SERIKALI YA TANZANIA YAFANIKIWA KUTEKELEZA KAULI MBIU YA UMOJA WA MATAIFA KUHUSU CHAKULA



Waziri wa Kilimo Profesa Adolf Mkenda akizungumza na waandishi wa habari katika ukumbi wa Kilimo 4 Wizara ya Kilimo jijini Dodoma wakati alipotangaza uzinduzi wa maadhimisho ya siku ya Chakula Duniani inayoadhimishwa na shirika la Chakula Duniani (FAO).

…………………………………………

Serikali ya Awamu ya Sita imefanikiwa kutekeleza kauli mbiu ya Umoja wa mataifa kuhusu siku ya Chakula Duniani inayosema ‘’Zingatia Uzalishaji na Mazingira Endelevu kwa Lishe na Maisha Bora kwa kuhakikisha uzalishaji wa chakula nchini unaimarika na kutosheleza mahitaji ya nchi kwa kipindi chote.Ambapo hali ya chakula mwaka huu imeendelea kuwa nzuri kutokana na uzalishaji mzuri katika msimu wa 2020/2021.

Kila mwaka Makao Makuu ya Shirika la Chakula na Kilimo Duniani (FAO) huchagua kaulimbiu ambayo huwa inatoa dira ya kuhamasisha wadau wote wa Sekta ya Kilimo, Mifugo na Uvuvi kuchangia katika kuhakikisha kila mtu anawezeshwa kupata chakula bora na cha kutosha wakati wote wa maisha yake.
Hayo amesasema Waziri wa Kilimo Mhe. Profesa Adolf Mkenda wakati walipozungumza na waandishi wa habari kwenye ukimbi wa Wizara ya Kilimo Kilimo 4 jijini Dodoma wakati akitangaza uzinduzi wa maadhimisho hayo yatakayozinduliwa rasmi kitaifa tarehe 10 Oktoba 2021 mkoani Kilimanjaro katika viwanja vya shule ya msingi Pasua, Manispaa ya Moshi na kilele chake kitakuwa tarehe 16 Oktoba, 2021.

Amesema tathmini iliyofanyika hivi karibuni imeonesha kuwa hali ya uzalishaji wa mazao ya chakula kitaifa na kimkoa katika msimu wa 2020/2021 na upatikanaji wake kwa mwaka 2021/2022 umefikia tani 18,425,250 kwa mlinganisho wa nafaka (Grain Equivalent) ambapo nafaka ni
tani 10,869, 596 na yasiyo nafaka tani 7,327,137. Ikilinganishwa na msimu wa 2019/2020 ambapo uzalishaji ulikuwa tani 18,196,733,

Ameongeza kuwa kumekuwa na ongezeko la uzalishaji wa tani 1,903,096 ambalo ni sawa na asilimia 10.5. Uzalishaji wa mahindi unatarajiwa kufikia kiasi cha tani 6,908,318 na mchele kufikia kiasi cha tani 2,629,519.

“Mahitaji ya chakula kwa mwaka 2021/2022 nchini, ni tani 14,796,751, ikilinganishwa na uzalishaji, nchi inatarajiwa kuwa na ziada ya tani 3,628,499 za chakula ambapo tani 1,222,103 ni za mazao ya nafaka na tani 2,406,396 ni za mazao yasiyo nafaka. Kiwango hiki cha uzalishaji kitaiwezesha nchi kujitosheleza mahitaji yake ya chakula kwa uwiano wa utoshelevu ( Self Sufficient Ratio-SSR ) wa asilimia 125.”Amesema Profesa Mkenda.

Pia amesema Pamoja na nchi kutarajiwa kuwa na utoshelevu wa chakula kwa kiwango cha Ziada (SSR ya 125), bado kuna Halmashauri 17 katika Mikoa 8 zenye maeneo yenye dalili za upungufu wa chakula kwa mwaka 2021/2022. Hali hii ni kutokana na sababu mbalimbali ikiwemo mtawanyiko mbaya wa mvua na visumbufu vya mazao shambani vilivyojitokeza katika msimu wa uzalishaji 2020/2021. Serikali inaendelea kufuatilia kwa karibu hali ya usalama wa chakula katika maeneo hayo ili kuhakikisha hali ya utengamano inaendelea kuwepo.

Amesema kuwa takwimu zinaonesha kuwa Mikoa inayozalisha chakula kwa wingi ndiyo yenye viwango vya juu vya udumavu kwa watoto mfano, Njombe asilimia 53.6, Rukwa asilimia 47.9, Iringa asilimia 47.1, Songwe asilimia 43.3, Kigoma asilimia 42.3 na Ruvuma asilimia 41.0. ambapo
Kwa upande wa Nyanda za juu Kaskazini mikoa ya Kilimanjaro, Arusha na Manyara, viwango vya udumavu si vya kuridhisha ingawa viko chini ikilinganishwa na mikoa iliyotajwa hapo juu. Takwimu zinaonesha kuwa hali ya udumavu kwa mkoa Kilimanjaro ni asilimia 20.0, Arusha 25.2, Manyara 36.1.

“Mkoa wa Kilimanjaro una changamoto ya tatizo la lishe iliyozidi (uzito uliozidi au kiribatumbo) kwa wanawake walio katika umri wa kuzaa (miaka 15 – 49) ambayo imefikia asilimi 49.0. Kiwango hiki kiko juu ikilinganishwa na wastani wa kitaifa ambao ni asilimia 31.7, kutokana na sababu mbalimbali ikiwa ni pamoja na elimu duni ya matumizi ya chakula na lishe kwa watanzania walio wengi”.

Aidha amebainisha kuwa kuwa Mikoa inayozalisha chakula kwa wingi ndiyo yenye viwango vya juu vya udumavu kwa watoto mfano, Njombe asilimia 53.6, Rukwa asilimia 47.9, Iringa asilimia 47.1, Songwe asilimia 43.3, Kigoma asilimia 42.3 na Ruvuma asilimia 41.0.

Kwa upande wa Nyanda za juu Kaskazini mikoa ya Kilimanjaro, Arusha na Manyara, viwango vya udumavu si vya kuridhisha ingawa viko chini ikilinganishwa na mikoa tajwa hapo juu. Takwimu zinaonesha kuwa hali ya udumavu kwa mkoa Kilimanjaro ni asilimia 20.0, Arusha 25.2, Manyara 36.1.

Aidha amesema chimbuko la maadhimisho haya ni Mkutano wa mwaka 1979 ambapo Nchi Wanachama wa FAO walikutana Jijini Quebec nchini Kanada na kujadili masuala mbalimbali kuhusu chakula. Mojawapo ya maazimio ya mkutano huo ilikuwa kufanya Maadhimisho ya Siku ya Chakula kila mwaka ili kutathmini na kuweka mikakati ya upatikanaji wa chakula cha kutosha, salama na chenye virutubishi kwa watu wote na kwa wakati wote.

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527

0/Post a Comment/Comments