WAZIRI MKUU APOKEA VYUMBA 14 VYA MADARASA


 WAZIRI MKUU Kassim Majaliwa amepokea vyumba 11 vya madarasa, ofisi mbili za walimu, samani na chumba maalumu cha wasichana vilivyojengwa na Benki ya TPB PLC katika shule ya msingi Nandagala wilayani Ruangwa, Lindi kwa gharama ya shilingi milioni 164.902.

Amepokea mradi huo wa ujenzi na ukarabati wa vyumba vya madarasa leo (Jumatatu, Desemba 28, 2020) alipotembelea shule hiyo akiwa katika ziara yake ya kikazi wilayani Ruangwa. Waziri Mkuu ameupongeza uongozi wa benki hiyo.

Waziri Mkuu amewataka wazazi, walimu na wanafunzi wahakikishe majengo hayo yanatunzwa ili yaweze kutumika kwa muda mrefu. “Tunataka majengo haya kama yalivyo leo yaendelee kuwa hivihivi. Tuyatunze haya majengo, Wanafunzi msifanye majaribio ya kuandika ukutani wala kupiga chapa ya miguu kwenye ukuta. Tunawashukuru TBP kwa kutukabidhi madarasa haya ambayo manne ni mapya na saba yamekarabatiwa.”

Akizungumzia kuhusu ufaulu, Waziri Mkuu amesema kati ya wanafunzi 63 waliofanya mtihani wa darasa la saba mwaka huu katika shule hiyo 57 wamefaulu na sita tu ndio hawakufaulu. Ameagiza watoto wote waliofaulu wapelekwe shule na wale sita waliosalia watapelekwa chuo cha VETA kinachotarajiwa kufungulia mwaka 2021 wilayani Ruangwa.

Awali, Mkurugenzi Mkuu wa TPB Bank PLC, Sabasaba Moshingi alisema utekelezaji wa mradi huo ni muendelezo wa mpango wa benki hiyo wa kurejesha sehemu ya faida wanayoipata kwa jamii kupitia miradi mbalimbali ya maendeleo ikiwemo ya ujenzi wa miundombinu ya elimu na afya.

Alisema mradi huo ulihusisha ukarabati wa vyumba saba vya madarasa pamoja na ujenzi wa vyumba vipya vya madarasa vinne, ofisi mbili za walimu, stoo, ukarabati wa matundu 28 ya vyoo, ujenzi wa chumba maalumu cha wasichana pamoja na utengenezaji wa samani za walimu ikiwa ni pamoja na meza 13 na viti 13.

Naye Mwenyekiti wa kamati ya ujenzi wa mradi huo Hamza Mkuyanda alisema kukamilika kwake kumeleta manufaa mengi yakiwemo mazingira bora ya kuvutia katika ufundishaji na ujifunzaji kwa walimu na wanafunzi na hivyo kuongeza kiwango cha taaluma shuleni hapo.

Pia, Waziri Mkuu alipokea vyumba vitatu vya madarasa na chumba kimoja cha walimu vilivyojengwa na wadau wa elimu katika shule ya msingi Mkata iliyoko kijiji cha Namahema wilayani Ruangwa kwa thamani ya shilingi milioni 76.


Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527

0/Post a Comment/Comments