MFUKO WA SELF MF UNAVYOTIMIZA NDOTO ZA WATANZANIA WA HALI YA CHINI

Na Dotto Kwilasa,DODOMA

ILI kukuza Mitaji itakayowezesha kuzifikia fursa zitakazoboresha maisha ya wananchi hususani wa pembezoni, Serikali kupitia Mfuko wa SELF Microfinance Fund (SELF MF)umetumia jumla ya shilingi bilioni 313 kuwezesha watanzania laki mbili na ishirini na tano elfu hali inayosaidia kuongeza kipato na kuondokana na umaskini.


Meneja Masoko na uhamasishaji wa SELF MF Linda Mshana amesema hayo Jijini hapa wakati akizungumza na Waandishi wa habari kuhusu huduma zinazotolewa na Mfuko huo na kuongeza kuwa ili kuboresha upatikanaji wa fedha mfuko huo unatoa huduma ya mikopo ya jumla na ya Mteja mmoja mmoja.


Amesema, Taasisi hiyo ikiwa imejikita kutoa huduma ya kubadili maisha ya watu na kutoa fursa ya kufanya kazi kwa kutoa mikopo kwa masharti nafuu inaendelea na utoaji wa elimu na mafunzo ya fedha ikiwa ni pamoja na kusaidia Taasisi kutengeneza na kuanzisha mifumo ya fedha.

"Kwa kuwa Mfuko wa SELF ni wa Serikali na uko chini ya Wizara ya fedha na mipango una jukumu la kutoa huduma za kifedha kwa wananchi wenye kipato cha chini ili kuwapa fursa ya kushiriki shughuli za uzalishaji mali ikiwa ni pamoja na kukuza mtaji na kuongeza wigo wa utoaji wa huduma za mikopo kwa wananchi,"amesema.


Kwa upande wake Meneja wa SELF MF Tawi la Dodoma Aristid Tesha aliitaja aina ya mikopo inayotolewa kuwa ni pamoja na mikopo ya kilimo, biashara,imarika,mtaji, mkulima, mikopo ya mishahara ,mkopo wa pamoja na mkopo wa makazi.


Alisema masharti ya mikopo ya Mfuko wa SELF MF ni pamoja na kuwa mjasiriamali mtanzania,uwe na dhamana au wadhamini ,uwe na nyaraka muhimu kuthibitisha uhalali Kutokana na aina ya mkopo pamoja na mkopaji kutakiwa kuwa na Ofisi ya kudumu.


"Sifa za mikopo ya Mfuko huu ni riba nafuu, kupokea mkopo ndani ya muda mfupi,marejesho rafiki na kiwango cha mkopo ni Kutokana na uhitaji wa mkopaji Kwa kuambatanisha viambatanisho vya awali ikiwemo Nida,leseni ya udereva,barua ya utambulisho wa Serikali za mitaa na leseni ya biashara.


Kutokana na hayo mmoja wa wanufaika wa mikopo ya Mfuko huo Aziza Nasib amesema ili kufikia uchumi wa kati na kitimiza malengo, wafanyabiasha ndogo ndogo wanapaswa kuchukua hatua ya kukopa kwenye Taasisi zinazoaminika.


Amesema biashara zenye malengo zinahitaji mtaji mkubwa hivyo kuwashauri wafanyabiashara kukuza biashara zao kupitia mikopo yenye riba nafuu.


"Nawashauri wafanyabiasha kutumia Mfuko wa SELF kukuza kipato kwa kuwa upo chini ya uangalizi wa Serikali na hauna ubabaishaji,"alisema mnufaika huyo ambaye kwa Sasa anamiliki kiwanda cha kusaga chupa.

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527

0/Post a Comment/Comments