TAKUKURU, CHAMA CHA SKAUTI TANZANIA WAZINDUA MWONGOZO KUPAMBANA NA RUSHWA

Naibu Waziri wa nchi,Ofisi ya Rais,Menejimenti ya Utumishi wa Umma  na utawala bora Deogratius Ndejembi  akiongea Kwenye uzinduzi wa  mwongozo wa mapambano dhidi ya rushwa

Na Dotto Kwilasa - Dodoma
SERIKALI kupitia Taasisi ya kuzuia na kupambana na rushwa nchini (TAKUKURU)imezindua Muongozo wa Mkakati wa makubaliano baina yake na Chama cha Skauti Tanzania wenye lengo la kusisitiza ushirikishwaji wa wadau katika mapambano dhidi ya rushwa  rushwa kuanzia ngazi ya chini.

Akiongea kwenye uzinduzi huo,Naibu Waziri wa nchi,Ofisi ya Rais,Menejimenti ya Utumishi wa Umma  na utawala bora Deogratius Ndejembi  amesema mwongozo huo utasaidia kujenga uchumi imara na kuchochea maendeleo ya huduma za kijamii.

Amesema Muongozo huo pia unajenga kuelimisha jamii kuacha vitendo vya rushwa huku akitoa   maelekezo  kwa maafisa elimu mikoa ,wilaya   na maafisa TAKUKURU, kuhakikisha wanatenga muda wa kuelimisha vijana na jamii kwa ujumla  kuhusu madhara ya rushwa.

Naibu Waziri Ndejembi amesema kutokana na kwamba vijana wengi wa Skauti wapo masomoni itakuwa rahisi kwao kufanya uelimishaji kupitia makundi mbalimbali huku akitoa agizo kwa wanufaika mafunzo hayo kupeleka kwa jamii elimu wanayoipata Kuhusu suala la rushwa.

Mbali na hayo ameeleza kuwa Serikali kwa upande wake itaendelea kuunga mkono juhudi hizo na kuleta mafanikio ambayo yatafikisha ujumbe kimataifa kwamba Skauti ni kundi muhimu linaloshiriki kurudisha haki kwa kuzingatia uzalendo na uwajibikaji.

Kutokana na hayo,Skauti Mkuu Mwantumu Mahiza ametumia nafasi hiyo kuwataka Viongozi na Wakuu wa idara  kuwapa ruhusa watumishi wa Umma kushiriki masuala ya Skauti pindi wanapohitajika na kuwapatia ruzuku Kwa ajili ya kujikimu Kwa kuwa kada hiyo haina fungu la ruzuku kwa wananchama wake.

Amefafanua kuwa,linapokuja Suala la Skauti kukutana ,baadhi ya Viongozi wa Taasisi za Serikali wamekuwa wagumu kutoa ruhusa kwa wafanyakazi wao ambao ni wananchama wa Chama cha Skauti Tanzania kwa kisingizia cha kutokiwa na ruzuku jambo ambalo amesema linabomoa miiko na maadili ya utumishi wa Umma.

"Ziko baadhi ya Taasisi ambazo hadi sasa hazielewi wala kutilia  maanani masuala ya skauti,kupitia hili naomba Serikali itoe mwongozo ili vijana wetu wa Skauti wasidharirike,Skauti sio uhuni,vijana hawa wana thamani ,wasomi na waadilifu lazima tuwaheshimu,"amesisitiza.

Mbali na hayo Skauti  huyo Mkuu nchini,ameiomba serikali kuwaona vijana hao wa Skauti pindi linapokuja Suala la uteuzi wa Viongozi na kuihakikishia Serikali kuwa vijana hao ni waadilifu na wawajibikaji wasiopenda rushwa.

Skauti Mkuu Tanzania,Bi.Mwantumu Mahiza amesema mwongozo huo wa kufundishia masuala ya rushwa utakuwa na tija kubwa kwani vijana walio wengi  hususan shuleni  ndio waathirika wa rushwa  kwa sababu rushwa huchelewesha maendeleo.

Aidha,amesema haiwezekani Tanzania tangu ipate uhuru mwaka 1961 bado inahangaika na miundombinu ya zahanati ,barabara kwani nchi zilizoendelea kuna masuala walishaacha na kujikita mambo mengine ya maendeleo.

Kwa upande wake Kaimu Mkurugenzi Mkuu TAKUKURU Neema Mwakalyelye amesema mwaka 2019 walisaini mkataba wa makubaliano na chama cha Skauti Tanzania katika mapambano dhini ya rushwa   na malengo ya mashirikiano hayo ni kuelimisha jamii madhara ya rushwa katika jamii .

Kupitia mkakati wa utekelezaji wa mwongozo huo,wanatarajia kuongeza upana wa makundi ya mapambano dhidi  ya rushwa  nchini ambapo kuna takriban vijana 105 wamenufaika na mafunzo hayo.

Mkurugenzi Elimu kwa Umma TAKUKURU  Dkt. Emmanuel Kiyabo amesema mafunzo hayo yamehusisha wadau mbalimbali ikiwemo chama  cha Maskauti Tanzania na watumishi kutoka TAKUKURU.

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527

0/Post a Comment/Comments