TANAPA KUHAMASISHA UTALII KWA MAKUNDI MAALUM




Na Dotto Kwilasa, DODOMA

SHIRIKA la Hifadhi za Taifa Tanzania (TANAPA)kwa kushirikiana na wanahabari wa utalii mkoani Dodoma kwa pamoja wameazimia kutoa elimu na kuhamasisha makundi maalumu  kuhusu utalii wa ndani hali itajayosaidia makundi hayo kuwa na taarifa sahihi za utalii.

Hatua hii imekuja ili kuunga mkono juhudi za Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Samia Suluhu Hassan kutangaza utalii wa ndani hivyo kuhakikisha makundi yote yanashirikishwa kukuza uchumi kupitia utalii kwa maendeleo ya Taifa.

Akiongea kwenye kikao maalumu na Waandishi hao jana Jijini Dodoma,Kamishna Msaidizi mwandamizi wa Jeshi la uhifadhi Ofisi ya TANAPA Dodoma Dkt.Noelia Myonga amesema uandishi wa habari za utalii unapaswa kwenda sambamba na makundi maalumu na kuleta chachu kwa jamii.

Amesema,ni muda mrefu sasa kumekuwa na harakati mbalimbali za kuhamasisha utalii kwa watu wanaojiweza na kusema kuwa sasa ni zamu ya kuangalia makundi maalumu na kuwapa haki sawa jambo ambalo linaenda sambamba na matakwa ya haki za binadamu.

"Serikali yetu inazingatia haki,hakuna ubaguzi na sisi kama TANAPA tukiwa na  dhamana ya hifadhi rasilimali nyingi za utalii tunataka kuanza kuyakumbuka makundi haya ,tuna Imani kupitia kwao jamii itaelewa umuhimu wa utalii 

Dkt.Myonga ameyataja makundi hayo kuwa ni pamoja na wazee, wasiojiweza,watu wenye ulemavu mbalimbali ikiwemo viziwi,walemavu wa viungo na wengine.

Kwa upande wake Mhifadhi Mkuu wa TANAPA Dodoma Frederick Malisa ameeleza juhudi zinazofanywa na Ofisi hiyo kuwa ni kuendelea kuhamasisha utalii wa ndani kwa kutoa elimu ya utalii hali itakayosaidia kuondoa taarifa zisizo sahihi zinazohusu utalii kwa wananchi.

Amesema jamii inapaswa kuelewa kuwa kila hifadhi ina kionjo chake hivyo kuwataka watanzania kwa ujumla kusherehekea mema ya nchi yao kwa kupanga muda kutembelea hifadhi zote 22 ikiwemo Kigosi,Kisiwa cha Saanane,Kitulo, mto Ugala na Ibanda-Kyerwa.

Akitolea mfano wa  hifadhi ya Burigi-Chato, Mhifadhi huyo amesema ni ya kujivunia kwa kuwa ina maziwa makubwa matano yenye mvuto duniani ikiwemo Burigi yenyewe na kutumia nafasi hiyo kuwashauri wadau wote wa maendeleo kuona haja ya kutembelea hifadhi zote kila mara.

Kutokana na hayo,baadhi ya wanahabari hao wa Utalii wameeleza kuwa wametia nia kutumia kalamu zao kuhamasisha jamii kufanya utalii wa ndani ili kukuza uchumi na kutangaza vivutito vyote.

Elizabeth Paul amesema ni wakati Sasa ambao dunia inapaswa kujua vivutio vilivyopo nchini hali itajayohamasisha watalii wengi zaidi kuzuru Tanzania na kuongeza mapato kwenye sekta ya utalii.



Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527

0/Post a Comment/Comments