DKT. ABBASI: TUTAITANGAZA NCHI KWA VIWANGO VYA KIMATAIFA


Katibu Mkuu Wizara ya Maliasili na Utalii, Dkt. Hassan Abbasi, amesema nia kuu ya Wizara hiyo kwa sasa ni kufanya uhifadhi na kutangaza utalii kwa viwango vya kimataifa.

Dkt. Abbasi ameyasema hayo leo Aprili 1, 2023 alipotembelea Hifadhi ya Taifa ya Mikumi na kukutana na viongozi wa hifadhi hiyo iliyopo Morogoro ambapo pia aliendesha kikao cha Kamati ya Utekelezaji ya Mradi wa Kuendeleza Utalii wa Maeneo ya Kusini mwa Tanzania (Regrow).

“Tutahifadhi na baada ya kuhifadhi tutatangaza na maono ya viongozi wetu kwa sasa kupitia kwa Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan na Waziri wetu Mhe. Mohamed Mchengerwa ni kujipanga kuutangaza utalii wa Tanzania Kimataifa zaidi, niwaahidi tu kwamba hatutakiwa na jambo dogo,” alisema Dkt. Abbasi.

Ameongeza kuwa hizi ni zama za Royal Tour, akisisitiza kuwa kama Rais Samia alitoka na kuutangaza utalii wetu kwanini sisi tujifungie maofisini na kuwahimiza viongozi hao kutumia teknolojia za kisasa kuhifadhi na kutangaza utalii wetu.

“Kuna mtafiti mmoja pia ameonesha watu wengi nchini hawaendi kutalii kwasababu wana woga wa gharama na namna ya kufika kwenye maeneo husika.

“Tuanzishe vifurishi mbalimbali vya kuwavuta watalii wa ndani na nje, sikukuu zinakuja je tumejipanga vipi kutangaza vivutio vyetu, je watu wanajua bei zetu na kwanini tusiwe na vifurushi maalum kwa ajili ya hizi sikukuu, naamini tunaweza kupata watalii wengi kupitia hizi sikukuu,” alisisitiza.

Akiongoza Kikao cha ziada cha Kamati ya Uongozi ya Mradi wa REGROW, Dkt. Abbasi amesema mradi huo umechelewa kwa sababu mbalimbali na kuagiza kuwa kila taasisi husika ihakikishe kwa siku zilizobaki za mradi hakuna mkandarasi anaongezewa muda bila hoja zito na wasioweza waondolewe mapema kabla hata ya kusaini mikataba.

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527

0/Post a Comment/Comments