WATATU WAFARIKI KWA KULIPUKIWA NA KINACHODAIWA KUWA NI BOMU


Watu watatu wamefariki dunia baada ya kulipukiwa na kile kinachodaiwa kuwa bomu mkoani Pwani.

Kamanda wa Polisi Mkoa wa Pwani, Wankyo Nyigesa, aliwaambia waandishi wa habari jana kuwa tukio hilo lilitokea juzi majira ya saa 8:00 mchana katika kijiji cha Pongwe Msungura, Kata ya Msata.

Wankyo alisema watu hao waliokota chuma kinachodhaniwa kuwa ni bomu ambacho kililipuka mikononi mwao na kusababisha vifo vyao.

Kwa mujibu wa Kamanda Wankyo, watu hao waliokota kitu hicho kwa lengo la kwenda kukiuza kama chuma chakavu, lakini kiliwalipukia muda mfupi baada ya kukiokota.

Aliwataja waliofariki dunia katika tukio hilo kuwa ni Athumani Ramadhani (20), Maneno Hamis (23) na Abdallah Rajabu (21), wote wakazi wa Msata.

Kamanda Wankyo alitoa angalizo kwa wananchi wanaojihusisha kuuza na kununua vyuma kuwa waangalifu wanapokusanya na vitu vingine kwa lengo la kwenda kuviuza.

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527

0/Post a Comment/Comments