VICTOR THOBIAS AONGOZA KURA ZA MAONI CCM UCHAGUZI UDIWANI NDEMBEZI...CHIFU ABDALLAH SUBE APITISHWA KUGOMBEA KUPITIA DEMOKRASIA MAKINI


Katibu wa Siasa na Uenezi CCM wilaya ya Shinyanga Mjini, Saidi Ahmedi Bwanga

Na Mapuli Misalaba, Shinyanga
Uchaguzi wa kura za Maoni kumpata mgombea atakayepeperusha Bendera ya Chama Cha Mapinduzi (CCM) katika Uchaguzi mdogo wa nafasi ya udiwani katika kata ya Ndembezi Manispaa ya Shinyanga umefanyika leo ambapo ,Victor Thobias  ameongoza dhidi ya wagombea wenzake sita.

Victor amepata kura 41 kati ya kura 78 zilizopigwa akifuatiwa na  Bi. Pendo Sawa  ambaye amepata kura 28.

Akitangaza matokeo hayo katibu mwenezi wa CCM Wilaya ya Shinyanga Mjini , Said Bwanga amesema nafasi ya tatu imeshikwa na Bwana Solomon Najulwa ambaye amepata kura tatu,na kwamba nafasi ya Nne wamegongana watu watatu ambao ni Dotto Joshua, Samwel Jackson na Hamis Hamis ambapo kila mmoja amepata kura mbili, huku nafasi ya tano ikishikwa na  Gelewa Njelo ambaye amepata 0.

Bwanga amesema mchakato wa kumpata mteule atakayepeperusha bendera ya CCM katika Uchaguzi huo mdogo atapatikana kupitia mchujo wa vikao vya ngazi ya Wilaya na Mkoa.

Wakati huo huo Kamati Kuu ya Chama cha Demokrasia Makini Wilaya ya Shinyanga Mjini imemteua Bwana Chifu Abdallah Issa Sube kuingia kwenye kinyang’anyiro cha kugombea nafasi ya udiwani wa kata ya Ndembezi Manispaa ya Shinyanga

Mteule huyo ambaye pia ndiye Mwenyekiti na msemaji wa Chama cha Demokrasia Makini Mkoa wa Shinyanga, ameeleza kuwa vikao vinavyohusika na uteuzi vimemthibitisha kuwa ndiye mwakilishi atakayeingia kwenye kinyang’anyiro hicho na wagombea wa vyama vingine vya siasa.

“Nimechukua fomu leo hii ya kugombea nafasi ya udiwani kata ya Ndembezi nimechukua peke yangu sikuwa na mpinzani chama kimeniamini mchakato yatari umefanyika sehemu zote hakuonekana mtu yeyote kusimama basi jina langu likapitishwa”

Mchakato huo wa uchaguzi unafuatia aliyekuwa Diwani wa kata ya Ndembezi Manispaa ya Shinyanga David Nkulila kufariki dunia hivi karibuni ambaye pia alikuwa meya wa Manispaa ya Shinyanga.

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527

0/Post a Comment/Comments