SEKTA YA UVUVI YAFANIKIWA KUPUNGUZA BIASHARA HARAMU YA MAZAO YA UVUVI KWA ASILIMIA 80

Waziri wa Mifugo na Uvuvi Mhe.Mashimba Ndaki akizungumza wakati akifungua  mkutano wa wadau wa sekta ya uvuvi katika ukumbi wa mikutano wa Kimataifa wa Julius Nyerere leo mjini Dar es Salaam. Wadau wa sekta ya Uvuvi wakifuatilia mkutano wa wadau hao katika ukumbi wa mikutano wa Kimataifa wa Julius Nyerere leo mjini Dar es Salaam. Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais (Uwekezaji), Prof. Kitila Mkumbo akizungumza katika mkutano wa wadau wa sekta ya uvuvi katika ukumbi wa mikutano wa Kimataifa wa Julius Nyerere leo mjini Dar es Salaam.

Naibu Waziri wa Mifugo na Uvuvi, Mhe. Pauline Gekul akizungumza katika katika mkutano wa wadau wa sekta ya uvuvi katika ukumbi wa mikutano wa Kimataifa wa Julius Nyerere leo mjini Dar es Salaam.

Waziri Mstaafu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe.Mizengo Pinda akizungumza katika katika mkutano wa wadau wa sekta ya uvuvi katika ukumbi wa mikutano wa Kimataifa wa Julius Nyerere leo mjini Dar es Salaam.

Waziri wa Mifugo na Uvuvi Mhe.Mashimba Ndaki akipata picha ya pamoja na wadau mbalimbwa wa sekta ya uvuvi katika mkutano wa wadau wa sekta ya uvuvi katika ukumbi wa mikutano wa Kimataifa wa Julius Nyerere leo mjini Dar es Salaam.


NA EMMANUEL MBATILO, DAR ES SALAAM

Sekta ya Uvuvi imefanikiwa kupunguza uvuvi na biashara haramu ya mazao ya uvuvi kwa asilimia 80 kwa upande wa maji baridi na asilimia 100 kwa matumizi ya vilipuzi katika Ukanda wa Bahari ya Hindi. 

Waziri wa Mifugo na Uvuvi Mhe.Mashimba Ndaki ameyasema hayo leo wakati akifungua  mkutano wa wadau wa sekta ya uvuvi wa siku tatu katika ukumbi wa mikutano wa Kimataifa wa Julius Nyerere mjini Dar es salaam.

Aidha Mhe.Ndaki amesema Serikali inatarajia kuanza utekelezaji wa Programu ya Kuendeleza Kilimo na Uvuvi chini ya ufadhili wa Mfuko wa Kimataifa wa Kuendeleza Kilimo (IFAD). Programu hiyo imelenga kununua meli nane (8) zitakazokabidhiwa kwa Shirika la Uvuvi Tanzania (TAFICO) meli nne (4) na Kampuni ya Uvuvi ya Zanzibar (ZAFICO) meli nne (4).

Amesema serikali inaendelea na mpango wa kufufua Shirika la Uvuvi Tanzania (TAFICO) ambapo kazi mbalimbali zimefanyika ikiwemo uandaaji wa Mpango Biashara (Business Plan) wenye maeneo matatu makubwa. Maeneo hayo ni uvuvi wa bahari kuu, ufugaji samaki na uchakataji wa mazao ya uvuvi.

Pamoja na hayo Mhe.Ndaki ametoa wito kwa wadau kutumia fursa ya mkutano huo kuainisha changamoto zinazoikabili sekta hiyo kuanzia ngazi ya mvuvi mmoja mmoja, Vyama vya Wavuvi, Wachakataji wa samaki na mazao yake, Serikali na Washirika wa Maendeleo.

“Tumieni jukwaa hili kuzijadili changamoto hizo na kisha kuwasilisha Wizarani mapendekezo ya namna bora ya kuzipatia ufumbuzi. Vilevile, ainisheni wahusika na muda wa utatuzi wa changamoto hizo kwa kuzingatia kuwa zipo changamoto ambazo utatuzi wake ni wa muda mfupi, wa kati na mrefu”. Amesema Mhe.Ndaki.

Hata hivyo Mhe.Ndaki amesema kuwa katika mwaka 2020, jumla ya tani 497,567 za samaki zenye thamani ya shilingi trilioni 2.34 zilivunwa ikilinganishwa na tani 362,645 zenye thamani ya trilioni 1.48 mwaka 2015/2016. Kati ya tani hizo, tani 435,408.9 ni kutoka maji baridi na tani 62,158.38 zilitoka maji chumvi mwaka  2020 ikilinganishwa na tani 409,332.72 zilizovunwa kutoka maji baridi na tani 60,976.51 kutoka maji chumvi mwaka 2019. Ongezeko la uvunaji wa rasilimali za uvuvi umetokana na kupungua kwa vitendo vya uvuvi haramu hali iliyosababisha kuongezeka kwa samaki katika maji yetu.

Kwa upande wake Naibu Waziri wa Mifugo na Uvuvi, Mhe. Pauline Gekul amesema kuwa katika mkutano huo watajadili mambo mengi yanayohusiana na sekta ya uvuvi na kuona ni changamoto gani wananzipitia na kisha kuzitatua ili kuweza kukuza sekta hiyo.

Aidha Mhe.Gekul amesema mpaka sasa zaidi ya watu milioni 4.5 wanajihusisha na sekta ya uvuvi ambapo wanategemea kuongeza ajira zaidi ya elfu 30 katika sekta hiyo.

“Tutaangalia na kujadili vikwazo ambavyo wanapitia kwenye viwanda vyetu na kuona viwanda hivyo vinaweza kuendelea na kuongeza ajira ambapo mpaka sasa tuna viwanda 14 katika sekta hii vinafanya kazi ikiwa 9 kule Ziwa Victoria na 5 katika ukanda wa bahari, hivi vinatosha  na kuchakata mazao yanayotokana na uvuvi”. Amesema Mhe.Gekul.

 



Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527

0/Post a Comment/Comments