MBUNGE NEEMA LUGANGIRA AGUSWA NA KAMPENI YA NAMTHAMINI AMWAGA TAULO ZA KIKE KWA WANAFUNZI

 

Mbunge Viti Maalum kupitia Chama cha Mapinduzi (NGOs Tanzania Bara) Mhe. Neema Lugangira akiwasilisha mchango wa Taulo za Kike kwa wanafunzi 42 mwaka mzima (dozen 42, packet 504), katika Ofisi za EATV, Mikocheni ikiwa ni kuunga mkono kampeni ya Namthamini

Mbunge Viti Maalum kupitia Chama cha Mapinduzi (NGOs Tanzania Bara) Mhe. Neema Lugangira amewasilisha mchango wa Taulo za Kike kwa wanafunzi 42 mwaka mzima (dozen 42, packet 504), katika Ofisi za EATV, Mikocheni ikiwa ni kuunga mkono kampeni ya Namthamini. 

Akizungumza baada ya kukabidhi mchango huo amesema kuwa kampeni ya Namthamini isiishie tu kwa wanafunzi mashuleni lakini pia ifike katika Magereza ili kusaidia pia wafungwa na mahabusu wakike ambao taulo hizo za kike pia ni changamoto kwao. 

“Nimeguswa na kampeni ya Namthamini na nimekuwa nikifanya hivyo kupitia Taasisi ya Agri Thamani ambayo mimi ni Mkurugenzi kwa lengo la kuhakikisha tunasaidia Watoto wa Kike kubaki Shule hasa madarasa yale ya mitihani (Kidato cha 2 na cha 4) ili Watoto hawa wasipoteze ndoto zao. Kwa mwaka huu 2021 kupitia Agri Thamani tulitoa Taulo za Kike za Mwaka Mzima kwa Wanafunzi wa Kike 1,800 wa Sekondari 16 za Kata za Bukoba Manispaa, Kagera kwa Kidato cha 2 na cha 4 na pia tulitoa kwa Wanafunzi wa Kike 3,700 wa Sekondari kutoka Mikoa 19 Tanzania Bara na Zanzibar na tutafanya tena mwakani 2022”, amesema Mh. Lugangira. 

Mheshimiwa Lugangira amesema pia yeye kama Mbunge amekuwa akitoa Msaada wa Taulo za Kike kwa Wafungwa na Mahabusu Wanawake ambao nao pia wanauhitaji mkubwa na mara nyingi wanasahaulia. 

Akiwa kama Mdau wa Masuala ya Local Content, Mh. Lugangira alisisitiza umuhimu wa kuthamini Viwanda vya Ndani vinavyozalisha Taulo za Kike zenye Ubora zinatakiwa kupewa nguvu katika uzalishaji wake kwa kuunga mkono wafanyabiashara wa ndani. 

“Nimeleta taulo hizi ambazo zinatengenezwa na kiwanda cha ndani chenye uzoefu wa zaidi ya miaka 40 ili kusisitiza Uzalendo kwanza kwa vitendo, tuthamini vya ndani na suala la hedhi salama kwa wanafunzi wa kike, wafungwa na mahabusu wa kike imekuwa ni moja ya hoja zangu hata ninapokuwa Bungeni”, amesema Lugangira.

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527

0/Post a Comment/Comments