MAAFISA WATENDAJI WA MITAA, KATA NA WENYEVITI WA MITAA , POLISI JAMII KATA WATAKIWA KUIMARISHA ULINZI NA USALAMA KUPUNGUZA UHALIFU


Kamishina wa Polisi jamii Tanzania Mussa Ally Mussa akisalimiana na baadhi ya viongozi Bukoba
Kulia ni Kamishina wa Polisi jamii Tanzania Mussa Ally Mussa akiwa na Katibu Tawala Mkoa wa Kagera Prof. Faustine Kamuzora
Watumishi na watendaji wa mitaa  Bukoba
Baadhi ya watendaji wa kata Bukoba
**


Na Mbuke Shilagi Kagera.

Viongozi wa Serikali za Mitaa na Kata katika Wilaya ya Bukoba Mkoani Kagera wametakiwa kuhakikisha wanaimarisha ulinzi na usalama katika maeneo yao ili kupunguza vitendo vya uharifu nchini.

Kauli hiyo imetolewa na Kamishina wa Polisi jamii Tanzania,  Mussa Ally Mussa Mei 9,2022  alipokutana na kufanya mazungumzo na wenyeviti wa mitaa pamoja na watendaji wa mitaa na kata kwenye uwanja wa Kaitaba wilayani  Bukoba mkoani Kagera   ili kutoa elimu  kwa viongozi hao  jinsi ya kukabiliana na vitendo vya uharifu katika mitaa yao.

“Unatakiwa kujua kila nyumba wanakaa watu gani na wanashugulika na nini, ndicho kinachotakiwa ili kujua eneo lako wezi ni watu gani, hauwezi kuzuia uharifu usipo jua wahusika ni watu gani na ndo maana kazi ya Polisi inakuwa ngumu kwa sababu mnaacha vipengele vidogo, hivyo fatilieni kujua kaya za maeneo yenu wanakaa watu gani” Amesema.

Kamishina Mussa amesema kwa taarifa alizopewa na RPC wa mkoa wa Kagera vitendo vilivyokithiri katika mkoa huo  kwa sasa ni mauwaji pamoja na ubakaji, na kwa taarifa alizonazo ni kwamba kipindi cha miezi mitatu inaonyesha si chini ya makosa 30 ya mauaji yanayo tokea mkoani humo.

 “Bado kuna tatizo katika serikali za mitaa, hawajatambua kuwa kudumisha ulinzi katika maeneo yao ni wajibu wao kisheria wala sio ombi, wanatakiwa kujua kuwa kazi ya kulinda wananchi ni kazi yao pia siyo jeshi la polisi peke yake” Amesema.

Naye Afisa Mtendaji  wa Kata ya Hamugembe iliyopo Manispaa ya Bukoba mkoani Kagera  Renovatus Mwesiga amemshukuru Kamishina wa Polisi Jamii Tanzania pamoja na viongozi wa ulinzi na usalama katika mkoa huo kwa elimu waliowapatia , huku akimuomba RPC wa Mkoa wa Kagera kuwakutanisha na polisi kata ili kuwajengea uelewa kwa pamoja.

Naye Katibu Tawala Mkoa wa Kagera,  Prof. Faustine Kamuzora  amesema kuwa, wao kama viongozi katika Mkoa huo wamekuwa wakiwasisitiza sana juu ya umuhimu wa kudumisha ulinzi na usalama katika maeneo mbalimbali ya mkoa licha ya  mkoa huo kuwa na idadi kubwa ya watu huku ameahidi kuendelea  kushirikiana nao ili kuhakikisha wananchi wa mkoa huo wanakaa kwa Amani na usalama.

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527

0/Post a Comment/Comments