DART YATAKIWA KUDHIBITI UVUJAJI WA MAPATO KWA KUIMARISHA USIMAMIZI WA MIFUMO

Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (TAMISEMI) Mhe. Angellah Kairuki akimsikiliza Mkurugenzi Mtendaji wa DART Dkt. Edwin Mhede katika ziara yake ya kukagua miundominu ya Usafiri wa Mabasi yaendayo haraka (DART) leo Oktoba 12,2022 Jijini Dar es Salaam. Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (TAMISEMI) Mhe. Angellah Kairuki akishuka kwenye basi la DART akiongozana na Mkurugenzi Mtendaji wa DART Dkt. Edwin Mhede katika ziara yake ya kukagua miundominu ya Usafiri wa Mabasi yaendayo haraka (DART) leo Oktoba 12,2022 Jijini Dar es Salaam. Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (TAMISEMI) Mhe. Angellah Kairuki akimsikiliza Mkurugenzi Mtendaji wa DART Dkt. Edwin Mhede wakiwa ndani ya basi ya DART katika ziara yake ya kukagua miundominu ya Usafiri wa Mabasi yaendayo haraka (DART) leo Oktoba 12,2022 Jijini Dar es Salaam. Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (TAMISEMI) Mhe. Angellah Kairuki akimsikiliza Mkurugenzi Mtendaji wa UDART Bw.John Nguya mara baada ya kutembelea depot ya DART Jangwani Jijini Dar es Salaam katika ziara yake ya kukagua miundominu ya Usafiri wa Mabasi yaendayo haraka (DART) leo Oktoba 12,2022 Jijini Dar es Salaam.

(PICHA ZOTE NA EMMANUEL MBATILO)

********************

WAZIRI wa Nchi Ofisi ya Rais Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (TAMISEMI) Mhe. Angellah Kairuki amewaagiza Wakala wa Mabasi Yaendayo Haraka (DART) kuhakikisha inadhibiti uvujaji wa mapato kwa kuweka mifumo mizuri inayoweza kuzuia tatizo hilo.

Ametoa rai hiyo leo Oktoba 12, 2022 wakati wa ziara yake ya kukagua miundombinu,karakana na maeneo mengine yaliyo chini ya DART, jijini Dar-es-salaam na kuupongeza Wakala huo kwa hatua mbalimbali zilizochukuliwa za kudhibiti mapato na kuutaka kuongeza jitihada zaidi ili kuhakikisha mapato ya Serikali hayapotei

“Hakikisheni mifumo yenu ni salama hakuna mianya na kuhakikisha inakaguliwa ili kupunguza mianya ya upotevu wa mapato kwenye vituo vya kukatia tiketi” amesisitiza Waziri Kairuki

Amesema kuwa kweye TEHAMA kumekuwa na changamoto nyingi, hivyo amewaelekeza kufanya ukaguzi na mapitio ya mara kwa mara ya mifumo kwa lengo la kujiridhisha kwenye suala la ukusanyaji wa mapato.

Pamoja na hilo pia Waziri Kairuki ametoa onyo kali kwa wananchi wote wanaoingilia miundombinu ya Mabasi hayo yaendayo haraka huku akisisitiza kuwa kuanzia sasa Serikali haitakuwa na 'Msalie Mtume' kwa yeyote atakayekiuka agizo hilo.

Amesema wakati Serikali ikisubiri ujio wa mfumo mpya wa unaotarajia kufungwa katika kipindi cha wiki 16 kuanzia sasa, sambamba na tiketi zilizopo sasa za usafiri wa mabasi hayo kuunganishwa na mifumo ya TRA, DART inapaswa kuwa na njia zaidi ili kulinda mapato hayo.

"Mhakikishe hakuna uvujaji wa mapato kwa kuipitia mara kwa mara mifumo yote na kujiridhisha kuwa ipo salama, pia muendelee kuifanyia ukaguzi na mapitio mifumo yote ya TEHAMA ili kuilinda dhidi ya upotevu huo wa mapato hayo" amesisitiza Waziri Kairuki.

Aidha, amemshukuru Rais Samia Suluhu Hassan kwa kuona umuhimu wa mradi huu wenye mabasi yapatayo 240 hadi sasa ikitoa huduma kwa wananchi zaidi ya 90,000 hadi 210,000 kwa siku na kuutaka Wakala huo kuhakikishe huduma zinazotolewa zinakidhi mahitaji ya wananchi

Vilevile, Waziri Kairuki ameuagiza Wakala wa Mabasi Yaendayo Haraka kuhakikisha inawaondolea usumbufu wananchi kwa kukaa muda mrefu vituoni wanaposubiri kupata huduma ya mabasi hayo kwa kuweka mifumo stahiki.

Aidha, amesema uwepo wa mfumo wa tiketi za kusafiria ambao hapo awali ulitanguliwa na mfumo wa kadi uzingatie muda wa utoaji huduma ili kuwaondolea usumbufu wananchi wa kukaa muda mrefu zaidi vituoni huku akiitaka kujiongeza hasa katika suala la matumizi ya mafuta.

Kwa upande wake Mkurugenzi Mtendaji wa DART Dkt. Edwin Mhede mbali na kumshukuru Waziri kwa kuwatia moyo katika eneo zima la utendaji wa taasisi hiyo na kuahidi kuwa changamoto zote zinazowakabili watazifanyia kazi ili kuboresha huduma wanazotoa.

Alisema wao kama DART lengo lao ni kuona huduma wanazozitoa zinakuwa zenye viwango bora ili kumfanya kila mwananchi aweze kuridhika nazo na hivyo kufikia matakwa ya kuanzishwa kwa wakala huyo.

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527

0/Post a Comment/Comments