SERIKALI YATENGA TRILIONI 2.03 KUZIKWAMUA KAYA ZOTE MASKINI NCHINI

 Na. James K. Mwanamyoto-Dodoma
Serikali imetenga kiasi cha shilingi trilioni 2.03 kwa ajili ya kuzikwamua kaya zote maskini nchini kutoka katika lindi la umaskini ikiwa ni sehemu ya utekelezaji wa Mpango wa Kunusuru Kaya Maskini katika Kipindi cha Pili cha Awamu ya Tatu ya TASAF kilichoanza 2020 mpaka 2023.

Hayo yamesemwa na Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Mhe. Mohamed Mchengerwa wakati wa semina ya kuwajengea uwezo Wajumbe wa Kamati ya Bunge ya Kudumu ya Utawala na Serikali za Mitaa kuhusu utekelezaji wa Mpango wa Kunusuru Kaya Maskini nchini iliyofanyika leo katika ukumbi wa LAPF jijini Dodoma.

Mhe. Mchengerwa amesema, kwa kuwa Serikali imetenga fedha za kutosha kuzifikia kaya zote maskini, amewaomba wajumbe wa kamati hiyo kufanya ufuatiliaji ili kaya zote maskini zinazostahili kupata ruzuku zinanufaika.

“Kama kuna kaya yoyote maskini imesahaulika, nawaomba mtupatie taarifa haraka ili watendaji wetu wazifikie na kukamilisha taratibu za kuwawezesha kupata ruzuku na kuongeza kuwa, katika utekelezaji wa awamu hii, Serikali itahakikisha kila Mtanzania anayestahili kunufaika na mpango huu, anapata ruzuku,” Mhe. Mchengerwa amesisitiza.

Aidha, Mhe. Mchengerwa amesema licha ya TASAF kuziwezesha kaya maskini kiuchumi, pia imewawezesha watoto wa kike wanaotoka kwenye kaya hizo maskini kupata elimu kwa manufaa yao na taifa kwa ujumla.

Kwa upande wake, Mwenyekiti wa Kamati ya Bunge ya Kudumu ya Utawala na Serikali za Mitaa, Mhe. Humphrey Polepole (Mb) ameipongeza Serikali inayoongozwa na Mhe. Rais Samia Suluhu Hassan kwa azma yake ya kutenga fedha za kutosha kuziwezesha kaya zote maskini nchini.

Mhe. Polepole amesema, azma ya Mhe. Samia ya kutenga fedha hizo inaonesha nia ya dhati ya Serikali yake na Watendaji wake ya kuzikwamua kaya zote maskini.

Akiwasilisha mada kwa kamati hiyo, Mkurugenzi Mtendaji wa TASAF, Bw. Ladislaus Mwamanga amesema, idadi ya kaya za walengwa katika utekelezaji wa Mpango wa TASAF, Kipindi cha Pili cha Awamu ya Tatu inatarajiwa kufikia milioni moja laki nne na nusu, hivyo wanufaika kwenye kaya hizo watakuwa zaidi ya watu milioni 10.

Bw. Mwamanga amesema, ofisi yake imetekeleza zoezi la utambuzi wa kaya maskini kwa kushirikisha jamii na viongozi katika maeneo husika ili kutatua changamoto zilizojitokeza katika utekelezaji wa awamu iliyopita.

Katika kuhakikisha hakuna udanganyifu wakati wa zoezi la uandikishaji wa kaya maskini, Watendaji wanaohusika na zoezi hilo wamesainishwa kiapo cha kutekeleza jukumu hilo kwa uadilifu.



Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527

0/Post a Comment/Comments