SHINDANO: UANDISHI WA MTANDAONI WENYE KULETA TIJA 'STORIES OF CHANGE'



Jamii Forums (JF) ni Asasi ya Kiraia inayoratibu mtandao wa JamiiForums na kuhamasisha Haki za Kidigitali, Demokrasia, Uwajibikaji na Utawala Bora.


Hadi kufikia Juni 2021, Tanzania ina watumiaji takribani milioni 30 wa Intaneti na Serikali imebainisha dhamira yake kuwa ifikapo mwaka 2025 nchi iwe na zaidi ya watumiaji milioni 50. Ongezeko hili la watumiaji wa mtandao nchini linamaanisha kuongezeka kwa watengenezaji na walaji wa maudhui ya mtandaoni hivyo kutengeneza uhitaji wa maudhui bora na yenye tija kwa umma.

Jamii Forums imekuwa mstari wa mbele katika kuhamasisha uandishi wa maudhui bora na yenye tija mtandaoni kwa zaidi ya miaka 15 kwa kutoa jukwaa la umma kwa wananchi (citizen journalists) kujieleza bila uoga, kuwawajibisha viongozi wao na kujenga uelewa zaidi katika masuala anuai. Ni kupitia safari hii na kujitolea kwake kwa Utetezi wa Haki za Dijitali, Jamii Forums inaendelea kutekeleza jukumu lake katika kuhakikisha mtandao unabaki mahali salama ambapo umma wa Watanzania unaweza kupata habari/taarifa bora na pia kutengeneza maudhui yanayochochea mabadiliko chanya.

Hivyo basi, JF inatoa nafasi kwa wadau wake na wananchi wote wenye uwezo wa kutayarisha maudhui kushiriki kwenye mashindano ya uandishi wa maudhui mtandaoni wenye kuleta mabadiliko(Stories of Change).

Awamu ya kwanza ya shindano hili itaanza Julai 14 hadi Septemba 15, 2021.

Shindano hili linakusudia kuongeza maudhui bora mtandaoni hususani ya lugha ya Kiswahili kwa ajili ya vizazi vya sasa na vya baadaye. Pia, tunalenga kuhamasisha ushiriki wa raia pamoja na makundi yasiyopewa vipaumbele kama watu wanaoishi na ulemavu kushiriki katika ukusanyaji na utayarishaji wa taarifa nchini.

Vigezo na masharti ya kushiriki katika shindano hili:
  • Mshiriki anatakiwa kutayarisha andiko linalochochea mabadiliko kwenye nyanja za Uchumi na Biashara, Afya, Maendeleo ya Jamii, Utawala Bora na Uwajibikaji, Demokrasia, Kilimo, Sayansi na Teknolojia, Haki za Binadamu n.k.
  • Andiko linaweza kuwa la Kiswahili au Kiingereza lenye maneno yasiyozidi 1,500.
  • Mshiriki atapewa saa 2 tu kulihariri andiko lake baada ya kulichapisha jukwaani hivyo atatakiwa kuwa makini katika uwasilishaji wake
  • Watendaji wa Jamii Forums na ndugu zao wa karibu hawaruhusiwi kushiriki kwenye shindano hili
  • Mshiriki anaweza kutumia jina la kubuni ‘pseudo name’ lakini atatakiwa kutoa ushirikiano endapo ataibuka mshindi
  • Makala zinatakiwa kuwa habari au makala halisi zisizowahi kuchapishwa sehemu nyingine yoyote. Plagiarism haitaruhusiwa
  • Matumizi ya picha au video yanaruhusiwa ili kushibisha andiko. Endapo picha na video sio za mshiriki atalazimika kutaja chanzo
Jinsi ya kushiriki:
  • Mtanzania yeyote mwenye umri wa miaka 18 na zaidi anaweza kushiriki, lakini ili kuchapisha Makala yako itakulazimu kuwa mwanachama wa JamiiForums. Endapo sio mwanachama unaweza kujisajili kupitia => (www.jamiiforums.com/register/ ). Ukipata changamoto katika usajili, wasiliana nasi kupitia mawasiliano yaliyowekwa chini katika bandiko hili
  • Maandiko yawasilishwe kati ya Julai 14 – Septemba 15, 2021 kwenye jukwaa la “JF stories of change” (Stories of Change )
  • Baada ya kuweka andiko lako jukwaani, JITAHIDI kushiriki kwenye mjadala utakaotokana nalo kwa kutolea ufafanuzi hoja zitakazoibuka ili kuupa mjadala uhai na kuwashawishi wanachama kukupigia kura
ZINGATIA: Unaweza kuandika mara nyingi kadiri uwezavyo ili kujiongezea nafasi ya ushindi.

Zawadi kwa Washindi

Washindi watapatikana kwa kuzingatia kura zitakazopigwa kwenye mnakasha (thread) husika na pia uamuzi wa jopo la wataalamu wa lugha, uandishi na ushirikishaji jamii.

Washindi watatangazwa kwenye jukwaa la JamiiForums “Stories of Change” na kurasa za Jamii Forums katika mitandao ya kijamii (Twitter, Facebook, Instagram na Telegram) na si vinginevyo

Zawadi kwa Washindi zitakuwa kama ifuatavyo:-

Mshindi wa Kwanza atapata fedha taslimu shilingi Milioni 5
Mshindi wa Pili atapata fedha taslimu shilingi Milioni 3
Mshindi wa Tatu atapata fedha taslimu shilingi Milioni 2

Zawadi nyingine zitahusisha Laptop, Tablet na Simu za mkononi.

Mawasiliano
Kwa mawasiliano zaidi wasiliana nasi kupitia namba ya simu: +255 743440000 (WhatsApp, Telegram na Signal) au barua pepe: stories@jamiiforums.com

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527

0/Post a Comment/Comments