Majaliwa: Tufanye Mazoezi Ili Tujiepushe Na Magonjwa


WAZIRI MKUU Kassim Majaliwa amewataka wananchi wabadili mitindo ya maisha yao kwa kujijengea utaratibu wa kufanya mazoezi ya mara kwa mara ili wajiepushe na maradhi mbalimbali pamoja na kuimarisha afya ya mwili na akili.

Ametoa agizo hilo leo (Jumamosi, Juni 12, 2021) wakati akizindua Bonanza la Michezo lililoandaliwa na Benki ya CRDB kwa kushirikiana na Ofisi ya Bunge na Ofisi ya Waziri Mkuu “CRDB Bank Pamoja Bonanza” lililofanyika katika Uwanja wa Jamhuri, Dodoma.

“Bonanza hili la leo limeandaliwa kwa ajili ya kutuhamasisha sisi wafanyakazi umuhimu wa mazoezi katika kujenga na kuimarisha afya zetu na litatusaidia kuboresha utendaji wetu sehemu za kazi. Kama mnavyofahamu wengi tumekuwa wahanga wa magonjwa yasiyoambukiza.”

Mheshimiwa Majaliwa amesema magonjwa hayo ambayo yanachangiwa kwa kiasi kikubwa na matumizi ya vilevi kama sigara na pombe, kutoshiriki mazoezi au shughuli za nguvu na kutozingatia lishe bora yamekuwa chanzo cha gharama kubwa za afya kwa Serikali na kupotea kwa nguvu kazi ya Taifa.

“Nitoe rai kwa washiriki na Watanzania kwa ujumla kushiriki mazoezi au shughuli za nguvu na kuzingatia mlo sahihi kwa ajili ya kujikinga na maradhi hayo kwani siku zote “Kinga ni Bora, Kuliko Tiba”. Tuendelee kuunda vikundi vya mazoezi ya ukakamavu (Jogging) na kushiriki matamasha mbalimbali ya michezo.”

Kadhalika, Mheshimiwa Majaliwa ametoa wito kwa Maafisa Utamaduni nchini kote waendelee kuunda vikundi kwa ajili ya kufanya mazoezi ili kuwawezesha watu wengi kushiriki katika mazoezi. “…Lazima kila Halmashauri iandae viwanja vitakavyowawezesha wananchi washiriki katika mazoezi.”

Amesema bonanza hilo ni utekelezaji wa wito wa Rais Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan ambaye amekuwa akisisitiza juu ya kuwaleta watu wote pamoja na kushirikiana katika kujenga uchumi wa Taifa. Nikimnukuu Mheshimiwa Rais katika hotuba yake amewahi kusema “Tukitaka kufika mbali ni lazima tutembee na wenzetu.”

Amesema Ofisi ya Waziri Mkuu imekuwa katika mkakati wa kulitekeleza jambo hilo kwa kuwaleta wadau wote pamoja, Serikali na taasisi zake, sekta binafsi pamoja na wadau wa maendeleo kutoka ndani na nje ya nchi ili waweze kufahamiana, kubadilishana uzoefu kwenye masuala mbalimbali na kujadili mikakati ya pamoja yenye manufaa kwa Taifa.

Amesema utekelezaji wa mkakati huo unahusisha makongamano, vikao kazi pamoja na shughuli nyingine rasmi zenye lengo la kufahamiana na kujenga mahusiano kama bonanza la leo ambalo linahusisha Wizara mbalimbali, Bunge na Benki ya CRDB.

(Mwisho)
IMETOLEWA NA:
OFISI YA WAZIRI MKUU


Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527

0/Post a Comment/Comments