema katika mwaka 2023/24 serikali imetenga Sh.Milioni 400 kwa ajili ya ununuzi vifaa tiba vya zahanati na vituo vya afya kwenye mji huo.

Hata hivyo, amesema serikali itahakikisha inatenga fedha za vituo vya afya vya Nanyamba.

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553
Previous Post Next Post