JESHI LA POLISI KAGERA LAWATAKA WANANCHI KUSHEREHEKEA KWA AMANI SIKUKUU YA PASAKA


Kamanda wa Jeshi la Polisi Mkoa wa Kagera ACP William Mwampaghale

Na Mbuke Shilagi Kagera.

Jeshi la Polisi Mkoani Kagera limewataka wananchi hasa waumini wa dini ya Kikristo kusherehekea kwa amani sikukuu ya Pasaka na kwamba jeshi hilo litaimarisha ulinzi katika maeneo yote ya mkoa.


Haya yamebainishwa na Kamanda wa Jeshi la Polisi Mkoa wa Kagera ACP William Mwampaghale wakati akizungumza na waandishi wa Habari ofisini kwakwe, kuhusu namna gani wamejipanga ili kuhakikisha Sikukuu inaisha salama.

Kamanda huyo amesema kuwa Jeshi la Polisi watakuwa kila mahali ikiwamo katika makanisa, kumbi za starehe, barabarani na kila mitaa ili kuhakikisha usalama unakuwepo.

ACP Mwampaghale ameongeza kuwa wananchi wote watakaokwenda katika maeneo ya fukwe wanapaswa kuwa makini na kusikiliza maelekezo ya askari, na kuzingatia sheria na taratibu zilizopo.

"Lakini pia wazazi kuweni makini na watoto, msiwaruhusu kwenda ufukweni mwa ziwa peke yao, ni hatari kwa usalama wao, kama mtaona lazima watoto wenu waende huko, basi wawe na mtu mzima ambaye ni mzazi au mlezi", amesema.


Aidha amewataka wananchi kuacha ulinzi nyumbani ili kuepusha vibaka kutumia fursa ya Sikukuu kuvunja nyumba na kuiba.

Amewataka pia madereva wanaojaza abiria na kuendesha magari na pikipiki kwa kasi kuacha tabia hiyo, na kuwataka pia kuepuka kutumia kilevi wakati wa siku kuu ili kuepuka ajali zinazoweza kuzuilika.

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527

0/Post a Comment/Comments