SHILINGI BILIONI 17.97 ZATOLEWA NA SERIKALI KUBORESHA MIRADI DODOMA

 

Mkuu wa mkoa wa Dodoma Antony Mtaka

Na Dotto Kwilasa - Dodoma
JUMLA ya Shilingi Bilioni 17.97 zimetolewa na Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa Mkoa wa Dodoma kwa ajili ya kuboresha miradi mbalimbali.

Hatua hii imekuja kufuatia  taarifa  ya TAMISEMI iliyotolewa jana na  Waziri  Ummy Mwalimu kutoa mchanganuo wa matumizi ya fedha hizo ambazo ni mkopo wa IMF kuwezesha kujikimu na Ugonjwa unaitikisa Dunia wa COVID-19.

Mkuu wa mkoa wa Dodoma Antony Mtaka amesema hayo leo kwenye kikao chake na Wafanyabiashara wa Jijini Dodoma kilicholenga kuwakumbusha  fursa hiyo na kuwawezesha  kuwa wanufaika wa kwanza.

Amefafanua mgawanyo wa fedha hizo kuwa Bilioni 12 zitahusisha ujenzi wa madarasa,Bilioni 3.5 kwa ajili ya madarasa shinikizi,Milioni 160 Kwa ajili ya kununua mabati pamoja na fedha za dharula ya afya milioni 900.

Nyingine ni milioni 100 kwa ajili ya ICU,milioni 840 kwa ajili ya huduma za X-ray na  milioni 450 kutumika kwenye ujenzi wa nyumba za watumishi.

"Kwa mgawanyo huo ni sawa na kusema  kwamba,mahitaji ya malighafi ni mifuko ya saruji elfu 88,nondo pisi elfu 44,mabati pisi elfu 44,kazi kwenu Wafanyabiashara,nawakumbusha hampaswi kulala,"amesisitiza Mtaka.

Amesema fedha hizo zitahusisha ujenzi kwa kila kata za Mkoa huu hivyo kuwataka Wafanyabiashara hao kuwa na kiwango kikubwa ya vifaa vya ujenzi  kuwezesha ujenzi kwenda kwa haraka.
.
"Niwakumbushe kuwa fedha hizi ni za kwenu,nyie ndío wanaufaika wa kwanza,msipandishe bei kiholela,"amesema

Kwa upande mwingine,Mtaka ametumia nafasi hiyo kuwataka Wafanyabiashara wote Mkoani Dodoma kufanya biashara zao kwa weledi huku wakielewa kuwa Dodoma ni makao makuu .

Amesema wengi wao hushindwa kuendelea na wengine hufilisika na kupelekea kuwa na imani za kishirikina kwamba huenda wamerogwa kumbe uchawi umetokana na wao wenyewe kwa kuwa hufanya biashara bila kuzingatia muda maalumu wa kufungua maduka yao.

"Tunashindwa jinsi ya kuwasaidia,mnafungua maduka yenu saa tatu asubuhi Kisha mnafunga saa 11 jioni hii inamaana kwamba watu wanaohitaji huduma wanakosa,mtatajirika lini ikiwa mnafungua biashara zenu kwa kujiskia,  Wafanyabiashara changamkieni fursa ya usambazaji wa vifaa vya ujenzi wa utekerezaji wa mradi kwa wakati,"amesema.

Amesema Fedha hizo ni fursa kiuchumi kupitia biashara na fedha hizo zimeelekezwa kwenda kwa Wafanyabiashara wazalendo ambao wanatakiwa kuachana na biashara ya uchuuzi badala yake wawe Wafanyabiashara wa kimataifa na Wafanyabiashara shindani.

"Tunataka mkue kwa kufuata mabadiliko, hatutaki uhaba bandia 
zingatieni ubora,tuna uzoefu wa miradi iliyopita tutasimamia vigezo vya  ubora.

Kwa upende wake Katibu tawala wa Mkoa wa Dodoma Dkt. Fatma Mganga amewataka wafanyabiashara hao kuzingatia maadili ya utumishi wa Umma,na kusema  wao ndio  wa kwanza kuwaaminisha watumishi.

"Kupitia miradi hii kataeni kuwahalalisha  baadhi ya watumishi wa Umma wanaotaka kujitajirisha kupitia fedha za Serikali ,msikubali kuuza bidhaa bila risiti,mnalipa kodi msituharibie nchi" ameeleza.

Aidha amesema wafanyabiashara wengi Dodoma hali ya huduma kwa wateja bado hairidhishi na hawajitambu kwa kushindwa kutoa huduma kwa wateja kama inavyotakiwa ikiwa ni pamoja na kuwavutia wateja wao kwa Kutoa huduma zenye ubora Kwa kuzingatia matumizi ya lugha nzuri.


Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527

0/Post a Comment/Comments