WALENGWA WA TASAF KATA YA RUSIMBI KIGOMA UJIJI WATAKIWA KUBORESHA MAISHA YAO


Naibu Waziri, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Mhe. Deogratius Ndejembi akizungumza na wananchi wa Kata ya Rusimbi, Mtaa wa Kawawa na Taifa mkoani Kigoma wakati wa ziara yake ya kikazi ya kukagua utekelezaji wa Mpango wa Kunusuru Kaya Maskini kwenye Halmashauri ya Wilaya ya Kigoma.

Wananchi wa Kata ya Rusimbi, Mtaa wa Kawawa na Taifa mkoani Kigoma wakimsikiliza Naibu Waziri, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Mhe. Deogratius Ndejembi (Wakwanza kulia) wakati akizungumza nao alipokuwa kwenye ziara yake ya kikazi ya kukagua utekelezaji wa Mpango wa Kunusuru Kaya Maskini kwenye Halmashauri ya Wilaya ya Kigoma.


Mkuu wa Wilaya ya Kigoma, Mhe. Ester Mahawe akimkaribisha Naibu Waziri, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Mhe. Deogratius Ndejembi kuzungumza na wananchi wa Kata ya Rusimbi, Mtaa wa Kawawa na Taifa mkoani Kigoma wakati wa ziara ya kikazi ya Naibu Waziri huyo yenye lengo la kukagua utekelezaji wa Mpango wa Kunusuru Kaya Maskini kwenye Halmashauri ya Wilaya ya Kigoma.


Mwakilishi wa Mkurugenzi Mtendaji wa TASAF, Bi. Catherine Kisanga akielezea utekelezaji wa majukumu ya TASAF katika Halmashauri ya Mkoa wa Kigoma wakati wa ziara ya kikazi ya Naibu Waziri, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Mhe. Deogratius Ndejembi yenye lengo la kukagua utekelezaji wa Mpango wa Kunusuru Kaya Maskini kwenye Halmashauri hiyo.

***************************

Na. Veronica Mwafisi - Kigoma

Tarehe 15 Novemba, 2022

Naibu Waziri, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Mhe. Deogratius Ndejembi amewataka walengwa wa TASAF Kata ya Rusimbi, Mtaa wa Kawawa na Taifa kuboresha maisha yao kupitia ruzuku wanayoipata ili kutomuangusha Mhe. Rais Samia Suluhu Hassan ambaye amefanya jitihada za kutafuta fedha na kuongeza muda wa kutekeleza Mpango wa Kunusuru Kaya Maskini nchini hadi kufikia mwaka 2025 badala ya mwaka 2023 ambao ndio ulikuwa ni ukomo wa utekelezaji wa mpango huo.

Mhe. Ndejembi ametoa wito huo, kwa wananchi na walengwa wa TASAF wa Kata ya Rusimbi Kigoma Ujiji, wakati wa ziara yake ya kikazi ya kukagua utekelezaji wa Mpango wa Kunusuru Kaya Maskini katika Halmashauri ya Wilaya ya Kigoma.

Mhe. Ndejembi amesema, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Samia Suluhu Hassan amefanya jitihada za kutafuta fedha na kuongeza muda wa kutekeleza mpango wa TASAF, ili kuwasaidia watanzania kutoka katika hali duni ya maisha na kuwa na maisha bora.

Mhe. Ndejembi ameongeza kuwa, Mhe. Rais Samia Suluhu Hassan kwa upande wake ameshatekeleza wajibu wake kwa kuwajali wananchi ambao ni walengwa wa TASAF na ndio maana utekelezaji wa mpango wa TASAF utaendelea hadi mwaka 2025, hivyo umebakia wajibu wa walengwa wa TASAF kuhakikisha wanaboresha maisha yao na kumuunga mkono Mhe. Rais kuliletea taifa maendeleo.

Kwa upande wake, Mratibu wa TASAF Manispaa Kigoma Ujiji Bw. Isaac Vyabandi amemueleza Mhe. Ndejembi kuwa, TASAF imekuwa ni chachu ya maendeleo ya kiuchumi kwa wananchi wenye kipato cha chini mkoani humo, na kuongeza kuwa tangu mwaka 2014 ambapo mpango huo ulianza kutekelezwa katika Manispaa ya Kigoma Ujiji jumla ya shilingi bilioni 15 zimepokelewa na kuwanufaisha walengwa.

Mkoa wa Kigoma ni miongoni mwa mikoa ambayo imenufaika na ruzuku inayotolewa kupitia Mpango wa Kuzinusuru Kaya Maskini nchini, unaoratibiwa na Mfuko wa Maendeleo ya Jamii (TASAF).

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527

0/Post a Comment/Comments