KUNAMBI ACHUKUA FOMU KUWANIA USPIKA ,AAHIDI KUONGOZA KWA KUFUATA MISINGI YA USAWA


Mbunge wa Jimbo la Mlimba, Morogoro Godwin Kunambi akiongea na Waandishi wa habari Jijini Dodoma muda mfupi baada ya kukamilisha taratibu za kuchukua fomu ya kuwania kiti Cha Spika wa Bunge la Tanzania.

Mbunge wa Jimbo la Mlimba, Morogoro Godwin Kunambi akiongea na Waandishi wa habari Jijini Dodoma muda mfupi baada ya kukamilisha taratibu za kuchukua fomu ya kuwania kiti cha Spika wa Bunge la Tanzania.

Na Dotto Kwilasa, Malunde 1 blog, Dodoma.
MBUNGE wa Mlimba kupitia tiketi ya Chama Cha Mapinduzi (CCM) Godwin Kunambi amechukua fomu ya kuwania nafasi ya Spika wa Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania huku akiahidi kuongoza kwa kufuata misingi,kanuni na sheria za Bunge iwapo atachaguliwa.

Hatua hiyo imekuja kufuatia Chama hicho (CCM) leo Januari 10, 2022 kufungua dirisha la uchukuaji fomu za kuwania kiti hicho hadi tarehe 15 mwezi huu baada ya kiti hicho kuwa wazi kufuatia kujiuzulu kwa  aliyekuwa Spika wa Bunge hilo Job Ndugai hivi karibuni.

Kunambi ambaye mbali na kuwa Mbunge wa Mlimba ni kada maarufu wa CCM huku akiwa amewahi kushika nyadhifa mbalimbali za uongozi,amekabidhiwa fomu hiyo na Katibu msaidizi Mkuu, Idara ya Oganaizesheni  Solomon Itunda katika Ofisi za Makao makuu ya Chama hicho Jijini  Dodoma.

Muda mfupi baada ya kumaliza kuchukua fomu hiyo na kukamilisha taratibu zote  amesema kuwa anataka  kutumia nafasi hiyo kuwatumikia watanzania na kuahidi kuliendesha bunge kwa misingi ya usawa,kanuni na sheria.

"Nina uzoefu wa kutosha kuongoza ,hata wananchi wanafahamu ,najiamini naweza kutokana  na taaluma yangu ya sheria nitaliongoza Bunge kwa viwango vya juu zaidi,"amesema Mbunge huyo ambaye amewahi kuwa Mkurugenzi wa Jiji la Dodoma.

Mbali na hayo ameeleza kuwa amekuwa katibu wa CCM wilaya,amekuwa mwanasheria wa CCM miaka mitano ,amekuwa mkurugenzi wa halimashauri ya Jiji la Dodoma na sasa ni mbunge wa Jimbo la Mlimba hali inayomtambulisha kwamba yeye ni mchapa kazi mwadilifu.

"Ninaomba ridhaa ya kuwa Spika kwa kuwa uwezo wa kuongoza ninao na nina shahada ya sheria ,shahada ya pili ya utawala hivyo ninaweza kuongoza bunge kwa kufuata misingi ya kikatiba pamoja na kanuni za Bunge.

"Nikipewa ridhaa ya kuwa Spika nitafuata usawa na hakutakuwepo ubaguzi wala upendeleo wa haina yoyote na kila mwenye sifa ya kuwa mbunge atapewa haki yake ya kikatiba,kikanuni na kutaratibu kwa kufuata misingi ya kibunge",amesema Kunambi.

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527

0/Post a Comment/Comments