Mashindano ya Mchezo wa Mpira wa miguu Kata ya Kolandoto Manispaa ya Shinyanga, ambayo yameandaliwa na Diwani wa Kata hiyo Mussa Andrew, yameanza kurindima leo katika viwanja vya michezo katika Shule ya Msingi Kolandoto.
Akizungumza kwenye uzinduzi wa Ligi hiyo, Andrew amesema ameamua kuanzisha mashindano hayo kwa lengo la kuibua vipaji vya vijana kupitia Soka.
Amesema kwenye kipindi cha Kampeni za uchaguzi Mwaka 2020, aliwaahidi vijana wa Kata hiyo kuanzisha Timu ya Kata pamoja na kuwapatia Mipira ,ahadi ambayo ameanza kuitekeleza kwa kuanzisha Ligi hiyo.
"Mashindano haya ni utekelezaji wa ilani ya uchaguzi ya Chama cha Mapinduzi CCM, ambayo niliahidi kwenye kipindi cha Kampeni kuwa nitaibua vipaji vya vijana kupitia michezo," amesema Andrew.
"Zawadi ambazo nitazitoa ni kwa mshindi wa kwanza ambaye atapewa Jezi pamoja na Mpira, na timu zote ambazo zimeshiriki zitapewa mpira, lengo la mashindano haya ni kuibua vipaji vya vijana," ameongeza.
Naye,Mtendaji wa Kata ya Kolandoto Wilson Mwakaluba, amewataka vijana hao watumie fursa ya mashindano hayo, kujitangaza katika timu zingine kwa sababu mpira ni ajira, ambapo wataweza kusajiliwa kwenye Timu zingine kubwa.
Aidha, Mwenyekiti wa Chama cha Mapinduzi CCM Kata ya Kolandoto Shija Nkingwa, amempongeza Diwani huyo kwa kuanzisha ligi hiyo, huku akiwataka vijana wacheze kwa nidhamu na kudumisha amani na siyo kuchezeana vibaya.
Kwa upande wao vijana, wamepongeza kuanzishwa kwa mashindano hayo, huku wakiahidi kucheza kwa nidhamu ya juu na kuonyesha vipaji vyao, na kuahidi kupata ushindi kwenye Ligi ya Wilaya pale itakapoanza kurindima.
Ligi hiyo itadumu ndani ya wiki mbili ambayo imeshirikisha Timu Nane kutoka vitongoji vya, Mwasimba, Wame, Mwamala, Kabondo, Luhumbo, Mwanubi, Kapine, pamoja na wenyeji Kolandoto.
Na Marco Maduhu.
No comments:
Post a Comment