NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII ATAKA WANANCHI KUTEMBELEA VIVUTIO


Naibu Waziri wa Maliasili na utalii Mary Masanja 
Wajumbe wa bodi ya Barabara wakipitia agenda za kikao.
**

Na Hellen Mtereko Mwanza

NAIBU Waziri wa Maliasili na Utalii Mary Masanja amewataka wananchi  kuweka utaratibu  wa kutembelea vivutio vya utalii vilivyopo  nchini  na siyo kuwaachia  wageni kutoka nje ya nchi.

Ametoa wito huo leo Februari 25, 2021 kwenye  kikao  cha pili cha bodi ya barabara ya mkoa wa Mwanza kwa mwaka wa fedha 2020/2021 kilichofanyika jijini Mwanza.

  Alisema ni vyema kila mtu  atembelee vivutio vilivyopo nchini kwa  kufanya utalii kwenye hifadhi na mbuga  zilizopo ili kuweza kujionea wanyama wa aina mbalimbali.

Alisema Watanzania wanapaswa kuwa wazalendo kwa kupenda  vivutio vyao kwa kuvitangaza kila sehemu  kwani  kuanzia mwaka 1993 kulikuwa na watalii waliokuwa wakiingia  kwenye hifadhi zetu 230000  ambapo mwaka 2019 idadi ya watalii iliongezeka na kufikia Milioni 1.5.

"Watanzania tupo wengi  kwa sasa lakini ukiangalia idadi ya watu wanaoingia kwenye hifadhi zetu  na kuangalia utalii ni wachache kuliko  idadi ya watu waliopo nchini hali hii inaonyesha sisi siyo wazalendo ni  vyema tupende  utalii wa kwetu wa ndani .Tunaendelea kuhamasisha watu wafanye utalii wa ndani ni lazima tupende vyetu vya ndani",alieleza

Ameongeza kuwa kila mmoja anapaswa kuwa balozi wa kutangaza vivutio kwenye mtandao kupokea watalii kutoka ndani na nje  kwani kufanya hivyo kutapelekea kuongeza pato la mtu mmoja mmoja na taifa kwa ujumla.

"Tuna mpango wa kuanzisha utalii wa majini  ambao utatumia Ziwa Victoria  kwa kutumia meli, watakuwa wakitoka Serengeti watapita Saa Nane kwenda Kisiwa cha Lubondo, watakuwa na uwezo wa kwenda  Chato. Halii hii itasaidia kutangaza hifadhi ya Buligi Chato na tunawahamasisha wafanya biashara kuandaa pakeji ili itakapokuwa tayari watalii watapita maeneo hayo na kuona utalii wa majini na wa nchi kavu",alisema.

Hata hivyo alisema kutokana  na barabara kuchangia kwa asilimia kubwa   ongezeko la watalii nchini ni vyema wakala wa barabara  vijijini na mjini (TARURA) kuona umuhimu  kuzitengeneza ili kusaidia kupitika kwa urahisi.

"Barabara zilikiwa hazijatengenezwa vizuri inakuwa changamoto kupitika ni vyema Wakala wa Barabara vijijini na mjini (TARURA)  kuona  umuhimu wa kizitengeneza  na ikiwezekana kuongeza bajeti ili kusaidia kwenye matengenezo hayo na ziweze kupitika   na zitasaidia  kuvutia watalii na kufika eneo husikakwa urahisi na kwa wakati,",alisema Masanja.

Kwa upande wake  Meneja wa TARURA mkoa wa Mwanza Mhandisi Mohamed Muanda alisema kutokana na bajeti iliyotolewa watahakikisha wanarekebisha Barabara hizo hususani maeneo korofi ili zisaidie katika kutangaza utalii.

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527

0/Post a Comment/Comments