DC MBONEKO ATEMBELEA KIWANDA CHA KUZALISHA HEWA YA OKSIJENI SHINYANGA


Mkuu wa wilaya ya Shinyanga Jasinta Mboneko, akiwa kwenye kiwanda cha kuzalisha hewa ya Oksijeni kilichopo Mwawaza Manispaa ya Shinyanga.

Na Marco Maduhu, Shinyanga
MKUU wa wilaya ya Shinyanga Jasinta Mboneko, amefanya ziara ya kukagua utekelezaji wa miradi mbalimbali ya maendeleo Manispaa ya Shinyanga, pamoja na kuona kiwanda cha uzalishaji wa hewa ya Oksijeni kilichopo Mwawaza Manispaa ya Shinyanga.

Mboneko amefanya ziara hiyo leo March 4, 2022, akiwa ameambatana na wataalam wa Manispaa ya Shinyanga, pamoja na wajumbe wa Kamati ya ulinzi na usalama wilaya ya Shinyanga.

Amefanya ziara kwa kukagua maendeleo ya ujenzi wa kituo cha Afya Ihapa, Hospitali ya Rufani ya Mkoa wa Shinyanga, Hospitali ya Magonjwa ya mlipuko, ujenzi wa shule mpya ya Sekondari Lubaga, vyumba vya madarasa, pamoja na viti na meza katika shule za Sekondari Kolandoto na Mazinge, maeneo ya uwekezaji na ujenzi wa stendi kuu ya mabasi na mnada Kata ya Ibadakuli.

Akizungumza wakati wa ukaguzi wa jenzi hizo,Mboneko amewataka wakandarasi waongeze kasi ya ujenzi wa majengo hayo na kuzingatia ubora unaotakiwa ili yadumu kwa muda mrefu.

“Nataka ubora wa majengo kwenye ujenzi huu wa huduma za afya, na elimu, na ugomvi wangu mkubwa mimi kwenye utekelezaji wa miradi hii ya maendeleo pale nitakapoona nyufa, nataka thamani ya fedha ionekane,”alisema Mboneko.

“Miradi yote hii ambayo nimeona kasoro zake zifanyiwe marekebisho ya haraka, na pia Wahandisi acheni kukaa maofisini tembeleeni miradi yote ambayo inaendelea kutekelezwa na kutoa ushauri wa kitaalam ili ijengwe kwa ubora,”aliongeza.

Aidha, akizungumza wakati wa ukaguzi wa viti na meza vilivyotengenezwa kwenye shule hizo za Sekondari mbili Kolandoto na Mazinge, ameonyesha kutoridhishwa na kuagiza uongozi wa shule utafute fundi na kufanyiwa marekebisho, huku akionya wanafunzi kuacha tabia ya kuchora chora viti hivyo na meza.

Katika hatua nyingine Mboneko amempongeza Rais Samia Suluhu Hassani, kwa kutoa fedha na kujengwa kiwanda cha uzalishaji wa hewa ya Oksijeni mkoani Shinyanga, ambacho kina uwezo wa kuzalisha hewa hiyo na kujaza mitungi 200 kwa siku.

Alisema kiwanda kingine kama hicho cha kuzalisha hewa ya Oksijeni kitajengwa pia katika Hospitali ya Mkoa, ambacho nacho kitazalishwa hewa hiyo kwa kujaza mitungi 200, ambapo mkoa huo kwa ujumla utakuwa ukizalisha hewa ya Oksijeni kwa mitungi 400 kwa siku.

“Tunamshukuru sana Rais Samia kwa kuendelea kutoa fedha za utekelezaji wa miradi mbalimbali ya maendeleo mkoani Shinyanga, ikiwamo ujenzi wa kiwanda hiki cha kuzalisha hewa ya Oksijeni, kwa ajili ya kuokoa afya za wananchi, hivyo hatuna budi kumpongeza Rais wetu kwa kujali afya za wananchi wake,”alisema Mboneko.

Alisema kipindi cha mlipuko wa ugonjwa wa COVID-19 uliposhika kasi, walikuwa wakipata tabu ya ujazaji wa hewa ya Oksijeni kwenye mitungi kwa ajili ya kukoa uhai wa wananchi, ambapo walikuwa wakisafirisha kujaza mitungi hewa hiyo jijini Mwanza, lakini sasa hivi uzalishaji utakuwa mkoani Shinyanga.

Kwa upande wake msimamizi wa shughuli za ujenzi wa miradi ya Afya katika Hospitali mpya ya Rufani mkoani Shinyanga, Hospitali ya magonjwa ya mlipuko na kiwanda hicho cha uzalishaji hewa ya Oksijeni kwa ajili ya Tiba Fred Mwakyoma kutoka Wizara ya Afya, alisema kiwanda hicho kipo hatua ya mwisho wa ukamilishaji, na walishafanya majaribio ya awali ya kujaza hewa ya Oksijeni kwenye mitungi.

Akizungumzia upande wa ujenzi wa Hospitali ya Magonjwa ya mlipuko, na ujenzi wa jengo la dharura na chumba cha wagonjwa mahututi (ICU), katika Hospitali mpya ya Rufaa mkoani Shinyanga, amesema ujenzi wake unaendelea vizuri na upo kwenye hatua nzuri.
Mkuu wa wilaya ya Shinyanga Jasinta Mboneko, akiwa kwenye kiwanda cha kuzalisha hewa ya Oksijeni.
Mkuu wa wilaya ya Shinyanga Jasinta Mboneko, akiwa kwenye kiwanda cha kuzalisha hewa ya Oksijeni.
Mkuu wa wilaya ya Shinyanga Jasinta Mboneko, akiangalia mitungi ambayo ipo tayari kujazwa hewa ya Oksijeni.
Muonekano wa mitambo ya kuzalisha hewa ya Oksijeni.
Mitungi ya hewa ya Oksijeni ikiwa katika eneo la kujazwa hewa hiyo, kwenye kiwanda cha uzalishaji wa hewa ya Oksijeni kwa ajili ya Tiba.

Via Shinyanga Press Club  blog

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527

0/Post a Comment/Comments