EWURA YATII KWA VITENDO MAAGIZO YA RAIS SAMIA


Kaimu Mkurugenzi Mkuu wa EWURA Mhandisi Godfrey Chibulunje akiongea na waandishi wa habari(hawapo pichani) kuhusu marekebisho ya tozo mbalimbali za biashara ya mafuta nchini.
Kaimu Mkurugenzi Mkuu wa EWURA Mhandisi Godfrey Chibulunje akiongea na waandishi wa habari(hawapo pichani)kuhusu ma rekebisho ya tozo mbalimbali za biashara ya mafuta nchini.

Na Dotto Kwilasa, Dodoma

KATIKA kukabiliana na kupanda kwa bei ya Mafuta katika soko la Dunia,Serikali kupitia mamlaka ya udhibiti wa huduma za nishati na maji(EWURA)imefikia hatua ya kurekebisha tozo mbalimbali kwa Taasisi zote zinazotoa tozo kwenye biashara ya Mafuta hapa nchini.

Uamuzi huo umefikiwa leo Oktoba 6 ,2021 baada ya Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Samia Suluhu Hassan kuitisha kikao cha kujadili namna bora za kupunguza bei za Mafuta hapa nchini na kuhakikisha kunakuwepo na utengano wa hifadhi ya Mafuta ikiwa ni pamoja na  kuwahakikishia Wafanyabiashara wa Mafuta hapa nchini wanafanyabiashara katika mazingira mazuri.

Baada ya maagizo hayo, EWURA imeibuka na kutoa taarifa kwa umma juu ya tozo ambazo Serikali imepunguza juu ya kukabiliana na ongezeko hilo na kueleza kuwa Serikali imebadilisha tozo ya matumizi ya miundombinu ya bandari ambayo inatozwa kwa Dola za Marekani kwa tani ambapo sasa itatozwa kwa Shilingi za Kitanzania huku tozo hiyo  ikipunguzwa kufikia Shilingi 15 kwa lita kutoka wastani wa Sh.22 kwa lita na kuondoa VAT katika tozo hiyo.

Akitolea ufafanuzi taarifa hiyo kwa  Vyombo vya habari,Kaimu Mkurugenzi Mkuu wa EWURA Mhandisi Godfrey Chibulunje ameeleza hali hiyo imesababishwa na sehemu ya tozo hiyo kuwekwa kwa ajili ya ujenzi wa boya la kupokelea Mafuta baharini ambao kwa sasa umekamilika na hivyo kiasi cha Shilingi 15 Kwa lita kinachopendekezwa kinaweza kutumika kwa ajili ya matengenezo.

"Mabadiliko haya yanaleta unafuu kwa watumiaji mafuta kwa wastani wa Shilingi bilioni 23.15 kwa mwaka kutokana na matumizi ya lita 3.42 kwa takwimu za mwaka 2020,"ameeleza.

Ametaja tozo nyingine ambayo Serikali imepunguza kuwa ni Mamlaka ya mapato Tanzania (TRA)ya kuchakata nyaraka kutoka Shilingi 4.8 kwa lita na kuwa kiwango maalumu cha Shilingi milioni 20 kwa kila meli ambapo kwa wastani meli 7 huleta shehena ya Mafuta kila mwezi .

"Mabadiliko haya yataleta nafuu kwa watumiaji mafuta kwa wastani wa shilingi bilioni 14.79 kwa mwaka kutokana na matumizi ya lita bilioni 3.42 kwa Takwimu za mwaka 2020,"amefafanua

Chibulunje amesema pia Serikali imepunguza tozo ya wakala wa vipimo Tanzania (WMA)kwa Shilingi moja kwa lita na kuwa tozo ya kiwango maalumu ambacho ni Shilingi milioni 7 kwa kila meli badala ya kutozwa kwa kila lita.

Mabadiliko mengine ya tozo ni ya Shirika la viwango Tanzania(TBS)ya kupima ubora wa Mafuta yanayoingizwa nchini kutoka Shilingi 1.24 kwa lita na kutozwa kwa kiwango maalumu ambacho ni shilingi milioni 12.8 kwa kila meli mabadiliko haya yataleta unafuu kwa watumiaji mafuta kwa wastani wa shilingi bilioni 3.21 kwa mwaka kutokana na matumizi ya Lita bilioni 3.42 kwa takwimu za mwaka 2020.

"Serikali pia imebadilisha mfumo wa tozo Kwa Shirika la Uwakala wa Meli (TASAC)kutoka Shilingi 3.54 Kwa lita na kuwa tozo ya kiwango maalumu ambacho ni shilingi milioni 20 kwa Kila mweli,tozo za udhibiti kwa shughuli za EWURA nazo zimepunguzwa kutoka wastani wa shilingi 5.54 kwa lita hadi Shilingi 3.06 kwa lita,"amefafanua .

Pia Serikali imefuta tozo  ya huduma inayotozwa na mamlaka za Serikali za mitaa Kwa Halmashauri za Temeke ,Kigamboni ,Tanga na Mtwara kwa Wafanyabiashara wa jumla ambao wana maghala ya kuhifadhia Mafuta ya jumla na kuleta unafuu wa wastani wa shilingi bilioni 19.82 kwa mwaka kutokana na matumizi ya lita bilioni 3.42 kwa takwimu za mwaka 2020.

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527

0/Post a Comment/Comments