MSITA : TOENI KIPAUMBELE KWA WANAFUNZI WENYE ULEMAVU

 
Madiwani wa Halmashauri ya Itigi wakiwa wanapitia makabrasha yao yenye bajeti ya mwaka wa fedha 202122 kwa ajili ya kuijadili, kupendekeza na hatimaye kuipitisha.

Na Abby Nkungu, Itigi

 

HALMASHAURI ya Mji wa Itigi wilayani Manyoni mkoani hapa imetakiwa kuangalia kwa jicho la pekee suala la utoaji wa elimu kwa watoto wenye mahitaji  maalum kwa kuweka miundombinu yote muhimu shuleni pamoja na kuboresha mazingira ya kufundishia na  kujifunzia.

Wito huo ulitolewa  mjini  Itigi  na baadhi ya  madiwani wa halmashauri hiyo kwenye kikao  maalum cha  baraza la madiwani kwa ajili ya kupitisha mapendekezo ya bajeti kwa mwaka wa fedha  2021/ 2022.

Mmoja wa madiwani hao Viti maalum ( Walemavu) tarafa ya Itigi,  Mhe Amina Msita alisema licha ya  Halmashauri  hiyo kuwa  na Shule ya msingi Mchanganyiko Mlowa ambayo ndio  pekee inayochukua watoto wenye mahitaji maalum  bado  haina miundombinu  rafiki kwa ajili ya kundi hilo.

"Mheshimiwa Mwenyekiti, kabla ya kupitisha bajeti hii naomba kutoa angalizo juu ya Shule ya msingi mchanganyiko Mlowa yenye walemavu zaidi ya 40. Kuna haja ya kuongeza bajeti kwa ajili ya ujenzi wa miundombinu rafiki ya majengo kwa kundi hili" alisema na kuongeza;

 Baadhi ya wanafunzi waliopo wanaishi kwa ndugu, jamaa au kwa walimu waliojitolea kuishi nao kutokana na ukweli kwamba wanatoka mbali, takriban kilomita 200 kutoka shule ilipo;  hivyo  kuna haja kwa shule hiyo kuongezewa madarasa, kujengewa mabweni, jiko na bwalo la chakula.

Alisema  kuwa iwapo  ujenzi wa miundombinu  hiyo  utafanyika na  kununua vifaa vya  kujifunzia na  kufundishia kwa watoto wenye  mahitaji maalum  sanjari na  kupeleka walimu wa kutosha wenye  ujuzi wa  kufundisha elimu maalum, itasaidia  kuondoa adha kwa wanafunzi  wa kundi hilo.

Alisema lengo ni kuhakikisha kuwa watoto wenye mahitaji maalum wanapata  fursa ya kupata haki yao ya msingi ya kusoma bila  kubaguliwa wala kuathiriwa na hali ya ulemavu  wao katika kupata elimu.

Akiunga mkono hoja hiyo, Diwani wa  Kata ya  Itigi mjini,  Ally Minja alisema kuwa suala la uwekezaji wa kudumu wa miundombinu ya majengo katika Shule mchanganyiko Mlowa haliepukiki kwa kuwa ndio shule pekee inayohudumia watoto wenye ulemavu katika halmashauri hiyo.

"Hii adha ya walemavu haiwahusu watoto wanaotoka mbali tu lakini hata wazazi walio karibu na shule hii bado wana kazi ya kumpeleka shule na kumrudisha nyumbani mwanafunzi mwenye ulemavu kwa kuwa hawezi kwenda shule na kurudi nyumbani peke yake hivyo kuna haja  kubwa  ya mabweni " alieleza

 

Alisema hivi sasa wazazi wengi wamehamasika kuwapeleka shule watoto wao wenye ulemavu baada ya kuona mabadiliko chanya kwa wale waliosoma na  ndio maana  hawawafichi tena majumbani hivyo ni jukumu ya halmashauri kuweka mazingira mazuri ya shule ili kutowakatisha tamaa.

Ofisa elimu ya msingi wa halmashauri hiyo, Doreen Lutahanamilwa alisema dhamira ya Serikali ni kuhakikisha kila mtoto anapatiwa elimu, bila kujali hali yake ya maumbile; hivyo kila halmashauri imeagizwa watoto wote wenye umri wa kwenda shule  kuandikishwa.

"Baada ya kufanya zoezi hili, tulibaini idadi kubwa ya watoto wenye mahitaji maalum wanaopaswa kwenda shule; hivyo tunakusudia kufungua Vituo vingine viwili vya Idondyandole na Mgandu. Aidha, tumebaini watoto hao wakiwekwa pamoja wanajisikia furaha".

Kikao hicho maalum cha baraza la madiwani kilipitisha jumla ya sh bilioni 22.75 ikiwa ni bajeti ya halmashauri hiyo kwa mwaka wa fedha 2021/22. 

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527

0/Post a Comment/Comments