Tanzia : ZACHARIA HANS POPE AFARIKI DUNIA

Mwenyekiti wa Kamati ya Usajili ya Klabu ya Simba na Mjumbe wa Bodi ya Wakurugenzi wa Klabu hiyo, Zakaria Hans Pope amefariki dunia usiku huu Ijumaa, Septemba 10, 2021 katika Hospitali ya Agha Khan alipokuwa amelazwa akipatiwa matibabu.

Uongozi wa Klabu ya Simba umeeleza kupokea kwa mshtuko mkubwa taarifa za kifo cha Mjumbe wa Bodi ya Wakurugenzi, Zacharia HansPope ambaye amefariki dunia usiku huu.

"Uongozi wa Klabu ya Simba umepokea kwa mshtuko mkubwa taarifa za kifo cha Mjumbe wa Bodi ya Wakurugenzi, Zacharia HansPope ambaye amefariki dunia usiku huu.
Taarifa zaidi zitawajia kupitia kurasa" - imeeleza taarifa ya Simba SC

Zacharia Hans Pope ni nani?

Marehemu Zacharia Hans Pope alizaliwa mwaka 1956 jijini Dar-es-salaam na kukulia mjini Iringa.

Baada ya kumaliza elimu yake ya Sekondari, Hans Pope alijiunga na jeshi la wananchi (JWTZ) ambako alifikia cheo cha Kapteni, kabla ya kuachishwa kazina kuhukumiwa kifungo cha maisha jela, kwa tuhuma za uhaini dhidi ya serikali ya awamu ya kwanza ya Hayati Mwl. Julius Kambarage Nyerere mwaka 1983.

Lakini mwaka 1995, marehemu Hans Pope aliachiwa huru kwa msamaha wa Rais wa awamu ya pili, Alhaji Ally Hassan Mwinyi, mwezi mmoja kabla hajamaliza muda wake wa Urais.

Zacharia Hans Pope na Simba

Marehemu Hans Pope alianza kuipenda Simba kutoka moyoni mwaka 1970 akiwa kijana mdogo.

 Marehemu Hans Pope aliwahi kunukuliwa akisema mechi ambayo ilimfanya aipende Simba  ilikuwa dhidi ya watani wa jadi, Yanga, June 23, 1973 ambapo Simba iliishinda Yanga kwa jumla ya bao 1-0

Marehemu Hans Pope alijiunga na kundi la marafiki wa Simba (Friends of Simba) na baadaye kuchaguliwa kuwa Mwenyekiti wa Kamati ya Usajili wa Klabu ya Simba, jukumu alililolifanya kwa weredi mkubwa hadi mauti yalipomkuta siku ya Ijumaa, 10/09/2021 saa 4:05 usiku katika Hospitali ya Agha Khan alipokuwa amelazwa akipatiwa matibabu kwa maradhi yaliyokuwa yakimkabili.

Hakika wana Simba wamepoteza nguzo muhimu sana, hakika Taifa limepoteza mtu muhimu sana kwa maendeleo ya soka letu.

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527

0/Post a Comment/Comments