SERIKALI YATOA SH. BILIONI 1.3 KUKAMILISHA UJENZI WA MRADI WA MAJI NJENDENGWA - IHUMWA JIJINI DODOMA

Na Dotto Kwilasa - Dodoma

JUMLA ya kiasi cha Sh.Bilion 1.3 zimetolewa na Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa ajili ya kukamilisha mradi wa maji wa Njendengwa -Ihumwa katika Jiji la Dodoma unaolenga kuwahudumia wakazi wa Njendengwa,Ihumwa,Nzuguni,Nyumba Miatatu,Iyumbu, Soko Kuu la Job Ndugai na FFU.

Hayo yamebainishwa leo 30 Agost 2021 na Waziri wa Maji Jumaa Aweso wakati alipofanya ziara ya kutembelea mradi huo wenye thamani ya sh.Bil 2.7.

Aweso amesema kuwa awali serikali ilitoa kiasi cha sh.Bil.1.4 kwa lengo la kuifanya makao makuu ya nchi kuondokana na adha ya maji ambayo ilikuwa ikiwakumba wananchi.

"Tunajua serikali inayoongozwa na Mama Samia Suluhu Hasani ni seriki abayo inawajali wananchi wa hali ya chini.

"Pamoja na kuwajali watu wa hali ya chini inakusudia kumtua mama ndoo kichwani kwa maana hiyo mama yetu Suluhu Hasani ameona ni vyema kuwawezesha wakazi wa Dodoma ambapo ni makao makuu ya nchi kiasi cha sh Bilioni 2.7 kwa ajili ya usambazaji wa maji katika maeneo tajwa.

"Awali Rais alitoa kiasi cha sh.bilioni 1.4 kwa ajili ya mradi huo wa maji,na sasa nimefanya ziara ya kutembelea na nimejiridbisha kuwa mradi unaenda vizuri,kwa maana hiyo sasa namuagiza Katibu Mkuu Wizara ya Maji Mhandisi Antony Sanga Kuhakikisha anatoa fedha zilizobaki kwa ajili ya kumaliza mradi huo ili kutatua changamoto ya maji katika jiji la Dodoma "amesema Aweso.

Pamoja na kuagiza fedha hizo zitolewe pia amemwagiza Mkurugenzi wa Mamlaka ya Maji safi na Usafi wa Mazingira( DUWASA) Mhandisi Aron Kasekwa kuhakikisha anasimamia mradi huo na kukamilika ndani ya miezi miwili kuanzia sasa.

Pamoja na mambo mengine Aweso amesema Kwa Mamlaka aliyonayo amemtangaza Mhandisi Mayunga Kashilimu ambaye alikuwa Meneja Ufundi DUWASA kuwa Meneja wa Mamlaka za Maji na kueleza kuwa Katibu Mkuu atamwandikia barua na kumpangia Mamlaka mojawapo.

Sambamba na hilo ameiagiza Bodi ya DUWASA kuona namna bora ya kumpatia ajira,mhandisi wa kujitolea James Ryoba ambaye amekuwa akifanya kazi ya kuunganisha mabomba ya maji ya mradi huo kwa kujitolea.

Kwa upande wake Mkurugenzi wa Mamlaka ya Maji safi na Usafi wa Mazingira, mhandisi Aron Joseph amesema mradi huo pamoja na kuwa umefikia hatua mzuri lakini changamoto ni kuwepo kwa miamba wakati wa uchimbani wa mitaro ya utandazaji wa mabomba.

"Changamoto tuliyonayo ni kukutana na miamba mizito wakati wa muchimba mitaro ya utandikaji wa mabomba,upitaji katika maeneo kwani maeneo mengi yamepimwa na ni viwanja vya watu.

"Lakini nataka kukuambia mheshimiwa Waziri mwanzoni mradi ulikuwa ni sh.Bilioni 2.4 lakini kutokana na muwepo kwa janga la Covid-19 vifaa vilipanda na kusababisha mradi kufikia kiasi cha Sh.Bilioni.2.7",amesema Mkurugenzi wa DUWASA.

Kwa upande wake Katibu wa CCM Mkoa wa Dodoma,Pili Mbaga akimkaribisha Waziri wa Maji Jumaa Awesso amesema kuwa pamoja na kuwa kwa sasa Changamoto ya maji imepungua kwa kiasi kikubwa lakini bado kuna sehemu zenye changamoto ya maji.

Ameyataja maeneo hayo kuwa ni pamoja na wilaya ya Kondoa na eneo la Nala katika Halmshauri ya Jiji la Dodoma.

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527

0/Post a Comment/Comments