AIRO AWASHUKIA WANAODAI HAMUUNGI MKONO CHEGE....ASEMA NI NJAMA ZA WAPINZANI KUWACHONGANISHA WANA CCM


Lameck Airo akiwazawadia watoto waliokuwa wakicheza ngoma ya utamaduni


Na Dinna Maningo,Rorya
Kitendo cha Makada wa CCM wilayani Rorya na waliokuwa wametia nia ya ubunge kuzidi kumwombea kura mgombea Ubunge jimbo la Rorya mkoani Mara Jafari Chege kimezidi kuwaweka njia panda vyama vya upinzani hali ambayo imesababisha baadhi kufanya uchonganishi wenye lengo la kukisambalatisha kikosi kinachoomba kura kwa wananchi.

Imeelezwa kuwa kuna baadhi ya wapinzani wamekuwa wakieneza uvumi kupitia mitandao ya kijamii ukiwemo wa Rorya Foram na kwa Chege kuwa aliyekuwa mbunge wa Rorya kupitia CCM Lameck Airo na Baadhi ya Watiania akiwemo Francis Olwero hawamuungi mkono Jafari huku wakishawishi Jafari awapige chini baadhi ya wanaomwombea kura akiwemo Airo.

Akizungumza kwenye uzinduzi wa Kampeni za mgombea Udiwani kata ya Nyamtinga Charles Chacha katika kijiji cha Nyarombo,aliyekuwa mbunge wa jimbo hilo na mgeni rasmi katika uzinduzi huo Lameck Airo alisema kuwa njama hizo zinasukwa na wapinzani kwa lengo la kuwadhoofisha kisiasa ili wapinzani wapate mwanya kushinda kwenye uchaguzi.

"Wanasema kwamba mimi sizunguki na Chege lakini kuna maeneo tumekuwa tukifanya kampeni tukiwa na Chege na wananchi ni mashahidi na hata maeneo ambayo tunapiga kampeni bila kuwa na Chege bado tukisimama jukwaani tunamwombea kura Chege na wagombea wengine wa CCM tunatumia gharama zetu kuzunguka.

Aliongeza" huo mtandao wa Rorya Foram una wapinzani wengi na ndiyo hao walisema wanataka mgombea msomi,CCM kwakuwa ni chama kinachosikiliza maoni ya watu wakamleta Chege lakini bado watu wanaendelea kutuchonganisha na Chege ili tuchukiane na tukichukia watia nia wakasirike waache kupiga kampeni abaki Jafari mwenyewe, akibaki yeye mwenyewe inakuwa ni njia rahisi kwa wapinzani kupenya."alisema Airo.

Airo alisema kuwa katika kipindi hiki cha uchaguzi yatasemwa mengi lakini hayatamkatisha tamaa nakwamba atapambana kuhakimisha CCM inashinda ambapo alisema atatafuta kura kwa kutumia njia mbalimbali zikiwemo za kupiga kampeni za chini kwa chini.

"Mimi siyo  mtu wa majukwaani hata nisipoongozana na Chege nina mbinu zangu nyingi za kupiga kampeni,mimi napiga kampeni za chini kwa chini,kampeni za usiku,kampeni za vikundi mimi ndiyo Airo CCM tutashinda tuu,maneno ya wapinzani kwenye mitandao ya kijamii hayanisumbui nayasikia nayapuuza sisi tunapambana kutafuta kura na siyo manenomaneo" alisema Airo.

Airo alisema kuwa ataendelea kumuunga mkono Chege" mimi nilikuwa spidi 100 Chege ataenda spidi 500 kwanza ana elimu ana nafasi yakuwa Waziri,mimi ni elimu ya la saba nilikuwa nimebania Rorya nafasi ya uwaziri kwa miaka 10 tuombe Mungu tushinde kwa kishindo ili Rais wetu akiona basi atupe upendeleo Rorya Chege awe Waziri"alisema Airo.

Akimwombea kura mgombea Udiwani kupitia chama hicho Charles Chacha anayetetea kiti hichi aliwaomba wananchi kumchagua Chege  na Chacha bila kumsahau Rais Magufuli kwa kile alichoeleza kuwa Serikali ya awamu ya tano imefanya maendeleo mengi na wananchi ni mashahidi.

Akizungumza na Malunde 1Blog mtiania ya ubunge ambaye kura zake hazikutosha Francis Olwero alisema"Kumekuwa kukienezwa habari za uzushi kuwa mimi namshika miguu Chege nimepewa milioni 15 na wapinzani kumwangusha,ni uongo mtupu mimi tangu kampeni zimeanza tuko na wenzangu tumeacha familia zetu Dar na kazi zetu kwa ajili ya kupambana kumwombea kura Chege.

Aliongeza" hizi ni njama za wapinzani na baadhi ya wana CCM wanaokishika chama miguu kutaka  tukate tamaa kumwombea kura mwenzetu, wanatushonganisha nae,sitakata tamaa maana nilisema nitamwombea kura mwenzangu Dar nitaenda na matokeo ya ushindi wa Chege, kwenye kampeni yanasemwa na yatazushwa mengi wao waendelee kusema kama nilipewa pesa waje  kwenye chama watoe ushahidi"alisema Olwero.

Mgombea Udiwani kata ya Nyamtinga Charles Chacha aliwaomba wananchi kumchagua tena ili aendelee kufanya maendeleo huku akiwaeleza mambo mbalimbali aliyoyafanya akiwa Diwani miaka mitano iliyopita.

"Kata yangu tumefanya maendeleo mengi kwa michango ya harambee tumejenga maboma 4 ya shule ya Sekondari matundu 30 ya vyoo katika shule zetu,tulipokea fedha milioni 175 za maendeleo,tumejenga nyumba za walimu,shule ya Rwang'enyi tumejenga madarasa 3,ofisi ya walimu nakupeleka milioni 7,mradi wa maji Nyarombo wa milioni 847,kijiji cha Manila madarasa 4 mradi wa umeme wa Rea uliogharimu milion 250" alisema Chacha.

Baadhi ya wagombea udiwani kata mbalimbali na wagombea udiwani viti maalumu walimwombea kura Chacha huku wakimwagia sifa kutokana na maendeleo aloyoyafanya akiwa Diwani.

Mwenyekiti wa CCM kata ya Nyamtinga Galus Oyieko alimwomba Airo kuwatengenezea barabara ya kutoka Mwalango hadi Rwang'enyi na alimtaka mgombea udiwani atakaposhinda ahakikishe anatoa hoja halmashauri ili ujenzi wa shule ya Sekondari Rwang'enyi ukamilike kwa wakati.


Walioketi mbele, kulia ni Mgombea Udiwani Kata ya Nyamtinga Charles Chacha katikati ni Lameck Airo aliyekuwa mbunge wa jimbo la Rorya wakiwa kwenye uzinduzi wa kampeni za mgombea udiwani
Kushoto ni Lameck Airo akimnadi mgombea udiwani kata ya Nyamtinga Charles Chacha
Kikundi cha kwaya kikitumbuiza wakati wa uzinduzi wa kampeni za mgombea Udiwani kata ya Nyamtinga
Wananchi wakiwa kwenye mkutano wa uzinduzi wa kampeni za mgombea udiwani
Wana CCM wakimpongeza mkazi wa Nyamtinga aliyekuwa akiigiza kusoma taarifa ya habari

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527