YANGA SC YAIBABUA MWADUI FC 5 - 0 UWANJA WA KAMBARAGE

YANGA SC wameendeleza wimbi la ushindi katika Ligi Kuu ya Tanzania Bara baada ya kuwachapa 5-0 wenyeji, Mwadui FC Uwanja wa Kambarage mjini Shinyanga.Mabao ya Yanga SC leo yamefungwa na kiungo mzawa Deus Kaseke dakika ya sita, mshambuliaji Mburkinabe Yacouba Sogne dakika ya 14 na 49 na winga Mkongo Tuisila Kisinda dakika ya 57 na beki Mghana, Lamine Moro dakika ya 70.

Kwa ushindi huo, Yanga SC inayofundishwa na kocha Mrundi, Cedric Kaze imefikisha pointi 37 katika mechi ya 15 na sasa inaongoza Ligi Kuu kwa pointi 10 zaidi ya Azam FC inayofuatia, wakati mabingwa watetezi, Simba SC ni wa tatu wakiwa na pointi 26 za mechi 12.
Katika mchezo huo uliochezeshwa na refa Ahmada Simba wa Kagera aliyesaidiwa na Rashid Zonga wa Iringa na Credo Mbiya wa Mbeya, winga wa zamani wa AS Vita ya Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo (DRC), Kisinda alishindwa kumalizia mechi baada ya kuumia na nafasi yake kuchukuliwa na Ditram Nchimbi zikiwa zimebaki dakika 10 na ushei.

Mechi nyingine za Ligi Kuu leo, Polisi Tanzania imelazimishwa sare ya bila kufungana na Ruvu Shooting Uwanja wa Ushirika mjini Moshi mkoani Kilimanjaro, wakati bao pekee la Seif Abdallah Karihe dakika ya 47 limeipa Dodoma Jiji FC ushindi wa 1-0 dhidi ya Gwambina Uwanja wa Jamhuri mjini Dodoma.

Kikosi cha Mwadui FC kilikuwa; Mussa Mbisa, Mfaume Omar, Issa Shaaban, Khalfan Mbarouk, Joram Mgeveke, Abbas Kapombe, Abubakar Kambi, Merckiard Mazellah/Deogratius Anthony dk54, Erick Nkhosi, Ismail Ally na Herman Masenga. 

Yanga SC; Metacha Mnata, Kibwana Shomari, Yassin Mustapha, Lamine Moro, Bakari Mwamnyeto, Mukoko Tonombe, Tuisila Kisinda/Ditram Nchimbi dk79, Feisal Salum, Michael Sarpong, Deus Kaseke/Haruna Niyonzima dk61 na Yacouba Sogne/Farid Mussa dk67.

 CHANZO - BINZUBEIRY BLOG

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527

0/Post a Comment/Comments