MGODI WA BARRICK NORTH MARA WAFIKIA LENGO LA UHIFADHI WA MABAKI YA TAKA ZITOKANAZO NA MCHAKATO WA UCHENJUAJI WA MADINI

Meneja Mkuu wa Mgodi wa Dhahabu wa Barrick North Mara, Apolinary Lyambiko, akielezea jambo kwa waandishi wa habari waliotembelea mgodi huo uliopo Wilaya ya Tarime mkoani Mara wakati wa kampuni hiyo ilipotangaza kufikia lengo lao la kukamilika kwa mradi wa kuhifadhi maji yatokanayo na uchenjuaji wa dhahabu pamoja na kusimika mitambo ya kisasa ya kusafisha maji kutoka lita milioni 2.5 ya zamani hadi lita milioni 40 kwa siku
Meneja Uchenjuaji wa mgodi wa Dhahabu wa Barrick North Mara,Christopher Mwinuka,akiwaonyesha waandishi wa habari jinsi mtambo wa kusafisha maji taka unavyofanya kazi.
Waandishi wa habari wakiangalia jinsi mtambo wa kusafisha maji unavyofanya kazi wakati walipotembelea mgodi wa North Mara.
Watendaji Waandamizi wa Barrick North Mara wakitoa maelezo kwa waandishi wa habari kuhusiana na mtambo mpya wa kusafisha maji unavyofanya kazi.
Mwenyekiti wa kijiji cha Matongo kilichopo wilayani Tarime Daudi Itembe akitoa neno la shukrani wakati wa hafla ya uzinduzi wa mfumo mpya wa TSF
Mtaalamu wa Usalama na uzalishaji wa Maji wa mgodi wa Dhahabu wa Barrick North Mara, Mohammed Balozi akifafanua jambo kwa waandishi kuhusiana mtambo mpya wa kusafisha maji


***
Mgodi wa Barrick wa North Mara umetangaza kuwa umetimiza dhamira yake ya kurudisha bwawa la kuhifadhia mabaki ya taka zitokanazo na mchakato wauzalishaji wa dhahabu (TSF) kama ulivyobuniwa ndani ya uwezo wake kufikia mwishoni mwa mwaka huu.


Barrick, ilitoa ahadi hiyo kwa serikali ya Tanzania ilipochukua udhibiti wa mgodi huo Septemba 2019. Wakati ambapo Baraza la Taifa la Usimamizi wa Mazingira nchini (NEMC) lilikuwa limefunga mfumo huo wa TSF ambao ulikuwa haufanyi kazi ipasavyo.


Ofisa Mkuu wa Uendeshaji wa kampuni hiyo kwa Afrika na Mashariki ya Kati, Willem Jacobs, alielezea kufikiwa kwa lengo hilo kama hatua kubwa kwa mgodi wa North Mara na timu ya watendaji wake, ambayo ilifanya juhudi kubwakuhakikisha mfumo wa TSF unaendana na ubora na viwango vya kimataifa unaotekelezwa na kampuni ya Barrick katika maeneo yake ya kazi.


Barrick ilitumia zaidi ya dola milioni 65 katika mradi huo, na kuongeza uwezo wa mtambo wa kusafisha maji mara 16 kutoka lita milioni 2.5 kwa siku hadi lita milioni 40 kwa siku. Kuongezwa kwa mtambo wa kusafisha maji kumepunguza kiasi cha chumvi katika maji machafu, na kuwezesha kuhifadhiwa kwa usalama.


North Mara itaendelea kufuatilia utendajikazi wa mfumo wa TSF na itashirikiana mara kwa mara na mamlaka husika ili kuhakikisha kuwa viwango vyake vya juu vinadumishwa. Hii ni pamoja na uchambuzi wa visima vya maji ya kunywa na vyanzo vya maji ya juu ya ardhi vinavyozunguka mgodi.


“Tulipochukua mali za zamani za Acacia nchini Tanzania, tuliunda ushirikiano na Serikali kusimamia migodi hii. Manufaa ya kweli ya ushirikiano huu yalijumuisha kurejeshwa kwa haraka kwa shughuli za uzalishaji katika mgodi wa North Mara na Bulyanhulu.


Maendeleo haya ya hivi punde ni uthibitisho zaidi wa uwezo wa falsafa ya ushirikiano wetu kuleta manufaa halisi na kujitolea kwetu kutunza ustawi na mazingira ya jumuiya zinazotukaribisha,” Jacobs alisema.

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527

0/Post a Comment/Comments