WAZIRI MCHENGERWA ATOA MAELEKEZO MAZITO YA KUBORESHA SOKA NCHINI.

Waziri wa Utamaduni, Sanaa na Michezo. Mhe.Mohamed Mchengerwa akiwa pamoja na Katibu Mkuu wwa Wizara hiyo Dkt.Hassan Abbasi akizungumza na waandishi wa habari leo Jijini Dar es Salaam Waziri wa Utamaduni, Sanaa na Michezo. Mhe.Mohamed Mchengerwa akisisitiza jambo mbele ya waandishi wa habari (hawapo pichani) leo Jijini Dar es Salaam Waziri wa Utamaduni, Sanaa na Michezo. Mhe.Mohamed Mchengerwa akizungumza na waandishi wa habari leo Jijini Dar es Salaam

************************

Na. John Mapepele

Waziri wa Utamaduni, Sanaa na Michezo. Mhe, Mohamed Mchengerwa leo Februari 14, 2022 ametoa maelekezo mazito kwa Baraza la Michezo la Taifa (BMT) na Shirikisho la Mpira wa Miguu nchini (TFF) yanayolenga kuboresha mchezo wa mpira wa miguu nchini.

Maelekezo hayo ameyatoa katika mkutano wa Waandishi wa Habari aliofanya katika Ukumbi wa Uwanja wa Taifa jijini Dar es salaam leo Februari 14 baada ya kufanya kikao na Viongozi wa TFF, BMT na watendaji wa Wizara.

Amefafanua kuwa Serikali ipo katika mikakati kabambe ya kuboresha miundombinu ya michezo katika shule 56 nchini ikiwa ni pamoja na kufunga mashine za kisasa za kufuatilia michezo (VAR) kwenye viwanja vitano kwa kuanzia pamoja na kujenga vituo vikubwa vya michezo.

Akitoa maelekezo ya Serikali, Mhe. Mchengerwa amesema BMT likutane na TFF mara moja kujadili namna ya kudhibiti vitendo vya ukiukwaji wa Sheria na taratibu za mchezo huo pendwa nchini ambapo pia amesisitiza kuwa Kamati inayohusika na Waamuzi ijitafakari kwa kuwa hadi sasa kwenye msimu huu wa ligi tayari imeshawaondoa waamuzi 13 kwa makosa ya upendeleo na rushwa.

Pia amesema TFF likutane na waamuzi wote ili kupata uvumbuzi wa changamoto na sintofahamu zinazoendelea kujitokeza katika mchezo huo kinyume na sheria ambapo TAKUKURU washirikishwe wawepo ili waweze kutoa elimu ya rushwa kwenye mchezo wa mpira wa miguu.

Amefafanua kuwa iwapo Serikali haitaweza kudhibiti vitendo vya rushwa kwenye mchezo wa mpira wa miguu, mchezo huo hautakuwa na maendeleo.

Aidha, amesisitiza waamuzi wasio na sifa waondolewe moja kwa moja na kuwaleta wengine wenye sifa na TFF lihakikishe utekelezaji wa sheria na kanuni za vilabu huku BMT iendelee kusimamia utawala bora ili kuwe na ustawi katika michezo.

Pia ameviomba Vyombo vya Habari kuelimisha jamii kuhusu programu mbalimbali za redio na televisheni kuhusu sheria za mpira wa miguu kupitia kwa wakufunzi na waamuzi.

Katika mkutano huo Mhe. Mchengerwa aliambatana na Katibu Mkuu wa Wizara yake Dkt. Hassan Abbasi, na Mkurugenzi wa Idara ya Maendeleo ya michezo na Kaimu katibu Mtendaji wa Baraza la Michezo la Taifa(BMT) na Uongozi wa TFF

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527

0/Post a Comment/Comments