MALKIA LADIES GROUP KUZINDULIWA RASMI JUMAMOSI TAREHE 20 NOVEMBA 2021

Mwenyekiti wa Kikundi cha Kikoba cha Malkia Ladies Group, Charity Mwakalonge ( wa pili kulia) akizungumza na waandishi wa habari jijini Dar es Salam leo wakati akitangaza Uzinduzi pamoja na kongamano la kikundi hicho utakaofanyika Jumamosi hii tarehe 20, 2021 katika ukumbi wa PTA Sabasaba Jijini Dar es salaam.

Mkutano huo mkuu unategemea kupokea wanawake zaidi ya 6,000. Kutoka Kushoto ni Mwanamuziki wa Muziki wa Dansi, Aneth Kushaba, Mwenyekiti wa Kamati ya Uwekezaji, Chevawe Mberesero na Kaimu Mwenyekiti Kamati ya Jamii, Husna Mkupete.

Kikundi cha Kikoba cha Malkia Ladies Group kinawakaribisha wanawake wote popote walipo kuhudhuria kwenye Tamasha kubwa la kikundi hicho chenye makazi yake jijini Dar es Salaam. Mkutano huo mkuu utafanyika Jumamosi hii tarehe 20, 2021 katika ukumbi wa PTA Sabasaba na unategemea kupokea wanawake zaidi ya 6,000. 

Hakuna kiingilio bali mtu yeyote anakaribishwa. Labda mtajiuliza Malkia ladies ni akina nani? Ni kikundi cha Kikoba kilichosajiliwa na Benki kuu ya Tanzania chenye lengo la kuwasaidia wanawake wengine kupitia elimu ya fedha yaani uwekaji wa akiba na pia uwekezaji kwa maendeleo yao wenyewe na familia zao. 

Kwa sasa wajumbe wa Malkia ladies Group wapo 34 na mzunguko wao wa fedha unafikia zaidi ya milioni 250 kwa mwaka, hii imetokana na kikundi hiki kuwa na nidhamu ya uwekaji akiba na pia kuanza kuwekeza kupitia fursa mbalimbali, sasa kina kuja na program maalumu ya kusaidia wanawake wengine kuanzisha vikundi kama hivi na kuvikilea ili kuja kuwa vikubwa na mwisho kuleta matokeo chanya ndani ya chama chenyewe na taifa kwa ujumla.
Siku ya Jumamosi tarehe 20, wanakaribishwa wanawake wengine wanaotaka kujifunza namna bora ya kuanzisha vikundi na pia kujifunza namna ya kuendeleza vikundi vyao ili vilete tija miongoni mwao. 

Siku hiyo watazindua rasmi kikundi cha Malkia pamoja na uzinduzi wa kampuni ya Bima (Insurance) ambayo itaanza kutoa huduma hivi karibuni, pamoja na kuzindua Ramani ya Malkia women market Mall yenye maduka Zaidi ya 100 ili kuwapa wanawake sehemu ya kuuzia bidhaa zao, mwisho watazindua Kitabu cha fursa 50 pamoja na Youtube Channel inayoitwa (Malkia Ladies TV) ambayo itakuwa chachu ya akina mama kupata elimu ya masuala ya vikundi na uwekezaji.

 Malengo yao ni kusaidia wanawake wenzao kupitia Biashara kwani wanategemea kwa watakao hudhuria na kuanzisha kikundi chao, watachagua vikundi vitatu kwa kuanzia ili tuvilee vifikie kiwango kikubwa kuliko hata chao.
Mgeni rasmi wa uzinduzi huu ulio katika mfumo wa kongamano ni Mheshimiwa Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu Sera, Bunge, Kazi, Vijana, Ajira na Walemavu, Mhe. Jenista Mhagama (mb) atakayeambatana na Mlezi wao Rais mstaafu wa bunge la Africa Mh. Getrude Mongella wanategemea kuwapokea wanawake wote wanaotaka kupata elimu ya vikundi na pia wanaotaka kuanzisha vikundi vyao waje wasikilize na wanaimani hawataondoka kama walivyokuja, wataondoka na kitu kikubwa sana cha kujenga na kubadilisha Maisha yao.

 Kauli mbiu ya Mkutano huo wa jumamosi ni “Mwanamke ni Nguzo ya Uchumi, Amka Uwekeze.” 

Wanawaomba wanawake wenzao popote walipo, karibuni kwenye ukumbi wa PTA SabaSaba jumamosi kuanzia saa mbili kamili asubuhi. Pia kutakuwa na burudani mbalimbali kutoka kwa Msanii Peter Msechu, Aneth Kushaba na The Star Band.
 Mada mbalimbali zitatolewa kutoka kwa watu maarufu kama Aunt Sadaka atakayeteta na wanawake wote watakao hudhuria siku hiyo.

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527

0/Post a Comment/Comments