ZAIDI YA SH. MILIONI TANO ZATUMIKA KUJENGA VIVUKO VYA WATEMBEA KWA MIGUU KATA YA KASHAI

Kivuko cha Golani
Diwani wa Kata ya Kashai Ramadhani Kambuga akizungumza
Diwani wa Kata ya Kashai, Ramadhani Kambuga akizungumza
Mwenyekiti wa CCM Bukoba Mjini Joas Mganyizi (aliyevaa kofia).
Baadhi ya wananchi


Na Mbuke Shilagi Kagera.

Zaidi ya milioni tano zimetumika kujenga vivuko saba vya watembea kwa miguu ambavyo vinaunganisha mitaa mbalimbali iliyoko kata ya Kashai katika Manispaa ya Bukoba Mkoani Kagera. 

Hayo yamebainishwa na Diwani wa Kata hiyo, Ramadhan Kambuga katika uzinduzi wa daraja la Golani ambalo limezinduliwa na Mwenyekiti wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) Bukoba Mjini Joas Mganyizi.

Diwani Kambuga amesema kuwa vivuko hivyo saba vimejengwa katika mitaa tofauti na kwamba viwili vimejengwa katika mtaa wa Mafumbo, viwili katika  mtaa wa Katatorwansi, kimoja katika  mtaa wa Rwome, kimoja mtaa wa Matopeni na kingine kimoja kinaunganisha mtaa wa Kashenye na Kisindi.

Amesema kuwa lengo la kujenga vivuko hivyo ni kuwawezesha wananchi kuvuka salama hasa katika msimu wa mvua, na kwamba amefanya kazi hiyo kwa fedha zake binafsi kwa kushirikiana na marafiki zake.

"Vivuko hivi mbali na kuchangia maendeleo ya kata pia vimechangia kuondoa adha kwa watoto ambao wanapita katika vivuko hivyo kwenda shule",amesema. 

Kwa upande wake Mwenyekiti wa CCM Bukoba Mjini Joas Mganyizi amempongeza Diwani huyo na kusema kuwa kata ya Kashai ni kata pekee ndani ya Manispaa ya Bukoba yenye watu wengi kuliko kata nyingne, hivyo zinahitajika jitihada za makusudi katika kuwaletea wananchi maendeleo.

"Kashai ni kata ambayo inapaswa kuwa na mtu mwenye uwezo wa kufikiri, upendo, mwenye kujituma na mbunifu, ndipo azma ya kuwaletea maendeleo endelevu wananchi itatimia", amesema Mganyizi.

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527

0/Post a Comment/Comments