MBUNGE KEMBAKI : HATA TUKIVAA BARAKOA KAMA MUNGU HAYUPO PAMOJA NA SISI NI BURE


Aliyenyoosha mkono ni Mchungaji wa Kanisa la Waadventista Wasabato mtaa wa Majengo wilayani Tarime akifanya maombi maalumu kumwombea Mbunge wa Jimbo la Tarime Mjini Michael Kembaki (aliyevaa tai nyekundu). Picha na Dinna Maningo
Aliyenyoosha mkono ni Mchungaji wa kanisa la Waadventista Wasabato mtaa wa Majengo wilayani Tarime akifanya maombi maalumu kumwombea Mbunge wa Jimbo la Tarime Mjini Michael Kembaki (aliyevaa tai nyekundu).
Mbunge wa Jimbo la Tarime Mjini Michael Kembakiakizungumza na waumini wa kanisa la Waadventista Wasabato mtaa wa Majengo wilayani Tarime 
Mbunge wa Jimbo la Tarime Mjini Michael Kembaki akizungumza na waumini wa kanisa la Waadventista Wasabato mtaa wa Majengo wilayani Tarime 
Walioketi mbele katikati ni Mbunge wa jimbo la Tarime Mjini Michael Kembaki, wa kwanza kulia ni katibu Mwenezi wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) wilayani Tarime Marema Sollo na wa kwanza kushoto ni Diwani wa Kata ya Kenyamanyori Farida Joel wakiwa kwenye ibada katika kanisa la Waadventista Wasabato Nkende ambapo walishiriki pia katika harambee ya kuchangia ujenzi wa kanisa
Wa Kwanza kulia ni Mbunge wa jimbo la Tarime mjini Michael Kembaki,anayemfuatia ni Makamu Mwenyekiti wa Halmashauri ya mji Tarime Thobias Ghati na wa tatu kulia ni Diwani wa Kata ya Turwa Chacha Marwa wakiwa kwenye ibada Kanisa la Waadventista Wasabato Majengo.

***
Na Dinna Maningo, Tarime
Mbunge wa Jimbo la Tarime mjini Michael kembaki amesema kuwa Mungu ndiye tumaini la Watanzania hata watu wakivaa barakoa kama Mungu hayupo pamoja nao ni kazi bure na kwamba ni vyema kuzidi kuombeana na kuliombea Taifa ili mwenyezi Mungu aepushe janga la Corona.

Kembaki aliyasema hayo wakati akichangia sh. milioni mbili ya ujenzi wa nyumba ya Mchungaji wa Kanisa la Waadventista Wasabato mtaa wa Majengo ikiwa ni sehemu ya utekelezaji wa ahadi yake huku akiwa ameambatana na Katibu Mwenezi wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) Marema Sollo, Makamu Mwenyekiti wa Halmashauri ya mji Tarime ambaye pia ni Diwani wa kata ya Nyamisangura Thobias Ghati na Diwani wa kata ya Turwa Chacha Marwa.

Mbunge huyo aliwaomba waumini hao kuzidi kuliombea taifa dhidi ya janga la Corona ambalo limesababisha hofu kwa wananchi huku akiwapongeza waumini hao kwa kutovaa barakoa na kuweka tumaini lao kwa Mungu.

"Nawashukuru sana kwa jinsi mnavyoliombea taifa Mungu ndiye tumaini letu bwana asipoulinda mji yeye aulindaye akesha bure, hata tukivaa barakoa kama Mungu hayupo pamoja na sisi ni bure, nimefurahi sijaona muumini hata mmoja aliyevaa barakoa.

"Kuna kanisa nilienda nikakuta asilimia 80 wamevaa barakoa na mimi nilikuwa sina barakoa ilinipa hofu sana, Mungu ndiye tumaini letu tuzidi kuliombea taifa letu ili lipite kwa ushindi katika janga hili ,mungu aliyetuepusha na janga hili wakati ule ndiye huyo huyo atatuokoa na janga hili",alisema Kembaki.

Mzee wa Kanisa la Majengo Simon Andrea alimshukuru mbunge kwa kutekeleza ahadi na kusema kuwa mtaa wa Majengo hauna nyumba ya mchungaji hivyo fedha hizo zitasaidia kuanza kujenga msingi kwa kuwa tayari wameshanunua uwanja.

"Mbunge katimiza ahadi yake mungu ambariki kuna watu wanatoa ahadi lakini hawatimizi, Mchungaji wetu anaishi nyumba ya kupanga kwa fedha hizi zitatusaidia kwenye hatua ya ujenzi nikuombe tutakapokuomba tena msaada tusikie na tusaidie", alisema Andrea.

Baada ya Mbunge huyo kuzungumza na waumini mchungaji wa mtaa wa Majengo Kumba Kihiri alifanya maombi maalumu kwa mbunge huyo ili mwenyezi mungu amuongoze katika kazi zake za kuwatumikia wananchi na familia yake pamoja na kumpatia afya njema.

Wakati huo huo, Mbunge Kembaki amechangia milioni 2.5 katika harambee ya kuchangia ujenzi wa kanisa la Nkende ambapo mgeni rasmi katika harambee hiyo alikuwa mbunge wa viti maalumu Ghati Chomete aliyechangia sh.milioni mbili na Mwenyekiti wa CCM mkoa wa Mara Samwel Keboye (Namba tatu) akichangia mifuko 50 ya saruji.

Baadhi ya viongozi wengine waliochangia fedha na saruji ni Mwenyekiti wa Halmashauri ya mji Tarime ambaye pia ni Diwani wa Kata ya Nkende Daniel Komote alichangia sh.500.000,Makamu Mwenyekiti wa Halmashauri hiyo Thobias Ghati alichangia 100,000 na Marema Sollo akichangia mifuko mitano ya Saruji.

Mwenyekiti wa CCM mkoa wa Mara Samwel Keboye aliwapongeza wabunge hao Madiwani na wana CCM kwa kujitolea kusaidia shughuli za kanisa, aliwaomba kuendelea kusaidia makanisa na misikiti mbalimbali pale kunapohitajika msaada Kwani kwakufanya hivyo Mungu atabariki na akawakumbusha waumini kuliombea Taifa lililokumbwa na Janga la Corona.

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527

0/Post a Comment/Comments