JKT YASIKITISHWA PICHA YA VIJANA WAKE KUHUSISHWA NA WENYE VVU "WAOMBE RADHI, WAONDOE PICHA MARA MOJA'

 Mkuu wa tawi la utawala wa Jeshi la kujenga taifa Brigedia Jenerali Hassan Mabena akizungumza na Waandishi wa habari Jijini Dodoma kwenye ukumbi wa habari Maelezo.

Na Dotto Kwilasa, DODOMA

JESHI la kujenga Taifa (JKT) limesema limesikitishwa na habari ya vijana wa JKT 147 kuwa na maambukizi ya VVU na kuambatanishwa na picha ya vijana wengine wanaohudhuria mafunzo ya Jeshi hilo makambini ambao hawahusiani na idadi hiyo .

Aidha Jeshi hilo limesema jambo hilo ni udhalilishaji wa utu wa binadamu na kwamba suala la kutumia picha za vijana hao ambao hawahusiki katika habari hiyo ni cha ukosefu wa maadili ya uandishi wa habari .

Hatua hiyo imekuja kufuatia kuripotiwa kwa habari iliyoenea kwenye vyombo vya habari iliyotokana na ripoti ya Bunge kupitia Kamati yake ya Ukimwi mnamo Februari 3,2023 kuwa jumla ya vijana 147 Wana maambukizi ya VVU jambo lililosababisha vyombo vya habari kutumia picha isiyohusika na kuibua taharuki kwa jamii.

Akitolea ufafanuzi suala hilo kwenye vyombo vya habari leo Jijini Dodoma,Mkuu wa tawi la utawala wa Jeshi la kujenga taifa Brigedia Jenerali Hassan Mabena amevitaka vyombo vyote vya habari na mitandao ya kijamii vilivyoripoti habari hiyo kwa kuweka picha za vijana wa JKT ambao si wahusika wa habari hiyo kuomba radhi na kuondoa picha hiyo mara moja .

"JKT tumeumizwa na taswira hiyo kwa sababu vijana hao hawahusiani na habari hiyo, ufafanuzi ni kwamba mafunzo ya vijana wa kundi la lazima ambao ni wahitimu wa kidato cha sita huendeshwa kwa kipindi cha miezi mitatu ambapo kabla ya kuanza mafunzo hufanyiwa usahili wa nyaraka zao pamoja na vipimo vya afya kufahamu utimamu wa mwili,"amesema

Pamoja na hayo Brigedia Jenerali Mabena amesema vijana ambao majibu ya vipimo vyao kuwa na changamogo za kiafya hufanya mafunzo yao chini ya uangalizi wa wakufunzi ili kuhakikisha wanamaliza mafunzo salama bila msongo wa mawazo.

"Kwa kuwa hili ni kundi la lazima,vijana Wenye ulemavu wa kuonekana kwa macho hupokelewa katika kikosi cha Ruvu JKT ambacho kina miundombinu ya kuhudumia watu wa jamii hiyo,"amesema na kuongeza;

JKT inasisitiza kuwa kigezo cha afya kwa vijana hao wa kundi la lazima wanaokuja makambini wakiwa na changamogo za kiafya kinazingatiwa kwa kuwaweka chini ya uangalizi na si vinginevyo. 

"JKT tunazingatia sheria,kanuni na taratibu za kitabibu sambamba na kuzingatia Mila na desturi za nchi yetu katika kutekeleza jukumu lake la msingi la malezi ya vijana,Umma unapaswa kufahamu kuwa mafunzo ya JKT ni salama na yenye kuzingatia miongozo ya malezi ya vijana,"amesisitiza

Kutokana na hayo Msemaji wa Serikali ambaye pia ni Mkurugenzi wa habari Maelezo Gerson Msigwa amevitaka vyombo vyote vya habari ambavyo vilitumia picha isiyohusika na haiendani na habari ya hao vijana 147 wa JKT wevye VVU kuomba radhi Kwa Umma kwani ni ukiukwaji wa haki za binadamu.

Msigwa amesema kutokana na vyombo hivyo kutumia picha ya vijana ambao hawahusiki,baadhi ya vijana hao wanaoonekana kwenye picha mitandaoni wanaweza kuathirika kisaikolojia na kujihisi kutengwa na jamii yao.

"Sote tunafahamu kuwa katika habari hii uhuru wa vyombo vya habari haukuzingatiwa, lazima wahusika waombe radhi ili kuwaweka salama vijana wetu,"amesisitiza Msigwa.

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527

0/Post a Comment/Comments