MAPINGAMIZI YAENDELEA KUTAWALA KESI YA FREEMAN MBOWE NA WENZAKE


 Mapingamizi yametawala katika kesi ya ugaidi inayomkabili Mwenyekiti wa Chadema, Freeman Mbowe na wenzake, tangu ilipoanza kusikilizwa katika Mahakama Kuu, Divisheni ya Makosa ya Rushwa na Uhujumu Uchumi.


Tangu kesi hiyo ianze kusikilizwa mahakamani hapo, mawakili wa kina Mbowe wameweka mapingamizi matano ambayo yote yalitupwa mbali.

Leo Jumanne, tarehe 9 Novemba 2021, mahakamani hapo mbele ya Jaji Joackim Tiganga, mawakili hao wa utetezi waliweka pingamizi dhidi ya nyaraka iliyoelezea namna Mbowe alivyokataa kutoa maelezo yake ya onyo mbele ya Afisa wa Polisi.

Wakili wa utetezi, Nashon Nkungu, aliweka pingamizi hilo akiiomba mahakama hiyo isipokee nyaraka hiyo akidai kuwa Mbowe hakuandika maelezo hayo.

Upande wa jamhuri uliiomba mahakama hiyo iondoe nyaraka hiyo ili shahidi wao aliyoileta aendelee kutoa ushahidi wake.

Pingamizi la pili, liliwekwa na mawakili wa utetezi, dhidi ya maelezo ya onyo ya mshtakiwa wa tatu, Ling’wenya,

Maelezo hayo yaliwasilishwa mahakamani hapo leo Jumanne na Mkuu wa Upelelezi wilayani Arumeru, mkoani Arusha, SP Jumanne Malangahe, anayedaiwa kumhoji mtuhumiwa huyo tarehe 7 Agosti 2020, katika Kituo cha Polisi cha Kati cha Dar es Salaam.

Wakili wa utetezi, Fredrick Kihwelo ametoa hoja zaidi ya tano, kupinga nyaraka ya maelezo hayo, alizodai kuwa zinaonesha maelezo hayo ni kinyume cha sheria.

Miongoni mwa hoja hizo ni, Wakili Kihwelo amedai mshtakiwa huyo wa tatu hakuwepo katika Kituo cha Polisi cha Kati Dar es Salaam, wala hakuandikisha maelezo hayo tarehe 7 Agosti 2020 na au siku nyingine yoyote.

Katika hoja ya pili, Wakili Kihwelo amedai, Lingwenya alilazimishwa kusaini nyaraka hiyo baada ya kutishiwa na kwamba akiwa katika Kituo cha Polisi Mbweni, Dar es Salaam, alilazimishwa kusaini nyaraka iliyodaiwa kuwa na maelezo yake.

Bila kuyasoma huku akipewa mateso ya kisailokolijia akisimamiwa na mtu aliyetajwa kwa jina la Goodluck Minja, aliyekuwa na silaha aina ya bastola huku SP Jumanne akimueleza asaini au akikataa apate mateso kama aliyopata akiwa katika Kituo cha Polisi cha Kati Moshi, mkoani Kilimanjaro.

Wakili Kihwelo alitaja hoja ya tatu kuwa ni, maelezo hayo yalichukuliwa nje ya muda kisheria huku nyingine ikiwa ni shahidi huyo namba nane alishindwa kunukuu kifungu cha sheria kilichotumika katika maelezo hayo.

Naye Wakili John Mallya ameipinga nyaraka hiyo, akidai kuwa haikuwepo katika mwenendo wa mashtaka (Committal Proceedings), na kwamba imeathiri haki ya mshtakiwa Ling’wenya na washtakiwa wengine.

Kwa upande wake, Wakili Peter Kibatala ameipinga nyaraka ya maelezo hayo, akidai kuwa hakukuwa na onyo kwa mtuhumiwa kwani sheria iliyotumika haipo nchini.

Wakili Kibatala amedai, sheria iliyowekwa katika maelezo hayo ya onyo inasomeka kama Sheria ya Kuzuia na Kupambana na Ugaidi, wakati Sheria iliyopo ni ya kuzuia ugaidi.

Wakili huyo wa utetezi amedai, nyaraka ya maelezo hayo ya onyo haikutaja vifungu vidogo vya Sheria ya Kuzuia Ugaidi (1 na 2), ambavyo vinaeleza mahali ambako kosa limetenda.

Amedai, Sheria ya Kuziia Ugaidi kifungu cha 24 (1), kinahusu kosa la kula njama za kufanya vitendo vya kigaidi nje ya Tanzania wakati cha 24 (2), kilihusu kosa la kula njama za kutenda vitendo vya kigaidi ndani ya Tanzania.

Pingamizi hilo liliibuliwa baada ya Mkuu wa Upelelezi Wilayani Arumeru jijini Arusha, SP Jumanne Malangahe, kuiomba mahakama hiyo ipokee maelezo hayo kama kielelezo cha ushahidi wa upande wa mashtaka.

Kwa upande wake, Wakili wa Serikali Mwandamizi, Robert Kidando amesema, 'Mheshimiwa Jaji nimesikia hoja za mapingamizi, ambayo ni ya aina mbili.'
 

Amezitaja ni, kwa maana kwamba kuna ambayo yanakijita kwenye kifungu cha 27 cha Sheria ya Ushahidi Sura ya 6 na kuna ambayo yanayojikita kwa kutokidhi matakwa ya Sheria ya Mwenendo wa Makosa ya Jinai kwenye vifungu kadhaa kama walivyo virejea.

“Kiutaratibu Mheshimiwa Jaji aina hiyo ya mapingamizi yalitakiwa kutatuliwa kwa mawakili Wa pande zote mbili kuelezea Mahakama na iweze kutoa maamuzi,” amesema Wakili Kidando na kuomba ifanyike kesi ndogo katika kesi ya msingi.

Hoja hiyo ilikubaliwa na upande wa utetezi na Jaji Joachim Tiganga anayesikiliza kesi hiyo, kuagiza mawakili wa pande zote mbili kukutana ili kuangalia ni mambo gani watakayokwenda kuyashughulikia katika kesi hiyo ndogo.



Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527

0/Post a Comment/Comments