SPIKA NDUGAI AMUOMBA RADHI RAIS SAMIA : NIMEKOSA MIMI,NIMEKOSA SANA,NISAMEHENI


Spika wa Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Job Ndugai,akizungumza na waandishi wa habari (hawapo pichani) leo Januari 3,2022 jijini Dodoma pamoja na kumuomba radhi Rais Samia na watanzania wote ambao waliupokea ujumbe wake kitofauti.

Spika wa Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Job Ndugai,akisisitiza jambo kwa akizungumza na waandishi wa habari (hawapo pichani) leo Januari 3,2022 jijini Dodoma pamoja na kumuomba radhi Rais Samia na watanzania wote ambao waliupokea ujumbe wake kitofauti.


Waandishi wa habari wakimsikiliza Spika wa Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Job Ndugai,wakati akizungumza nao leo Januari 3,2022 jijini Dodoma pamoja na kumuomba radhi Rais Samia na watanzania wote ambao waliupokea ujumbe wake kitofauti.

.........................................................

Na.Alex Sonna,Dodoma

Spika wa Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Job Ndugai amemuomba radhi Rais Samia Suluhu Hassan na Watanzania wote ambao waliupokea ujumbe wake kitofauti kuwa yeye ni miongoni mwa watu wanaopinga jitihada zinazofanywa na Rais katika kuliletea Taifa maendeleo.

Pia amewahakikishia watanzania yeye ni yule yule ni uimara wake upo palepale na wale waliomrushia matusi amewasamehe bure na wengine hawajui wayatendayo na ndio maana amebeba matusi yote hivyo amekosa na asamehewe.

Spika Ndugai ameomba radhi hiyo leo Januari 3,2022 jijini Dodoma wakati akizungumza na Waandishi wa habari ambapo amesema amesema kuwa hotuba yake haikuwa na jambo la kukashifu wala kudharau juhudi za Serikali bali alikuwa anasisitiza ulipaji wa kodi na tozo mbalimbali.

“Kwa hiyo binafsi yangu popote pale ambapo nilihisiwa kwamba nimetoa neno la kumvunja moyo Rais wetu na akavunjika moyo, ninatumia fursa hii kupitia kwenu kumuomba radhi sana mheshimiwa Rais na kwa Watanzania wote,”amesema.

Amesema anaunga mkono jitihada zote za Serikali ikiwa ni pamoja na kukopa fedha kwa ajili ya kutekeleza miradi mbalimbali ya maendeleo, na wanaomuona yuko kinyume basi wamemuelewa vibaya.

Spika Ndugai amesema wao ni kitu kimoja na katu haitatokea wakatengana na wataendelea kumsaidia Mheshimiwa Rais Samia Suluhu Hassan.

“Katika hali kama hii haiwezi kutokea na haitatokea na si rahisi jambo kama hili kutokea peke yake hataweza, tumsaidie kwa sababu kwa pamoja ndio tutaweza.Mtawasikia Wabunge wapo na Rais na sisi wote tunatekeleza sera ya ilani ya CCM hatugombani hata siku moja hao washindwe na walegee,”amesema.

Pia,amesema nchi nzima inafurahia kwa jinsi mpango wa fedha za Uviko 19 zilivyotumika ambapo ametoa wito matumizi ya fedha hizo yaendelee kutumika hivyo hivyo kwani itakuwa ni faida kwa nchi.

“Mfano kwangu Kongwa nimefuatilia kila chumba cha madarasa kinachojengwa hakuna jengo zuri kama majengo hayo.Tumepiga tiles madarasa yetu yote,tumejenga vyumba 150 wastani wa bilioni 3 Kongwa,makusanyo yetu halmashauri ya Kongwa ni bilioni 3.

“Nitakuwa mtu wa kubeba dhambi kubwa sana kwa mafanikio makubwa haya kumpinga Rais,tusimvunje moyo Rais wetu mtamsikia kila mbunge na fedha hizi ziliidhinishwa,”amesema.

Spika Ndugai ameyasema hayo kufuatia kauli yake aliyoitoa tarehe 26 mwezi Desemba mwaka 2021 kuzua mijadala katika mitandao ya kijamii na baadhi ya vyombo vya habari hapa nchini, huku yeye akishutumiwa na baadhi ya watu kuwa anaenda kinyume na mipango ya Serikali.

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527

0/Post a Comment/Comments