VIJANA WALIOANZISHA KIWANDA CHA CHAKI SHINYANGA WALIA KUKOSA SOKO...WAMUANGUKIA RC

 

Mwenyekiti wa kikundi cha Uzalendo cha vijana 15 Manispaa ya Shinyanga Hashimu Issa, akionyesha chaki ambazo wanazitengeneza kiwandani hapo.

Na Marco Maduhu, Shinyanga.
Kikundi cha vijana 15 ambao ni wakazi wa Manispaa ya Shinyanga, walioanzisha kiwanda cha kutengeneza Chaki kwa ajili ya kujikwamua kiuchumi, wamemuomba Mkuu wa Mkoa wa Shinyanga Zainab Telack, kuwaunga mkono kwa kutoa maagizo kwa shule zote mkoani humo zinunue chaki kutoka kiwandani hapo.

Mwenyekiti wa kikundi hicho Hashimu Issa, akizungumza na Waandishi wa habari walipotembelea kwenye kiwanda hicho cha Chaki, amesema katika mkoa mzima wa Shinyanga wao pekee ndiyo wenye kiwanda cha Chaki, hivyo wanaomba uungwaji Mkono na Serikali ili wakue kiuchumi na kuchangia pato la Taifa.

Amesema kiwanda hicho walikianzisha mwaka jana, kupitia fedha za mkopo bila riba za Halmashauri asilimia nne za vijana Sh. Milioni 24.2 ili wajikwamue kiuchumi na kuendesha maisha yao kwa kujiajiri wenyewe, na kubainisha wanauwezo wa kuzalisha Chaki Boksi 30 kwa siku zenye  vipande 100 lakini hakuna soko la kutosha.

“Changamoto ambayo tunakabiliana nayo kwa sasa ni ukosefu wa Soko la kutosha, sababu tunauza chaki hizi kwenye Shule za Serikali tu zilizopo Manispaa ya Shinyanga, ambapo tunauwezo wa kuuza chaki kwa shule zote mkoani Shinyanga zikiwamo na binafsi,”alisema Issa.

“Kutokana na changamoto hii ya Soko, tunamuomba Mkuu wetu wa Mkoa wa Shinyanga, atuunge mkono kwa kutoa maagizo kuwa shule zote mkoani hapa, zinunue chaki kutoka kwenye kiwanda chetu, kama walivyofanya mkoani Simiyu kwenye kiwanda cha Chaki wilayani Maswa, sababu kwa mkoa mzima wenye kiwanda cha chaki ni sisi tu, ili tukue na kuchangia pato la taifa,” aliongeza.

Aidha alisema kiwanda hicho kitakapopanuka, kitaongeza ajira nyingi kwa vijana tofauti na walivyo hivi sasa 15, na kuomba uugwaji wa mkono ili waendelee kutatua changamoto ya ukosefu wa ajira kwa vijana mkoani Shinyanga.

Kwa upande wake Mkuu wa Wilaya ya Shinyanga Jasinta Mboneko, ambaye alitembelea kiwanda hicho hivi karibuni, aliwapongeza vijana hao na kutoa maagizo kwa walimu na wakuu wote wa Shule wilayani humo kununua chaki kiwandani hapo, huku akiahidi kuwatafutia masoko zaidi.

TAZAMA PICHA HAPA CHINI
Mwenyekiti wa kikundi cha Uzalendo cha vijana 15 Manispaa ya Shinyanga Hashimu Issa akielezea changamoto ambayo wanaipata kwenye utengenezaji wa Chaki, kuwa ni Masoko.
Hashimu Issa akiwa kwenye Mashine ya kutengeneza chaki.
Hashimu Issa, akionyesha chaki ambazo wanatengeneza kiwandani hapo.
Hashimu Issa, akionyesha chaki ambazo wanatengeneza kiwandani hapo.
Mkuu wa Wilaya ya Shinyanga Jasinta Mboneko, (kushoto) hivi karibuni akiwa kwenye kiwanda hicho cha kutengeneza chaki, akiona namna vijana walivyojiajiri wenyewe kupitia fedha za vikundi vya mkopo wa vijana wa Halmashauri.
Mkuu wa Wilaya ya Shinyanga Jasinta Mboneko, akiangalia ubora wa Chaki.

Na Marco Maduhu- Shinyanga.

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527

0/Post a Comment/Comments