WALIMU WATAKIWA KUTUMIA FURSA YA PROGRAM YA MAFUNZO ENDELEVU


Mkurugenzi wa halmashauri ya Arusha Seleman Msumi akifungua semina ya mafunzo ya walimu iliyofanyika katika halmashauri hiyo.


Na Rose Jackson,Arusha

Walimu halmashauri ya Arusha, wametakiwa kutumia fursa inayotolewa na serikali ya kupitia programu ya Mafunzo Endelevu kwa Walimu Kazini (MEWAKA), mafunzo yenye lengo la kuboresha utalamu kitaaluma kwa walimu, ili kuwa mahiri katika mbinu za ufundishaji zinazoendana na wakati.

Rai hiyo imetolewa na Mkurugenzi Mtendaji, halmashauri ya Arusha, Seleman Msumi, wakati akifungua semina ya Mafunzo ya Walimu Kazini, iliyojumuisha walimu wakuu wa shule za msingi pamoja na Maafisa Elimu wa kata zote za halamshauri hiyo, semina iliyofanyika kwenye Ukumbi wa shule ya Msingi Green Acress.

Mkurugenzi Msumi, amewataka walimu hao, kutumia fursa hiyo, inayotolewa na serikali kuhakikisha wanapanga muda wa kujifunza zaidi kupitia miongozo na utaalam uliotolewa kwenye moduli za MEWAKA, mafunzo ambayo yatawawezesha kupata maarifa mapya na mbinu shirikishi za ufundishaji, pamoja na kufanya tathmini kwa wanafunzi.

"Serikali inatambua na inathamini kazi kubwa inayofanywa na walimu, na kuona umuhimu wa kuandaa mkakati wa MEWAKA, utakowewezesha kapata mafunzo kazini, hivyo nitoe wito kwenu viongozi wa shule, kuratibu na kusimamia mpango huo katika maeneo yenu ya kazi, ili kufikia malengo ya serikali ya kuinua kiwango cha taaluma shuleni" amesisitiza Mkurugenzi Msumi.

Naye Afisa Elimu Msingi halmashauri ya Arusha, Salvatory Alute, amefafanua kuwa, lengo la semina hiyo kwa viongozi hao wa elimu ngazi ya kata na shule ni kuwajengea uwezo wa kuratibu na kusimamia programu ya MEWAKA katika maeneo yao ya kazi, ikiwa ni pamoja na kuwawezesha kuwa wathibiti ubora wa ndani ya shule, kufuatilia utekelezaji wa MEWAKA na kufanya tathmini, kuwawezesha wadau wa elimu katika kupanga gharama za uendeshaji wa mafunzo na upatikanaji wa rasilimali pamoja na usimamizi wa rasilimali hizo.

Hata hivyo Afisa Elimu huyo, amebainisha kuwa mfumo wa MEWAKA umeondoa changamoto nyingi zilizokuwepo za mifumo iliyotumika hapo awali ya mafunzo kwa walimu, hivyo programu ya MEWAKA ni mfumo rasmi ambao umeandaliwa na Serikali kutekeleza mtaala wa elimu msingi, unaozingatia umahiri wa mbinu za kufundishia na kujifunzia, kufanya tathmini kwa wanafunzi, pamoja na kuendeleza mafunzo hayo kwa kuhawilisha taaluma kwa walimu wote.

"MEWAKA imeandaliwa na Taasisi ya Elimu kwa kushirikiana na Ofisi ya Rais TAMISEMI, kwa zingatia mitaala ya elimu inaozingatia umahiri, ndani yake kuna moduli mbalimbali zitakazowawezesha walimu kujinoa kitaaluma na kuwa mahiri katika ufundishaji pamoja na kujifunza namna ya kuendeleza mafunzo hayo kwa walimu wote ili kuwa na umahiri unaoendana na wakati" amefafanua Afisa Elimu Alute.

Aidha walimu hao wameweka wazi kuwa, MEWAKA imekuja wakati muafaka, kutokana na kasi ya maendeleo ya kisayansi, yanayotokana na mabadiliko ya teknolojia, mabadiliko yanayomlazimu mwalimu kujisomea sana ili kupata maarifa mapya, huku wakithibitisha kuwa, program ya MEWAKA, inawapa walimu fursa endelevu ua kujinoa kitaaluma kwa kusoma na kubadilishana uzoefu wa kazi.

Mwalimu Mkuu, shule ya Msingi Ngaramtoni, mwalimu Makanjo Twaty, amesema kuwa program ya MEWAKA ni muhimu kwa walimu, na watahakikishia kutumiammuda wa ziada kujifunza miongo yote iliyoainishwa bila kuathiri ratiba za masomo kwa wanafunzi, huku akisistiza kuwa MEWAKA itawafanya walimu kufundisha kwa kuendana na wakati, hasa kwa walimu waliosoma miaka mingi iliyopita.

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527

0/Post a Comment/Comments