JAMAA ATENGENEZA MASHINE YA KUPIKA UGALI DAKIKA 3 UNGA WA KILO 10


Ugali ni chakula kinacholiwa sana barani Afrika. Huenda kikawa ndio chakula chenye umaarufu mkubwa Afrika, kikitokana na nafaka hasa ya mahindi.

Ubugali (Burundi, DR Congo, Sudan, Sudan Kusini, Rwanda), moteke (RDC) na busima (Uganda), ni sehemu ya majina maarufu ya ugali katika ukanda wa afrika Mashariki ambao kawaida hupikwa kwa kutumia mwiko.

Lakini Video fupi inayomuonyesha mwanaume mmoja akiandaa ugali imekuwa ikisambaa sana kwenye mitandao ya kijamii ikonekana pia kama inafurahisha.

Video hii inamuonyesha mtu huyu akichanganya unga na maji kwenye sufuria kabla ya kuusonga kwa kutumia mashine badala ya mwiko uliozoeleka na wengi wakati wa kusonga ugali. Inaelezwa kwamba mashine hiyo imeandaliwa na mtu mmoja anayeishi Kakamega, Kenya ikiwa na uwezo wa kupika ugali kwa rekodi ya muda wa dakika tatu tu.

Kwa mujibu wa mtandao wa tuko Kenya, uliochapisha taarifa za uvumbuzi huu, uandaaji wa ugali unatofautiana kati ya kabila na kabila, lakini kwa ujumla ugali mzuri ulioiva vizuri unaweza kupikwa kwa kati ya dakika 8 mpaka 15 inategemea na kiwango cha ugali wenyewe; mkubwa, wa wastani ama mdogo.

Video hii imewashangaza watu wengi kwenye mitandao ya kijamii baadhi yao wakieleza kwamba, si rahisi kupika ugali ukaiva vizuri kwa dakika tatu. “Ugali hauwezi kuiva ama kuwa tayari kwa dakika tatu. Huo sio ugali. Unaweza kuusonga lakini huo utakuwa “ugali maji”. Moto hautakua umeingia ndani vizuri. Haya ni ya wataalamu,” alisema Ja’Rusinga.

Kwa muonekano wa mashine hii kupitia video hiyo, ni mashine inayoonekana kutumia umeme ili iweze kujizungusha na kuusonga ugali, ikishikiliwa kwa mikono miwili na mtu anayeiendesha ama kutumia kusonga ugali.
Pengine hili linawafanya watu kuamini kwamba, itakuwa inarahisisha kwa kutumia muda mfupi na nguvu kidogo, lakini itakugharimu umeme au gesi ama mkaa unaotumika kupikia ugali huo.

Kupika ugali bila kutumia Mwiko

Njia mpya ya kupika ugali bila kutumia mwiko badala yake kwa kutumia mashine imeibua hisia tofauti kwa baadhi ya wakenya. Wapo wanaompongeza aliyebuni mashine hiyo lakini na wapo pia wanaokosoa.

Video hiyo ya ‘ubunifu’ huo mpya iliyosambaa sana imekuwa ikikosolewa na baadhi ya watu, wengi wakisema kwamba wana wasiwasi baada ya kuchanganya maji na unga wa ugali na kwa kutumia hiyo mashine kuusonga, ugali utakaotoka huenda usiwe umeiva vizuri.

Wanasema ugali unahitaji zaidi kuiva kuliko kusongwa. Mashine inatumika kuusonga na haina uwezo wa kuuivisha, hivyuo muda wa kuiva ugali hauwezi kuathiriwa na mbinu yoyote ya kuusonga iwe kwa kutumia mashine ama kwa kutumia mwiko.

Mwingine akasema; “Ugali huu utakuwa wa gharama ya juu kwa sababu ya kutumia gesi au mkaa na umeme lakini kazi nzuri kwa injinia,” alisema Mohamed Ali.

Mwanamuzi wa Kenya Owen Mwatia anayejulikana kama Daddy Owen, na yeye aliunga mkono wanaosema ugali huo hautakuwa umeiva vizuri ukisongwa kwa mashine hiyo na kwa muda huo mfupi. “Nimeona uvumbuzi mpya wa kupika ugali bila mwiko.

Hatuhitaji uvumbuzi mwingine wowote linapokuja suala la ugali! Pili kupika ni sanaa na mwiko ni brashi (kukamilisha Sanaa)! Kupika ugali bila mwiko, utapata chakula bila ‘malondo’ ni kama vitafunwa tu,” aliandika kwenye mtandao wake.

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527

0/Post a Comment/Comments