KIKOKOTOO MWIBA MCHUNGU KWA WAFANYAKAZI MKOA WA PWANI

Katibu wa TUICO Mkoa wa Pwani Bi. Neema Wilbard
Mkuu wa wilaya ya Kibiti ,Kanali Joseph Kolombo

Na Elisante Kindulu - Chalinze

SHIRIKISHO la vyama vya wafanyakazi mkoa wa Pwani (TUCTA) limeishauri Serikali kurudisha kikokotoo cha zamani kwani kimewanyong'onyesha wafanyakazi katika utendaji wao wa kazi.


Hayo yalisemwa na Katibu wa TUICO Mkoa wa Pwani Bi. Neema Wilbard, alipokuwa akisoma risala ya shirikisho la vyama vya wafanyakazi (TUCTA) katika sherehe za Mei Mosi Mioa wa Pwani zilizofanyika mjini hapa.


"Suala la kikokotoo ni kidonda ndugu kwa wafanyakazi, kwani kiwango wanachopata wastaafu sasa Ni kidogo mno. Tunaiomba Serikali kuangalia upya Jambo hili kwani mioyo ya watumishi inasononeka kadri muda wa kustaafu unavyokaribia", alisema Katibu huyo.


Bi. Neema alizaja changamoto zingine zinazowakabiri wafanyakazi kuwa ni pamoja na mrundikano wa madeni ya mapunjo ya mshahara(arrears), fedha za mafunzo, likizo, matibabu, uhamisho na masaa ya ziada kazini.


Changamoto zingine Ni ucheleweshaji wa mafao kupitia mifuko ya hifadhi ya jamii ya PSSSF na NSSF, wingi wa Kodi na baadhi ya waajiri wa mashirika binafsi kukiuka sheria ya ajira kwa kutotoa mikataba ya ajira.


Naye Mratibu wa sherehe hizo ambaye pia Ni katibu wa chama cha walimu mkoa wa Pwani (CWT) Bi. Sekela Amosi aliwataka baadhiya waajiri kutoa zawadi zinazoendana na utendaji bora wa mfanyakazi ambapo kiwango kilichokubalika ni kuanzia thamani ya shilingi 500,000/=.


Akijibu risala hiyo ,Mkuu wa mkoa wa Pwani Bw. Aboubakari Kunenge aliyewakilishwa na Mkuu wa wilaya ya Kibiti Kanali Joseph Kolombo aliwataka waajiri wasihamishe watumishi kama hawana fedha za kuwalipa.

Aidha ameyataka majina ya makampuni yasiyotoa mikataba ya ajira mkoani Pwani yafike kwa mkuu wa mkoa ili kwa kushirikiana na maafisa Kazi kuweza kutatua changamoto hiyo.


Jumla ya wafanyakazi bora 252 kutoka mkoa wa Pwani walipewa zawadi za fedha, vifaa na vyeti ikiwa sehemu ya pongezi .

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527

0/Post a Comment/Comments