HEWA YA UKAA YAWAPAISHA KIUCHUMI WANANCHI WILAYA YA TANGANYIKA


Mwakilishi wa Carbon Tanzania Bw. Frank Kweka akimkabidhi Hundi yenye thamani ya shilingi 225,000,000/- Mkuu wa Mkoa wa Katavi Mhe Juma Z. Homera. Fedha inatokana na mauzo ya hewa ya ukaa
Mkuu wa Mkoa wa Katavi Mhe Juma Z. Homera akimkabidhi hivi karibu ni Hundi yenye thamani ya shilingi 225,000,000/- Mwenyekiti wa Kijiji cha Katuma Bw. Masanja Nchimani. Fedha hiyo inatokana na mauzo ya hewa ya ukaa.
Mkuu wa Mkoa wa Katavi Mhe Juma Z Homera akimkabidhi Hundi yenye thamani ya shilingi 25, 000, 000/- Mkurugenzi wa Halmashauri ya Wilaya ya Tanganyika Rojas Rumuli. Fedha hiyo inayotokana na mauzo ya hewa ya ukaa, ni kwa ajili ya shughuli za usimamizi Halmashauri ya Tanganyika
Mkuu Ofisi wa Mkoa wa Katavi Mhe Juma Zuber Homera akishiriki upandaji wa miti ili kutunza mazingira Mkoani kwake
***

Na William Budoya, Afisa Habari Mkuu, Ofisi ya Mkuu wa Mkoa Katavi

Hewa ya ukaa ni biashara poa na inalipa. Kazi kubwa unayotakiwa kufanya ili uweze kufanya biashara hii ni kuhifadhi mistu ya asili iliyo katika eneo lako na kutunza mazingira yako. Misitu ya asili ina uwezo mkubwa wa kufyonza na kuhifadhi hewa ya ukaa na hewa sumu.

Ukiwa na misitu hii lazima uzuie uharibifu wa misitu mfano kukata miti, kufyeka miti, kuchoma misitu na kufanya shughuli zingine hatarishi kwa uhifadhi wa misitu na kupanda miti mbali mbali katika maeneo yetu. Ukiweza kufanya hayo lazima utakuwa na uhakika  wa kuvuna hewa ya ukaa na kufanya biashara ya hewa ya ukaa.

Pengine unaweza kujiuliza, je biashara hii ni kama biashara ya mahindi au biashara nyingine? Kwamba mtu anaweza kupanda na kuvuna mahindi na kuuza sokoni? Hapana sivyo. Katika biashara hii mwenye biashara anatakiwa kuhifadhi misitu asili iliyo katika eneo lake. Aidha akishafanya uhifadhi huo basi, Carbon Tanzania watamtafutia wateja duniani wa kutoa ruzuku kwa uhifadhi huo.  

Biashara hii imeshaingia katika Mkoa wa Katavi, Wilaya ya Tanganyika katika Halmashauri ya Wilaya ya Tanganyika. Wananchi 21,000 katika vijiji 8 walio katika Halmashauri ya Wilaya ya Tanganyika, wamenufaika na mradi wa hewa ya ukaa baada ya kuivuna hewa hiyo na kupewa kiasi cha shilingi 380,000,000/= na Carbon Tanzania chini ya mradi uitwao NTAKATA MOUNTAINS REDD Plus PROJECT.

Wananchi katika Wilaya hiyo wamezuia uharibifu wa misitu waliyoihifadhi ili iwasaide kutunza mazingira pamoja na mambo mengine kufyonza hewa ya ukaa na hewa sumu iliyo katika la anga la nchi yetu na nje ya nchi. Kwa kufanya hivyo, wananchi katika Wilaya hiyo wametengeneza biashara ya kuuza hewa ya ukaa.

Kwa ufafanuzi, vijiji hivyo vimevuna jumla ya tani 82,000 za hewa ya ukaa na kuiuza  kwa thamani ya shilingi 250,000,000/=. Hata hivyo pamoja na uvunaji wa tani hizo, mauzo yake hayajafikia hata nusu ya tani 270 ambazo hazijauzwa bado.

Aidha 12/11/2020 na 2/5/2020 kiasi cha fedha 130,000,000/= zilitolewa kama motisha na wadau mbali mbali wa hifadhi kwa vijiji kabla ya kupata wateja na vyeti  vya uuzaji wa hewa ya ukaa na kugawanywa kulingana na makubaliano ya mradi. Makubaliano hayo yanabainisha kuwa 10% ya fedha zinazopatikana zinaenda kwenye Halmashauri ya Wilaya ya Tanganyika ili kugharimia shughuli za usimamizi wakati 90% zinapaswa kugawiwa kwenye vijiji vilivyo katika mradi ambao unakadiriwa kuwa na hekta 230 katika msitu wa Tongwe Magharibi.

Fedha hizo zilizopatikana zitasaidia kuleta maendelao ya kijamii na kiuchumi kwa wananchi mfano ujenzi wa madarasa na utengenezaji wa madawati, kujenga vituo vya Afya na kuwaletea wananchi nishati ya umeme.

Katika misitu hiyo kuna utajiri mkubwa, inaelezewa kuwa ikiwa hewa ya ukaa itauzwa kwa wingi na ukamilifu wake uliopo katika misitu ya vijiji hivyo, basi kuna uwezekano wa kupata kiasi cha 6,000,000,000/-. Wananchi wanatakiwa kuendelea kuhifadhi misitu na kutunza mazingira. Miti isikatwe ovyo wala kuchomwa, waepuke kilimo cha kuhamahama na ufugaji usiozingatia tija.

Kwa kuvitaja, vijiji vilivyonufaika na mauzo ya hewa ya ukaa, ni Lugonesi, Mwese, Lwega na Bujombe. Aidha vijiji vingine vilivyo katika mradi wa mauzo ya hewa ya ukaa ni Kapanga, Mpembe, Kagunga na Katuma. Baadhi ya vijiji hivyo viko katika Kata ya Mwese, Tarafa ya Mwese na vijiji vingine viko Kata ya Kasekese.

Carbon Tanzania ndio taasisi inayowezesha vijiji hivyo kupata masoko ya hewa ya ukaa ipatikanayo katika misitu ya hifadhi za vijiji na maeneo ya malisho.

Je, biashara hii imeanzaje? Biashara hii imeanza baada ya vijiji 8 kuwekwa kwenye mpango wa matumizi bora ya ardhi. Matumizi bora ya ardhi ni nini? Ni uwezo wa wananchi kujipangia namna ya kutumia ardhi yao kwa faida yao. Kwa mantiki hiyo, wananchi katika vijiji hivyo wamejipangia ardhi yao kwa mahitaji mbali mbali mfano kutenga maeneo kwajili ya kilimo, makazi, malisho na maeneo mengine kuyaacha kwa ajili ya uhifadhi misitu kwa ajili ya kuvuna na kuuza hewa ya ukaa. Matumizi bora ya ardhi ndio  chanzo cha mradi wa hewa ya ukaa . Wananchi wametenga maeneo ya hifadhi ya misiti na kuyaacha maeneo hayo kwa ajili biashara ya hewa ya ukaa. Mradi huu, unaokadiriwa kuwa na hekta 230, unajulikana kama NTAKATA MOUNTAINS REDD Plus PROJECT, ambao uko chini ya usimamizi wa Carbon Tanzania.

Malengo ya mradi huu ni kuhifadhi misitu ya asili na mazingira, kulinda na kuhifadhi  bionuai zote muhimu hasa zilizo hatarini kutoweka kama Sokwe, kukabiliana na mabadiliko ya tabia nchi, kutunza vyanzo vya maji, kutunza wanyamapori na kuwawezesha wananchi , walio katika vijiji venye uhifadhi wa misitu asili, kufanya shughuli za maendeleo yao katika vijiji vyao kupitia mauzo ya hewa ya ukaa.

 Mashuleni tunafundishwa kuwa hewa ya ukaa al maaarufu kama C02, ni muungano wa atomi 1 ya kaboni na atomi 2 za Oksijeni hutengeneza hewa ya ukaa(C02). Sisi binadamu hupumua hewa ya ukaa  na baadaye hewa hiyo hufyonzwa na miti na kuhifadhiwa kwenye miti na ardhini. Aidha sisi binadamu huvuta hewa ya oksijeni kutoka kwenye mimea.  Kwa asili hewa ya ukaa ni miongoni mwa gesi zilizopo angani. Hewa kwa kawaida ina gesi mbali mbali ikiwemo hewa ya ukaa.

Hewa ya ukaa ni hewa chafu zinazozalishwa na shughuli mbali mbali za mwanadamu. Uzalishaji mkubwa wa kaboni angani huchochea athari ya jopogesi na kusababisha mabadiliko ya tabia ya nchi. Ongezeko la viwango vya hewa ya ukaa na gesi nyingine angani zinazotokana na shughuli za binadamu husababisha kiwango cha joto duniani kuongezeka.

Mabadiliko haya yana maana gani? Mabadiliko haya yana maana ya kuongezeka kwa jotoridi, kuwa na misimu ya mvua isiyoaminika, kupata mvua chache, utabiri wa majira kuwa mgumu, makali ya ukame na mafuriko kuzidi, mvua kunyesha nje ya misimu iliyozoeleka. Aidha kuna athari katika kilimo, uzalishaji wa chakula kupungua kwa sababu ya uhaba wa mvua na ongezeko kubwa la joto, milipuko ya magonjwa na wadudu waharibifu wa mazao waweza kusambaa hata maeneo ambayo hawakuwemo awali. Ongezeko la joto duniani limesababisha kuyeyuka kwa theluji katika ncha za duniani ambayo inasababisha ongezeko la kima cha bahari.

Binadamu nao huongeza hewa ya ukaa angani kwa kasi zaidi kuliko uwezo wa dunia kufyonza gesi hii. Uchomaji wa mimea husababisha hewa ya ukaa kwenda angani katika hali ya moshi, ukataji wa misitu kwa sababu mbali mbali hupunguza uwezo wa ardhi kuhifadhi hewa ya ukaa, tunapochoma mafuta, kuendesha magari yetu na wakati wa kuzalisha umeme.

Hali hiyo ni hatari kwa maisha ya mwanadamu. Sasa tunafanyaje ili kukabiliana na mabadiliko ya tabia nchi?

Watalaam wamefanya tafiti na kubaini kuwa njia pekee inayoweza kukabiliana na mabadiliko ya tabia nchi ni uhifadhi wa misitu ya asili. Misitu ya asili ina uwezo mkubwa wa kutumia hewa ya ukaa na hewa sumu kama chakula chake. Miongoni mwa vyakula ambavyo miti hutumia ni hewa sumu zinazotokana na viwanda na zile zingine ambazo binadamu anazalisha. Miti inapotumia hewa ya ukaa inatoa hewa ya oksijeni ambayo hutusaidia sisi binadamu kuvuta. Misitu ya asili iliyopo Halmashauri ya Tanganyika ni miongoni mwa misiti iliyo na uwezo wa kukabiliana na mabadiliko ya Tabia nchi.

 Misitu hiyo ndio imekuwa msitu wa kwanza ya kitropiki Afrika kufanikiwa kuuza hewa ya ukaa. Hii ina maana kwamba kumbe inawezekana kuwa na misitu mbali mbali katika nchi yetu  kuwekwa kwenye utaratibu wa kuuza hewa ya ukaa na ikanufaisha zaidi siyo nchi yetu tu kwa kiwango kikubwa zaidi bali na Bara la Afrika mfano DRC Congo.

Wananchi waliopo Mkoani Katavi na watanzania wote na Bara la Afrika hatuna budi kuhifadhi misitu na kutunza mazingira yetu kwa manufaa yetu na vizazi vijavyo. Tuendelee kutunza mazingira yetu kwa kupanda miti mbali mbali(mfano Korosho, Mipeini) kwa ajili ya kutunza mazingira na kuongeza uchumi na kuzingatia kanuni mbali mbali za kutunza mazingira.    


Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527

0/Post a Comment/Comments