HUAWEI YAWAPIGA MSASA WATALAAM 19 WA TEHAMA KUENDANA NA MABADILIKO YA TEHAMA


Mwakilishi kutoka Huawei Tanzania, Yohana Mathias (kushoto) akimkabidhi cheti Rweyemamu Barongo ambaye ni mmoja wa washiriki mafunzo ya uchakataji wa data kubwa yaliyotolewa jijini Dar es salaam na Kampuni ya Huawei Tanzania kwa kushirikiana na Tume ya Taifa ya Tehama kwa muda wa siku saba. Kulia ni Msimamizi wa shughuli za uendeshaji wa Tehama kutoka katika Tume hiyo, Mhandisi Jasson Ndanguzi
Mwakilishi kutoka Huawei Tanzania, Yohana Mathias (kushoto) akimkabidhi cheti Catherine Teodor ambaye ni mmoja wa washiriki mafunzo ya uchakataji wa data kubwa yaliyotolewa jijini Dar es Salaam na Huawei Tanzania kwa kushirikiana na Tume ya Taifa ya Tehama kwa muda wa siku saba. Kulia ni Msimamizi wa shughuli za uendeshaji wa Tehama kutoka katika Tume hiyo, Mhandisi Jasson Ndanguzi
Baadhi ya washiriki wa mafunzo ya uchakataji wa data kubwa yaliyoratibiwa na Kampuni ya Huawei Tanzania kwa kushirikiana na Tume ya Taifa ya Tehama jijini Dar es Salaa. Jumla ya watalaam 19 wa Tehama wamepatiwa mafunzo hayo ya siku saba.
Msimamizi wa shughuli za uendeshaji wa Tehama kutoka katika Tume hiyo, Mhandisi Jasson Ndanguzi akizungumza na washiriki wa mafunzo ya uchakataji wa data kubwa yaliayofanyika jijini Dar es Salaam kwa muda wa siku saba.
Mwakilishi kutoka Huawei Tanzania, Yohana Mathias akizungumza na washiriki wa mafunzo ya uchakataji wa data kubwa yaliayofanyika jijini Dar es Salaam kwa muda wa siku saba.
Washiriki mafunzo ya uchakataji wa data kubwa yaliyotolewa na Kampuni ya Huawei kwa kushirikiana na Tume ya Taifa ya Tehama kwa muda wa siku saba jijini Dar es salaam wakiwa katika picha ya pamoja.
***


Na Mwandishi  wetu
Kampuni ya Huawei Tanzania kwa kushirikiana na Tume ya Tehama imetoa mafunzo kwa wataalamu 19 wa Tehama kutoka katika sekta ya umma na binafsi kwa lengo la kuwaongezea ujuzi watalaam wazalendo. Anaripoti Mwandishi wetu. 

Akifunga mafunzo hayo jijini Dar es Salaam leo, Mwakilishi wa uongozi kutoka Kampuni ya Huawei Tanzania, Yohana Mathias amesema mafunzo hayo ni chachu katika kuendelea kuibua ubunifu mpya kwenye sekta ya Tehama.

Amesema mafunzo hayo yaliyofanyika kwa siku saba ni kielelezo tosha namna Huawei inashirikiana na Serikali katika kunoa Watanzania wengi waweze kumudu kufanya kazi kubwa zinazohusu uchakataji wa data badala ya kwenda kuchukua watalaam kutoka nje ya nchi.

“Huawei kila mara tumekuwa tukishirikiana na Serikali kutoa mafunzo ya aina hii kwa sababu tunaamini Tehama ni sekta ambayo inakua kwa kasi hivyo ni vema kuwaandaa Watanzania kuendana na mapinduzi ya nne ya viwanda duniani,” amesema.

Aidha, Msimamizi wa shughuli za uendeshaji wa Tehama kutoka Tume ya Taifa ya Tehama, Mhandisi Jasson Ndanguzi pamoja na kuishukuru kampuni ya Huawei kwa jitihada hizo, amesema mafunzo hayo ni moja ya mikakati ya Tume hiyo katika kutengeneza mpango wa Taifa wa miaka mitatu wa maendeleo.

Amesema mpango huo pia unalenga kuwasajili watalaam wa Tehama, pamoja na kuwaendeleza kwa kuwajengea uwezo ili kuenenda na maendeleo ya Tehama duniani.

“Ndani ya mapinduzi ya nne ya viwanda kunatumika teknolojia ya hali ya juu ndio maana Tume tumeona kuna haja ya kuwajengea uwezo mpya kwa sababu inawezekana teknolojia wanazotumia zinapitwa na wakati…na hii ndio sababu tunawashukuru sana wenzetu wa Huawei kwa jitihada zao katika kufanikisha mpango huu,’’

“Kwa hiyo mbali na mafunzo tunawasajili ili tuweze kujua tuna wanataalam wangapi kama nchi na watalaam hao kila mwaka na kila siku wanajiendeleza kivipi ili kama nchi tujue tuna ujuzi kiasi gani na tunaweza kunufaika vipi na fursa zilizopo kwenye Tehama,” amesema.

Ameongeza kuwa Serikali imekuwa ikiboresha miundombinu ya Tehama lakini sasa inaanza kuweka mkazo kwenye uboreshaji wa rasilimali watu ili Tanzania iwe na watalaam wa kutosha.

“Kwa hiyo mafunzo haya yanahusu big data analysis yaani uchakataji wa data kubwa ambazo zinaweza kusaidia kutoa taarifa sahihi na kuwezesha kufanya maamuzi sahihi ya kiutawala na kimaendeleo,” amesema.

Amesema tangu wazindua mpango wa mafunzo hayo Aprili mwaka huu, jumla ya washiriki 157 wamefaidika na kuongezewa ujuzi katika maeneo ya uchakataji wa data kubwa, usimamizi wa miradi ya Tehama, Cyber security na mafunzo mengine.

Aidha, Mmoja wa wakufunzi wa mafunzo hayo kutoka Huawei, Oscar Mashauri amesema Mwalimu amesema mafunzo hayo ni muarobaini kwa watalaam hao ambao walikuwa wanashindwa kuchakata data kubwa kwenye ofisi zao kwa kuwa hawakuwa na mbinu wala utalaam wa kuzichakata.

“Wameridhika na mafunzo kutoka Huawei kwa sababu wamegundua wanaweza kufanyia kazi wakiwa kwenye maofisi yao,” amesema.

Aidha, mmoja wa washiriki wa mafunzo hayo Rweyemamu Barongo ambaye ni mtaalam wa Tehama kutoka Benki Kuu ya Tanzania (BOT), amesema mafunzo hayo yanakwenda kuwapeleka kwenye ulimwengu mpya.

“Tuna imani yatatusaidia kwenye maeneo yetu ya kazi na kuonggeza ubunifu mpya kwa manufaa yetu na manufaa ya nchi kwa ujumla…na zaidi niishukuru sana kampuni ya Huawei kwa kufanikisha hili,” amesema.

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527

0/Post a Comment/Comments