WANANCHI WATAKIWA KUCHUKUA HATUA KUKABILI UKATILI WA KIJINSIA


Mratibu wa vituo vya taarifa na maarifa kutoka TGNP Flora Ndaba akizungumza katika mdahalo wa kupinga ukatili wa klijinsia uliofanyika kijiji cha Titye wilaya ya Kasulu mkoani Kigoma. (Picha zote na Fadhili Abdallah)
Mratibu wa vituo vya taarifa na maarifa kutoka TGNP Flora Ndaba akizungumza katika mdahalo wa kupinga ukatili wa klijinsia uliofanyika kijiji cha Titye wilaya ya Kasulu mkoani Kigoma.
Polisi kata katika kata ya Titye wilaya ya Kasulu mkoani Kigoma Mkaguzi wa polisi Bwire akizungumza katika mdahalo wa kupinga vitendo vya ukatili na unyanyasaji kijinsia uliofanyika kijiji cha Titye wilaya ya Kasulu mkoani Kigoma
Polisi kata katika kata ya Titye wilaya ya Kasulu mkoani Kigoma Mkaguzi wa polisi Bwire akizungumza katika mdahalo wa kupinga vitendo vya ukatili na unyanyasaji kijinsia uliofanyika kijiji cha Titye wilaya ya Kasulu mkoani Kigoma
Viongozi wa kijiji na kata ya TITYE wakifuatilia mdahalo wa kupinga ukatli wa kijinsia ulioandaliwa na Mtandao wa jinsia Tanzania (TGNP).
Wananchi wa kijiji cha Titye Halmashauri ya wilaya ya Kasulu mkoani Kigoma wakifuatilia mdahalo wa kupinga ukatili wa kijinsia ulioandaliwa na TGNP.


Na Fadhili Abdallah,Kigoma

WITO umetolewa kwa jamii ya watanzania kuchukua hatua sasa katika kukabiliana na tatizo la ukatili wa kijinsia na watoto kwa kuamua kwa dhati kupambana na vitendo vya ukatili vinavyotokea kwenye maeneo yao.

Mratibu wa vituo vya taarifa na maarifa kutoka Mtandao wa jinsia Tanzania (TGNP),Flora Ndaba alisema hayo katika mdahalo wa wananchi wa kupambana na ukatili uliofanyika kwenye kijiji cha Titye wilaya ya Kasulu mkoani Kigoma.

Mratibu huyo alisema kuwa serikali na mashirika yanasaidia kukabili jambo hilo kwa kusimamia sera, sheria na taratibu za kisheria lakini katika kuhakikisha matukio yanakoma jamii inapaswa kuwa ndiyo mtekelezaji mkuu kutokana na matukio hayo kutokea kwenye maeneo yao.

Mafunzo, elimu na uhamasishaji umeshafanyika sana lakini bado wananchi wanionyoshea kidole serikali wakati wanao wajibu na jukumu kubwa katika kusimamia ukomeshaji wa vitendo hivyo.

“Ukiangalia vitendo vya ubakaji, ulawiti, mimba za utotoni kwa wananfunzi, vipigo kwa wanawake na unyanyasaji mwingine vyote vinatokea kwa watu wa familia wenye mahusiano ambao ndiyo wanapaswa kuwa walinzi wa watoto na familia zao",alisema Flora Ndaba kutoka TGNP.

Alisema kuwa serikali na mashirika wanatoa elimu na kuhamasisha kutokomeza ukatili kwa sababu inataka kuwaelimisha kujua wajibu wao kwamba suala la ulinzi, matunzo na malezi ya familia yanaanza kwa baba na mama ambao wanapaswa kusimamia jukumu lao jambo ambalo litasaidia kukabili vitendo vya ukatili kwa kiasi kikubwa.

Kwa upande wake Afisa Maendeleo ya jamii Halmashauri ya wilaya Kasulu, Maria alisema kuwa familia kwa kutumia serikali za vijiji ndiyo msingi wa kuzuia ukatili wa kijinsia kwa kuweka mipango ambayo wataitekeleza na kuondoa changamoto hizo,

Pamoja na hilo Maria alisema kuwa utoaji wa taarifa kwa wanajamii kwenda kwenye vyombo vya ulinzi na serikali ni muhimu ili hatua ziweze kuchukuliwa lakini wananchi wamekuwa waoga kutoa taarifa na wakati mwingine kushiriki kuwaficha wahalifu ili wasichukuliwe hatua wengi wakiwa ndugu wa karibu wanaohusika na matukio hayo.

Hata hivyo kwa upande wao wananchi wa kijiji cha Titye akiwemo Mussa Ndofu ambao wamesema kuwa licha ya kuripotiwa kwa vitendo vya ukatili na mimba kwa wanafunzi lakini inashangaza kuona watuhumiwa wakikamatwa na baadaye kuachiwa bila kufanywa lolote.

Naye Isaya Haminimana alisema kuwa wanafunzi wa shule za msingi na sekondari wanapewa ujauzito na walimu lakini hakuna hatua zinazochukuliwa kwa wanafunzi kuacha masomo na walimu wanaendelea kufundisha bila kufanya lolote.

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527

0/Post a Comment/Comments