BASHUNGWA AAGIZA MAAFISA ELIMU KUBORESHA MIUNDOMBINU KWA WANAFUNZI WENYE MAHITAJI MAALUM

WAZIRI wa Nchi Ofisi ya Rais Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa, Innocent Bashungwa akiongea kwenye mkutano mkuu wa mwaka wa Maafisa  Elimu Maalum Tanzania Bara (UMEMTA) leo Juni 20,2022 Jijini Dodoma.


 Na Mwandishi wetu,OR - TAMISEMI 

WAZIRI wa Nchi Ofisi ya Rais Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa Innocent Bashungwa amewaagiza Maafisa Elimu wote nchi nzima kuendelea kuijengea jamii uelewa kuhusu upatikanaji wa elimu kwa watoto wenye mahitaji maalum na kuboresha miundombinu na mazingira ya kujifunzia na kufundishia katika shule ili ziwe rafiki kwa wanafunzi wote wakiwemo wanafunzi wenye mahitaji maaalum. 

Ametoa agizo hilo  Juni 20, 2022 Jijini Dodoma wakati akifungua mkutano mkuu wa mwaka wa Maafisa  Elimu Maalum Tanzania Bara (UMEMTA) na kuzielekeza Halmashauri zote nchini kuwapa ushirikiano Maafisa Elimu Maalum wakati wanapotekeleza majukumu yao ili kuimarisha huduma kwa wanafunzi wenye mahitaji maalum nchini.

Amesema Serikali imekuwa ikifanya jitihada mbalimbali kuhakikisha utoaji wa elimu kwa watu wenye ulemavu kwa kuwabaini na kuhakikisha wanaandikishwa kujiunga na ElimuMsingi ambapo kwa mwaka 2022, Watoto 16,377 walibainika na kuandikishwa kwenye shule stahiki. 

Bashungwa amesema, Serikali  imeboresha miundombinu kwa kuwajengea mabweni 50 wanafunzi wa shule za msingi yenye gharama ya shilingi 4,000,000,000/, kununua vifaa na Visaidizi Maalum vyenye thamani ya shilingi billioni 4.5 ili kuhakikisha kuwa wanafunzi wenye mahitaji maalum wanapewa fursa ya kupata elimu kwa faida yao, jamii na nchi.

Aidha, Bashungwa ameelekeza uteuzi wa viongozi wa elimu katika ngazi za shule, kata, halmashauri na mikoa uzingatie umahiri na uzoefu wa wasimamizi wa elimu ili kuleta tija katika usimamizi wa ufundishaji shuleni.

Ameagiza ifikapo mwishoni mwa julai 2022, uundwe mkakati wa kuboresha elimu ili kuongeza namna bora ya utekelezaji wa mitaala nchini katika kuizibainisha changamoto zilizopo na kuleta ufumbuzi wa nini kifanyike sasa kuimarisha ufundishaji na ujifunzaji.

Vile Vile, amemuagiza Katibu Mkuu wa Ofisi ya Rais - TAMISEMI ndani ya siku 7 kuwataka Maelezo Wakurugenzi wote ambao hawajaruhusu Maafisa Elimu Maalum kuhudhulia Mkutano huo Pia, Wakurugenzi wahakikishe wanalipa madeni na posho za kudhurulia mafunzo ya Maafisa  elimu Maalum na sio kuwakopa.

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527

0/Post a Comment/Comments