WASIOJULIKANA WAUA MLINZI NA KUIBA MCHELE MASHINENI DIDIA - SHINYANGA


Mfano wa mchele

Na Kadama Malunde - Malunde 1 blog

Mwanaume aliyejulikana kwa jina la Jofrey Justine (45) anadaiwa kuuawa kwa kunyongwa na watu wasiojulikana wakati akiendelea na kazi ya ulinzi katika mashine ya kusaga na kukoboa nafaka katika kitongoji cha Majengo kijiji cha Didia kata ya Didia wilaya ya Shinyanga mkoani Shinyanga.

Watu hao pia waliiba mchele kilo 500 wenye thamani ya shilingi Milioni moja na laki 2.

Kwa mujibu wa mashuhuda waliozungumza na Malunde 1 blog, tukio hilo limetokea usiku wa kuamkia Jumamosi Septemba 24,2022 ambapo pamoja na kufanya mauaji hayo watu hao wasiojulikana waliondoka na kilo 500 za mchele na kutokomea kusikojulikana.

Akielezea kuhusu tukio hilo, Mwenyekiti wa Kijiji cha Didia Mrisho Hamad amesema mlinzi huyo ambaye ni mwenyeji wa Karagwe mkoani Kagera alikutwa ameuawa siku ya Jumamosi asubuhi.

“Nilipigiwa simu majira ya saa 2 asubuhi nikaambiwa kuna mtu amefariki dunia kwenye Mashine ya mzee Richard. Nilifika eneo la tukio tukakuta mwili wa marehemu umelazwa nyuma ya mashine. Hatukuona majeraha ila tuliona tu damu kidogo mdomoni”,ameeleza Mwenyekiti huyo wa kijiji akizungumza na Malunde 1 blog

“Kwenye hiyo mashine tukaona kuna sehemu ilikuwa imetobolewa na kubaini kuwa kuna upotefu wa magunia matano ya mchele yenye kilo 100. Nikawapigia simu polisi wakaja, wakauchukua mwili wa marehemu”,ameongeza Hamad.

Kamanda wa Jeshi la Polisi Mkoa wa Shinyanga ACP, Janeth Magomi amethibitisha kutokea kwa tukio hilo na kueleza kuwa wanaendelea kufanya upelelezi ili kuwabaini watu waliohusika kwenye tukio hilo la mauaji na wizi wa mchele kilo 500.

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527

0/Post a Comment/Comments