NYONGO ATAKA AJIRA ZA MGODI MPYA ZITOLEWE KWA WAZAWA


 Na Issa Mtuwa – Singida
Mgodi mpya wa Singida Gold Mine, uliozinduliwa mkoani  Singida, wilayani Ikungi umeagizwa  kuzingatia utoaji wa ajira za wafanyakazi mgodi hapo huku kipaumbele kikiwa kwa wananchi wanaozunga mgodi huo. 


Hayo, yalisemwa na Naibu Waziri wa Madini Stanslaus Nyongo katika hafla ya uzinduzi wa ujenzi wa mgodi huo tarehe 16 Octoba, 2020. Ameongeza kuwa uwepo wa mgodi huo utakuwa chachu ya maendeleo kwa Wanasingida na nchi nzima kwa ujumla. 


Nyongo alisema, kwenye mgodi huo una fursa nyingi zitakazotolewa kwa wananchi kushiriki mambo mbalimbnali ndani na nje ya Mgodi alitoa mfano; biashara, ulinzi, ajira rasmi na ajira zisizo rasmi. Aliongeza kuwa kodi itakayolipwa na mgodi kwenye Halmashauri fedha zake zitakwenda kutumika kwa ajili ya maendeleo Ikungi.


Akizungumzia ulipaji wa maduhuli ya Serikali, Nyongo alisema, Wizara ya Madini iko mstari wa mbele kuchangia pato la Serikali. Mwaka jana tulipangiwa kukusanya bilioni 470, mpaka kufikia mwisho wa mwaka, Wizara iliweza kukusanya kiasi cha bilioni 528. Mwaka huu 2020/2021 Wizara imepangiwa kukusanya maduhuli ya Serikali bilioni 526.9 


Mtendaji Mkuu wa Tume ya Madini, Prof. Shukran Manya, aliemuwakilisha Katibu Mkuu wa Wizara ya Madini, alisema kuzinduliwa kwa mgodi huo, kunaongeza wigo wa kukusanya maduhuli ya Serikali ambayo yanakusanywa na Tume ya Madini. Hivyo kuwe na mpango waharaka wa kuanza kuzalisha.


Meneja Mkuu wa Singida Gold Mine, Filbert Rweymamu, alimwambia Mgeni rasmi Naibu Waziri wa Madini, kuwa mgodi umejipanga kushirikiana na Wanaikungi na kuweka mipango ya kuwainua wananchi kimaendeleo. Alisema wamepanga kutoa ajira kwa wafanyakazi 200 kipaumbele kikiwa wananchi wa Ikungi na Singida. 


Kuhusu kushirikia na wachimbaji wadogo, mgodi umepanga kutoa mafunzo ya wachimbaji wadogo kuhusu namna ya uchimbaji salama katika maeneo yao.  


Akizungumzia mchango kwa taifa, Rweymamu alisema wanazingatia sheria mpya ya madini inayoipa Serikali kwa niaba ya wananchi,  umiliki wa asilimia kumi na sita (16% free carried interest) watazilipa kodi kama zitakavyobainishwa. 


Mkuu wa Mkowa wa Singida, Dkt. Rehema Nchimbi, alisema amefurahi kuzinduliwa ujenzi huo ili uanze uzalishaji. Uzalishaji utakapoanza anategemea vijana wa Singida hawatakuwa na muda kwenda Dodoma Makao Makuu kwakuwa ajira hapa zitakuwa za kutosha kwa watakao ajiriwa ndani na wengine watajiajiri kwa kupeleka bidhaa na huduma mgodini.


Kwa Wananchi kwa nyakati tofauti, wamefurahia kuzinduliwa mgodi huo kwani wanamatumaini kwa kuwa kutakuwa nafursa nyingi zitakazo tolewa. Wameomba fursa za mgodi wapewe kipaumbele  wanaozunguka mgodi. 


Waziri  wa Madini, Doto Biteko aliwahi kusema; Geita kuna dhahabu lazima dhahabu iwanufaishe wana Geita, Tanga kuna Vipepeo vya kipekee ambapo watalii hufika kuviangali, Vipepeo hivyo lazima viwanufaishe Wanatanga, Shinyanga kuna Almasi, lazima Almasi hiyo iwanufaishe Wanashinyinga, hata Korosho kule Mtwara lazima ziwanufaishe Wanamtwara. Kwa maelezo ya Biteko, dhahabu hii ya Singida lazima iwanufaishe watu wa Singida kutokana na fursa ya uwepo wa dhahabu.




Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527

0/Post a Comment/Comments