VITUO VYA TAARIFA NA MAARIFA VYATOA MAPENDEKEZO KUHUSU BAJETI YA HALMASHAURI YA JIJI LA DAR ES SALAAM


Veronica Wana kutoka Kituo cha Taarifa na Maarifa cha Kivule akisoma maoni na mapendekezo katika eneo la masuala mtambuka ya Jinsia hasa kwenye vipaumbele muhimu kwenye upangaji wa Bajeti yenye mrengo wa Usawa wa Kijinsia kwa wadau wa Usawa wa Kijinsia(Bajeti Jumuishi) kwenye Bajeti ya Halmashauri ya Jiji la Dar es Salaam
Mwanakituo wa Kituo cha Taarifa na Maarifa cha Majohe Rehema Shunda akisoma uwasilishwaji wa Bajeti ya Halmashauri ya Jiji la Dar es Salaam kwenye sekta ya kilimo, uvuvi na mifugo pamoja na mapendekezo ya kisera kwa Halmashauri kwenye sekta ya kilimo wakati uwasilishwaji wa mapendekezo ya vipaumbele muhimu kwenye upangaji wa Bajeti yenye mlego wa Usawa wa Kijinsia kwa wadau wa Usawa wa Kijinsia(Bajeti Jumuishi) kwenye Bajeti ya Halmashauri ya Jiji la Dar es Salaam
Mwanakituo wa Kituo cha Taarifa na Maarifa cha Kipunguni Tausi Msangi akisoma kuhusu hali ya Bajeti ya Halmashauri ya Jiji la Dar es Salaam kwa mwaka wa fedha wa 2022/23 pamoja na Mapato ya Jiji hilo wakati uwasilishwaji wa mapendekezo ya vipaumbele muhimu kwenye upangaji wa Bajeti yenye mrengo wa Usawa wa Kijinsia kwa wadau wa Usawa wa Kijinsia(Bajeti Jumuishi) kwenye Bajeti ya Halmashauri ya Jiji la Dar es Salaam
Katibu wa Kituo cha Taarifa na Maarifa cha Kivule Erick Anderson akisoma utangulizi wa Uchambuzi wa Mapitio ya Bajeti ya Halmashauri ya Jiji la Dar es Salaam kwa miradi ya maendeleo kwa mwaka wa fedha wa 2022/23 kwa kuzingatia vipaumbele vya wanajamii kwa mtazamo wa usawa wa kijinsia


*****




Vituo vya Taarifa na Maarifa kata za Kipunguni, Kivule, Zingiziwa na Majohe vimetoa mapendekezo ya vipaumbele muhimu kwenye upangaji wa Bajeti yenye mlego wa Usawa wa Kijinsia kwa wadau wa Usawa wa Kijinsia(Bajeti Jumuishi) kwenye Bajeti ijayo ya Halmashauri ya Jiji la Dar es Salaam ya mwaka 2023/24 ili kuweza kunufaisha wanajamii kwa ujumla.


Wamesema kipaumbele cha kwanza ni Viwanda vya kuongeza thamani ya mazao ya kilimo, mifugo na uvuvi ili mazao yaliyolimwa katika maeneo mbalimbali ya Ilala yanahitaji kuongezewa thamani kama mboga mboga na matunda zinazolimwa katika Eneo la Kituo cha Kilimo la Kinyamwezi litumike pia kama kiwanda cha wananchi cha kuzalisha bidhaa mbalimbali za kilimo na kuzitafutia masoko ndani na nje ya nchi.


Pia katika Ukuaji wa Uchumi na Maendeleo ya Watu wamesema bado kuna ombwe kubwa kati ya hali halisi ya Jamii na dhana ya ukuaji wa uchumi kwa kuzingatia kwamba uchumi unatakiwa kugusa maisha ya watu moja kwa moja hivyo basi tunapendeleza serikali kuwekeza zaidi kwenye Nyanja za uchumi mdogo wa watu hasa katikia uzalishaji na masoko.


Wamesema Jiji la Dar es Salaam lifanye maboresho ya mfumo wa kusajili viwanda vidogo na kuondoa tozo au kuboresha mlolongo wa kupata usajili ili kuwezesha kuanzishwa kwa viwanda vingi vya wanawake vya usindikaji kwani wazalishaji wa Bidhaa za kilimo kama viungo hawapati usajili wa Mamlaka ya Viwango Tanzania (TBS) kwa urahisi, hii imechangia kuzagaa kwa bidhaa nyingi za wajasiriamali wadogo mitaani ambazo hazijafanyiwa vipimo na uhakiki kutokana na urasimu wa TBS kupata usajili na tozo kubwa za kulipia.


Wamesisitiza kuwa ni muhimu sana kutenga bajeti ya kusimamia utekelzaji na kufuatilia Mpango Kazi wa Taifa wa Kutokomeza Ukatili wa Kijinsia kwa wanawake na watoto (MTAKUWWA1) na kuweka nguvu katika kuharakisha uandwaaji wa Mpango wa II kwa kuwa Halmashauri nyingi hazilipi suala la Ukatili wa Kijinsia kipaumbele, licha ya kutumia fedha nyingi kwenye miradi ya maendeleo hasa sekta ya elimu bado hakuna jitihada za dhati kuzuia kabisa au kutokomeza Ukatili wa Kijinsia kama ulinzi wa mtoto wa kike asibakwe, kukeketwa, kuolewa au kupata ujauzito.


Pia huduma za ustawi wa jamii kwa Jiji la Dar es salaam haithaminiwi na kuwekewa rasilimali fedha na Bajeti ya kutosha ya kukabiliana na vitendo vya Ukatili wa Kijinsia hivyo wamependekeza kuongezwa kwa fedha kwa ajili ya kuwezesha dawati la ustawi wa Jamii ili kufanya kazi zao kwa ufanisi ili kuwawezesha manusura wa Ukatili wa Kijinsia kupata huduma za uokozi kwa haraka.


Kutokana na kutokuwepo kwa uelewa mpana juu ya masuala ya Kijinsia kwa watunga sera, wataalamu na watendaji wametoa ushauri kwa afisa jinsia wa Halmashauri aandae utaratibu wa mafunzo ya Jinsia na bajeti yenye mlengo wa Kijinsia kwa Halmashauri ili wataalamu kutoka Mtandano wa Jinsia Tanzania (TGNP) waweze kutoa elimu hiyo.


Wamesisitiza kuwa bado viongozi na watendaji wengi hawazingatii umuhimu wa kutenga fedha kwenye bajeti kwaajili ya kutoa taulo za kike kwa wanafunzi walioko mashuleni hasa wanaotoka kwenye familia masikini kwani Fedha zilizotengwa kwa Halmashauri ya Jiji kwa mwaka wa fedha 2022/23 hazijatolewa kwa lengo hilo, na sehemu ya fedha zimetumika kwa matumizi mengine hivyo wameshauri wasichana walioko mashuleni wapatiwe taulo ili waweze kushiriki kikamilifu masomo wanapokuwa kwenye hedhi, ili kuongeza ufaulu kwa wasichana.

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527

0/Post a Comment/Comments