BALOZI DKT. BASHIRU ALLY AAPISHWA IKULU....ATOA AHADI 3 ... 'MSHTUKO WA UTEUZI HAUNIPI KUSEMA MENGI'

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mheshimiwa Dkt.John Pombe Magufuli akimuapisha Balozi Dkt. Bashiru Ally Kakurwa kuwa Katibu Mkuu Kiongozi katika hafla fupi iliyofanyika Ikulu jijini Dar es Salaam leo tarehe 27 Februari 2021.
Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mheshimiwa Dkt.John Pombe Magufuli akishuhudia Kamishna wa Maadili Jaji wa Mahakama ya Rufani, Sivangilwa Sikalaliwa Mwangesi kushoto alipokuwa akiongoza Kiapo cha Maadili kwa Viongozi wa Umma kwa Katibu Mkuu Kiongozi Balozi Dkt. Bashiru Ally Kakurwa mara baada ya kuapishwa Ikulu jijini Dar es Salaam.
Picha na Ikulu

Habari na  Elias Msuya - Mwananchi
 Katibu mkuu kiongozi, Balozi Bashiru Ally ameapishwa kushika wadhifa huo leo Jumamosi Februari 27, 2021 Ikulu Dar es Salaam na kuahidi mambo matatu ikiwemo kuimarisha mawasiliano kati ya Serikali na wananchi.

Dk Bashiru ambaye pia ni katibu mkuu wa CCM, aliteuliwa na Rais John Magufuli jana Ijumaa Februari 26, 2021 kuwa balozi na katibu mkuu kiongozi kuchukua nafasi ya aliyekuwa katibu mkuu kiongozi, Balozi John Kijazi aliyefariki dunia Februari 17, 2021.

“Hii ni mara ya pili kunipa fursa maalum, kwanza ndani ya chama chetu na sasa hivi ndani ya Serikali. Imani hiyo nitailipa kwa imani, nikuombee kwa mwenyezi Mungu akupe nguvu, hekima na busara iendelee kutuongoza kwa ujasiri kama unavyofanya,” amesema Dk Bashiru akimwambia Rais Magufuli.

Amesema atatekeleza maelekezo ya Rais Magufuli ikiwa pamoja na umuhimu wa mawasiliano Serikalini na kati ya Serikali na umma.

“Hili nitalisimamia ili kuhakikisha kwamba Serikali inafanya kama timu moja kupitia watumishi wa umma, idara, wizara inatoa taarifa kwa haraka kwa wananchi,” amesema.

Pia amesisitiza kuendeleza uzalendo, uadilifu na utumishi kwa wananchi hasa katika kutatua kero zao.

Jambo la tatu alizosisitiza ni umuhimu wa kusimamia haki na kusisitiza wajibu wakila mmoja.

“Umezungumza umuhimu wa vyombo vinavyohusika kuhakikisha kwamba kila uamuzi tunaofanya unazingatia haki hususani haki za wanyonge.”

“Kama ni suala ushuru kodi au tozo mbalimbali, utaratibu wa kisheria unazingatiwa lakini pia kusimamia uwajibikaji ili nchi yetu ipige hatua za kutosha,” amesema.

Akizungumzia uteuzi huo, Dk Bashiru amesema hakutegemea kwani tayari Rais alikuwa amempa majukumu mengine ya CCM na alikuwa akijiandaa kuyatekeleza.

“Jana jioni nipo nasoma mafaili yangu napata taarifa kuwa umeniteua. Mshtuko huo haunipi kusema mengi. Bado natafakari sana.

“Nitafanya nini nitafanya vipi kukidhi matarajio yako kwa imani uliyonipa kwa mfululizo. Niwaombe Watanzania wote mniombee niweze kukidhi matarajio ya Rais,” amesema.

Via Mwananchi

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527

0/Post a Comment/Comments